Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mungu na ninakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kwanza kuchangia katika hoja hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijatoa mchango wangu, niseme tu kwamba Mheshimiwa Rais alipochagua vijana kuongoza katika sehemu mbalimbali, nadhani kusudio lake lilikuwa vijana waoneshe uwezo kwa sababu ya ujana wao, uwezo wa kufikiri, kukimbia na kutenda kwa haraka. Ni kwa sababu hiyo nataka niwapongeze Mawaziri hawa watatu; Mheshimiwa Jafo pamoja na wenzake Mheshimiwa Kandege na Mheshimiwa Kakunda kwa kazi wanayofanya. Wizara hii ni kubwa sana, lakini kwa muda mfupi wameweza kukimbia nchi nzima na kufanya hayo mengi waliyoyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niseme tu kwamba kwa mara ya pili leo hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani imekosekana. Sasa jambo hili siyo afya kwa Bunge na wala siyo rekodi nzuri ambayo inaandikwa katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kushauri Uongozi wa Bunge uchukue hatua dhidi ya jambo hili, kwa sababu jambo hili likiendelea linafedhehesha demokrasia ndani ya Bunge na vizazi vijavyo vitatuona kwamba tumeweka precedent mbaya sana katika nchi yetu na Bunge letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sasa napenda sana nizungumze suala la elimu. Suala la elimu sasa ni jambo ambalo linazungumzwa na wengi katika nchi yetu na miezi michache iliyopita, Mheshimiwa Rais Mstaafu Benjamin Mkapa alitoa rai lifanyike kongamano kwa ajili ya kujadili elimu ya nchi hii ambayo inaporomoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami leo ningependa kusema kwamba ni lazima elimu yetu tuibadilishe tujikite kwenye elimu yenye ujuzi kwa watoto wetu; elimu yenye malengo ambayo itawezesha watoto wetu wakimaliza hata primary school wajue kwamba ni nini ambacho wameandaliwa kwenda kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale wahenga wenzangu ndani ya Bunge, wanakumbuka kwamba baadhi yetu tulimaliza darasa la saba tukiwa tuna ufundi wa namna fulani. Tulikuwa tunajua kutengeneza meza, bustani mbalimbali, masweta, mashuka na kadhalika, lakini leo hii mtoto anamaliza darasa la saba hajui chochote. Hata kilimo ambacho anaambiwa akafanye hajui, mtoto anamaliza form four hajui chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana turejee kwenye elimu ya zamani ya kujitegemea. Nasema tuache kuendesha elimu kwa matamko. Siku chache zilizopita, tumesikia habari ya kuondolewa michango mbalimbali kwenye mashule; ni sawa kuna michango ambayo ilikuwa inakera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nazungumza sana kuhusu mchango wa chakula mashuleni. Upo utafiti unaosema kwamba akili za watoto wetu zimedumaa kwa asilimia 42 kwa sababu ya lishe duni. Hii vile vile inatokana na elimu tunayowapa. Zamani tulikuwa tunalima bustani tunakula mboga mashuleni; tulikuwa tunafuga sungura, tunakula sungura mashuleni; tulikuwa tunafuga kuku, tunakula mayai shuleni; na tulikuwa tunafuga ng’ombe tunakunywa maziwa shuleni. Sasa ni mdudu gani aliyeingia katika nchi yetu akaondoa mambo haya katika Shule za Msingi matokeo yake watoto wetu sasa tunawadundulizia? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali iangalie uwezekano wa kuwapa watoto wetu wote chakula. Wale ambao mmesoma zamani mtakumbuka jinsi Mwalimu Nyerere alivyoenda kwa Rais J. F. Kennedy wakati ule tukapata shayiri na maziwa watoto wakasoma, kiwango cha elimu kilipanda namna gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ni huduma. Pamoja na kwamba tunajenga standard gauge, reli; tunanunua ndege na kadhalika, kama hatutaangalia tukahudumia elimu yetu sawasawa, Taifa hili litakwenda kuangamia. Mifano tunayo, sasa hivi bajeti inajadiliwa katika nchi zote za Afrika Mashariki. Ukienda Kenya wanajadili kuhusu ajira kwa vijana na akinamama, wanajadili habari ya uwekezaji katika assembling ya viwanda vya magari. Ukienda Uganda wanajadili habari ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tupo katika Bunge, Watanzania wanajadili habari ya watoto waliotelekezwa. Ni kwa sababu akili zetu tumezi-corner kwenye kujadili vitu vidogo vidogo badala ya kujadili issues kubwa za kuisaidia nchi yetu. Kwa hiyo, naomba kabisa Wizara iangalie namna ya kututoa hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, nizungumze habari ya asilimia kumi ya wanawake na watoto. Naunga mkono yale yaliyosemwa na Kamati yangu, lakini tumekuwa tukiwalaumu Wakurugenzi hapa. Hawa Wakurugenzi, leo nataka niseme kwamba Wakurugenzi katika nchi yetu wanafanya kazi katika mazingira magumu sana na sababu ni kwamba fedha za kuendesha Halmashauri hawapati. Matokeo yake wanaangalia