Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kutoa mchango wangu. Naomba nianze kutoa pongezi kwa Serikali yetu kwa kazi nzuri sana inayofanyika katika kudumisha na kuboresha huduma za afya, hongera sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama unavyofahamu sote tumeshuhudia bajeti ya dawa imeongezeka kutoka bilioni 30, mpaka bilioni 270 hili siyo jambo dogo. Nachukua nafasi hii kumpongeza pia Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayofanya kusimamia sekta ya afya, nawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti,achukua nafasi hii pia kuwapongeza Wataalam wetu wanaosimamia MSD kwa kazi nzuri waliyoifanya na wanayoendelea kuifanya ya kusambaza madawa, wamefanya mambo mengi pale, mengi yanaonekana kwa mfano, wakinunua magari kila mtu anayaona, ni rahisi kupongeza magari yanaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo kubwa walilolifanya zaidi ya magari ni kuweka mfumo wa Car Tracking System ambao gari inapobeba dawa za MSD ikisimama popote pale dereva atapigiwa simu hapohapo na kuambiwa mbona umesisima na ulikosimama siyo sehemu tuliyokutuma. Hili ni jambo kubwa na naomba waendele kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijamaliza hatua ya pongezi nimpongeze rafiki yangu, lakini pia Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, Mheshimiwa Profesa Janabi. Mwaka 2000 nilikutana na Profesa Janabi kule Japan alikuwa anafanya PhD yake, nikamuuliza sasa hii PhD unayosoma unasomea nini, aliniambia mambo mawili, moja sitalisema kwa sababu za kitalaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, alilisema, aliniambia angependa siku moja Tanzania waweze kufanya operation ya moyo bila kupasua moyo. Nikamwambia Mzee hii inawezekana, akasema ndiyo maana niko huku na itawezekana. Sasa hiyo ilikuwa ni ndoto yake mwaka 2000 leo hii sote tunakubali hapa Profesa Janabi na wenzake wanafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu moyo wa Profesa Janabi aliouonesha kwamba unapopelekwa nje kusoma basi ukisoma uwe na jambo ambalo unasema ukirudi Watanzania watanufaika namna gani. Kwa hiyo, nampongeza sana. Nakumbuka wakati ule Profesa Janabi alijaribu kunishauri akasema sasa Mheshimiwa umekuja huku Japan kwa nini usirudi na gari Tanzania nikamwambia na mimi nina ndoto yangu, hizi posho nikizikusanya hapa nikirudi nyumbani ndogo yangu ni kwenda kuwa Mbunge na nikaitekeleza. Kwa hiyo, Profesa Janabi wakati na mimi nakupongeza ukipata fursa na wewe usisite kunipongeza kwamba ndoto zako zilitimia, lakini na ndoto za kwangu zilitimia, ndiyo maana leo hii nipo hapa, nakupongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nizungumze kwa haraka nimeshashukuru MSD. Pia namshukuru sana Mheshimiwa Waziri, nilipeleka ombi langu kwake rasmi, kwamba kituo chetu Bunazi hatuna mashine ya anesthesia breathing machine, leo hii nimepata taarifa za uhakika mashine hiyo imefika kwenye kituo na sasa mambo yote yanaenda vizuri. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote tunafahamu kuwa Tanzania tumejaliwa miti ya asili mingi tu yenye uwezo wa kutengeneza madawa, nyote mnafahamu kuna dawa moja maarufu sana inaitwa Cotecxin, lakini dawa ile inatengenezwa kwa miti inayopatikana hapa Tanzania hasa pale Iringa. Wenzetu wanachukua miti wanapeleka kule wanatengeneza dawa wanatuuzia. Tanzania tunasema tunataka kujenga nchi ya viwanda lakini kujenga nchi ya viwanda ni jambo kubwa na hasa viwanda vya madawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba Wizara ya Afya ishirikiane na Wataalam wengine kuondoa vikwazo vinavyochelewesha Tanzania kuweza kujenga viwanda vya madawa. Nina rafiki yangu Mchina amekuja kuwekeza Tanzania kwenye kiwanda cha madawa na amewekeza, lakini ilimchukua miaka miwili kupata cheti cha kusajili dawa yake wakati Kenya inachukua siyo zaidi ya miezi sita kupata cheti cha kusajili dawa. Tanzania ya viwanda ina mambo mengi, naomba tushirikiane ili kuweza kuelekea huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mpango mzuri unatekelezwa unaitwa RBF (Result Based Financing), huu mpango ni mzuri sana unasaidia katika ujenzi wa kutoa miundombinu pamoja na motisha katika vituo vyetu vya afya na hasa kuboresha huduma ya mama na mtoto. Mpango huu nimeupenda sana kwa sababu pamoja na kusaidia miundombinu unatoa motisha kwa wafanyakazi kwa 25%.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mango huo umesababisha hata Wakunga, Manesi wao wenyewe wanazunguka kutafuta nani mama mjazito anakaribia kujifungua ili aende akajifungulie kwenye kituo chake cha afya. Mpango huu ni mzuri na nashauri usambazwe kwa Tanzania nzima. Najua hivi sasa unatekelezwa katika mikoa saba, lakini mpango huu kwa kuwa umeonesha mafanikio ukisambazwa Tanzania nzima itakuwa jambo jema.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni la Bima ya Afya, natambua nimesoma kwenye hotuba kwamba sasa mpango huu wa huduma ya CHF iliyoboresha utaanza 2018, mwaka 2018 ni sasa, mpango huu utawezesha kutoa ile CHF na wananchi wataweza kutibiwa si tu kwenye kituo kile cha afya, ataweza kutiwa kwenye zahanati kwenye vituo vya afya hadi hospitali ya mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango huu ni mzuri naomba utekelezwe kwa haraka na kwa kweli mimi niko tayari hata kusitisha mambo yote lakini mpango huu ukatekelezwe. Ni kwa sababu mpango huu ndiyo utaleta ukombozi mkubwa kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nimalize kwa jambo moja na lenyewe ni kwamba MSD wanajenga pale Kairabwa ujenzi wa Kairabwa Logistics Center. Center hiyo ni muhimu naunga mkono kwa asilimia 100 na namshukuru na Mkuu wa Mkoa wa Kagera anaunga mkono mpango huu. Kwa kweli Wabunge wengi wa Mkoa wa Kagera tunaunga mkono mpango huu, naomba ifanyike haraka itakavyofanyika ili center hiyo iweze kujengwa, tuweze kuboresha huduma za afya, madawa yawafikie wananchi kwa uharaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusisitiza ule mpango CHF iliyoboreshwa, ni mzuri na utasaidia sana katika kuboresha huduma za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.