Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi nichangie hii Wizara ya Afya.

Kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu na watendaji wote wa Wizara ya Afya. Naipongeza Hospitali ya Wilaya ya Mpwapwa, madaktari na wauguzi wanafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Afya ina kurugenzi kubwa mbili; kwanza Kurugenzi ya Tiba na Kurugenzi ya Kinga. Mimi niongelee kwanza Kurugenzi ya Tiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zahanati, vituo vya afya na hospitali, ili iitwe hospitali ni dawa pamoja na watumishi. Naipongeza sana Serikali kwa kujitahidi kutenga fedha za kutosha kwa ajili ya kununua dawa. Naipongeza MSD kwa kununua dawa za kutosha na kununua magari ya kusambaza dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Mheshimiwa Waziri wa Afya, hii fedha ya kununua dawa bado haitoshi. Tuendelee kuongeza hela ya kununua dawa. Hii ni kwa sababu kama alivyosema Mwenyekiti, hizi dawa kweli zinasambazwa lakini kuna baadhi ya zahanati dawa hazifiki, sasa hii inakuwa ni shida. Kwa hiyo, MSD mna Kanda, hakikisheni Mameneja wenu wanatembelea kwenye zahanati na vituo vya afya wanakagua kama kweli dawa hizi zinawafikia wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upungufu wa watumishi, kama nilivyosema Wizara ya Afya ilikuwa na mpango wa kuongeza Vyuo vya Clinical Officers na Clinical Assistants. Sasa kwa nini upungufu wa watumishi unaendelea? Kwa mfano, pale Mpwapwa kuna Chuo cha Afya, lakini vyuo kama vile wanaweza kupanua wakaongeza Clinical Officers wakachanganya pale Maafisa Afya, wanasoma na tunaongeza idadi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zahanati nyingi sana Wahudumu wa Afya ndio wanaofanya kazi (Medical Auxiliaries) ndio wanaofanya kazi nzuri sana, lakini bahati mbaya sana unakuta zahanati moja ina mtumishi mmoja tu, Medical Auxiliary; hakuna Clinical Officer wala Clinical Assistant. Huyo ndio achome sindano, a-prescribe dawa na agawe dawa.

Naomba sana Wizara ya Afya itengewe fedha za kutosha ili waweze kuajiri watumishi wengi, kila zahanati iwe na Clinical Officer na Clinical Assistant. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nizungumzie Idara ya Afya Kinga na nizungumzie Maafisa wa Afya kuhamishiwa Ofisi ya Makamu wa Rais. Afisa wa Afya is a professional na wamesomea. Mimi mwenyewe ni Retired Health Officer. Wamesomea miaka mitatu mambo ya afya. Sasa tatizo linakuja wanahamishiwa Ofisi ya Makamu wa Rais, kwa sababu ya lile neno tu la environmental basi; lakini hawa wamesoma mambo ya Public Health and Preventive Medicine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa nashauri, ukitembelea nchi nyingine kwa mfano Kenya, Uganda, Malawi na Namibia, Idara ya Afya Kinga ni idara kamili na ina vote yake kabisa, yaani Maafisa Afya wana idara yao kamili na Wakurugenzi wao, lakini hapa sasa tunaanza kuwagawa Maafisa Afya, wengine waende Ofisi ya Makamu wa Rais. Kwa hiyo, nakushauri Mheshimiwa Waziri, Maafisa Afya wote warudi Wizara ya Afya ili waweze kuimarisha kitengo hiki cha Idara ya Afya Kinga. Hawa ndio wanaoshughulika na usafi, kukagua mambo ya nyama, mahoteli na hizi food premises, lakini sasa ukiwapeleka kule, anaitwa Afisa Mazingira, haitwi tena Afisa Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi vyuo nadhani mngevibadilisha majina. Sisi wakati tunasoma kilikuwa kinaitwa Chuo cha Maafisa wa Afya, lakini sasa mkishasema Chuo cha Afya ya Mazingira, Afisa Afya amesoma mambo mengi sana. Syllabus ya sasa wanasoma kama madaktari. Wanasoma mambo ya minyoo na mambo mengi sana; mambo ya preventing. Ukimuuliza Afisa Afya, kwanza ndio wanaokagua nyama (meat inspectors) wanajua ante- mortem inspection wanajua post-mortem. Unaweza ukachinja hapa ukatundika carcass ukimwambia Bwana Afya akague anakagua na anakwambia kabisa hawa ni taenia solium, hawa ni taenia saginata, wanakwambia. Ni wataalam wa haya magonjwa. Sasa kuwahamishia Ofisi ya Makamu wa Rais, it is wrong. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa namwomba sana Mheshimiwa Waziri wa Afya, Maafisa Afya wote warudi na muanzishe kada ya Health Assistant au Assistant Health Officer kama zamani, kwa sababu hawa Maafisa Afya, wale wenye Diploma wengi wapo katika Wilaya lakini Health Assistant wanatakiwa wakae kwenye Zahanati. Kila Zahanati iwe na Health Assistant. Kazi yao kubwa ni elimu ya afya (Health Education), kuelimisha wananchi kuzungukia vijiji kuhusu usafi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Muhimbili zamani tulikuwa na kituo chetu cha Health Education Unit, wapo Maafisa Afya kwa ajili ya elimu ya afya. Hata hospitali zetu zote hizi tulikuwa tunatoa elimu ya afya kwa wagonjwa (out- patient na in-patient) lakini siku hizi sijui kama linafanyika hili. Kwa sababu kinga ni bora kuliko tiba. Kinga is less expensive lakini tiba ni very expensive. Mtu akiugua kipindupindu, gharama ya kumtibu ni ngumu, lakini ukimwambia mtu achimbe choo, achemshe maji ya kunywa na atunze usafi, umezuia ule ugonjwa. Kwa hiyo, kidogo inakuwa ni gharama nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa na hayo machache. Nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, ninaunga mkono hoja hii ya Mheshimiwa Waziri wa Afya, lakini waongeze bidii ya kutenga fedha kwa ajili ya kununua madawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile Hospitali yangu ya Mpwapwa iongezewe madawa na watumishi wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.