ile asilimia kumi ndiyo inayowasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kuna Halmashauri ambazo hazilipi posho kwa Madiwani; na sababu ni kwamba fedha ambazo walikuwa wanategemea kwenye vyanzo mbalimbali, Serikali Kuu imechukua, yaani ni kana kwamba hawa Wakurugenzi wamefungwa mikono na miguu halafu wanaambiwa wakimbie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, pamoja na utekelezaji wa hayo Kamati iliyosema, lakini ni lazima Serikali iangalie uamuzi wake wa kuzinyang’anya hizi Halmashauri vyanzo vyake vya mapato. Ni kweli asilimia kumi inasaidia, katika Jimbo langu najua. Jimboni kwangu Warombo ni watu wanaohangaika dunia nzima wamo, Halmashauri zote Tanzania Warombo wapo kwa sababu wamezoea hivyo. Wangepata hizi pesa, zingewasaidia zaidi. Kwa hiyo, naunga mkono itungwe sheria, lakini pia iwepo akaunti maalum ambapo hizi pesa zitaingia ziweze kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze kuhusu TARURA. Naunga mkono TARURA kwa sababu hapo nyuma fedha za barabara zilikuwa zinagawiwa kisiasa. Diwani anataka barabara yake anakwenda ana-influence kule, inajengwa. Diwani ambaye hawezi kufanya hivyo, anashindwa. Sasa nasema tu kwamba ili kuondoa malalamiko TARURA ishirikishe Halmashauri kwa kutoa taarifa mbalimbali ya kazi wanazofanya ndani ya Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuwe na Bodi ya TARURA ngazi ya Wilaya na bajeti ya TARURA iongezwe kutoka asilimia 30 ya Mfuko wa Barabara sasa, angalau ifike asilimia 50 na uanzishwe mfuko wa matengenezo ya barabara ya dharura kwa sababu barabara hizi za za vijijini ni tofauti na zile barabara kuu. Hizi za vijijini zinaharibika mara kwa mara mvua inaponyesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumze kuhusu utawala bora. Tumeshuhudia ugomvi na kutoelewana katika Halmashauri mbalimbali kati ya Wakurugenzi, Madiwani pamoja na Watendaji wengine. Tunaiomba Serikali kwa mara nyingine itafute namna ya kuondoa hii migogoro, kwa sababu kwenye migogoro kazi haiwezi kufanyika. Wakurugenzi ambao wanafikiri wanataka kufanya siasa, wanafikiri wanataka kuua Wabunge, ni vizuri Serikali iwa- identify wakae pembeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ni kwa Halmashauri zote, unakuta Wakurugenzi wamekaa pale, Mkurugenzi wa Halmashauri X ana uhusiano na Mkurugenzi wa Halmashauri Y huko, wanachoreana namna ya kupata Ubunge, matokeo yake wanaingiza migogoro katika Halmashauri, Halmashauri haziendi kwa sababu huyu ana tamaa. Wachunguzeni ili iamuliwe, kama wanataka kufanya siasa, wafanye siasa. Vinginevyo tunao wajibu kabisa wa Kimungu wa kuhudumia watu wetu na siyo kuvutana kwa ajili ya nani awe nani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, yapo maagizo yanayotolewa na viongozi wetu. Kwa mfano, Mawaziri wetu wametoa maagizo kuhusu Halmashauri ya Tunduma kwa barua mara mbili, Mkuu wa Wilaya hatekelezi, Mkurugenzi hatekelezi, Madiwani na Halmashauri iliyochaguliwa na wananchi haifanyi kazi na haikai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unashindwa kuelewa, hii dharau ya Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa kwa Mawaziri wetu inatoka wapi? Kwa sababu Waziri anamwakilisha Rais na Waziri anapotamka maana yake anaangalia sera, sheria na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie viburi vya baadhi ya Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya na Watendaji ili Halmashauri zetu ziweze kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna kamata kamata ya...


TAARIFA . . .

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, bila shaka umenilindia muda wangu, sasa hii siyo nafasi yako ya kujitetea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, sasa hivi kumekuwa na matamko mbalimbali na ya ajabu ya kuhatarisha usalama wa nchi. Yupo mtu mmoja anaitwa Cyprian Musiba, anaita mkutano na Vyombo vya Habari anaanza kushukutumu baadhi ya Viongozi na kutoa maagizo, kwamba ningekuwa mimi ningeua hata 200. Juzi Maaskofu wamezungumza, anaitisha Vyomb vya Habari, anasema ningeua hata 200. Hivi nchi hii si Usalama wa Taifa wapo, nchi hii si ina dola? Hivi huyu mtu mnamkalia kimya ina maana mnamtuma? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi watu wanapotea, sasa hivi watu wanauawa, mtu anasimama hadharani anasema ningekuwa ningeua 200, ningekuwa ningeua 300, halafu anaangaliwa tu hivi na anaandika kwenye gazeti lake. Wakati Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe, shemeji yangu, unafungia magazeti kwa sababu mbalimbali, huyu anatoa matamko kwenye hilo gazeti lake kwamba ataua, atakamata, atafanya nini! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara ya mwisho amenitaja mimi kwamba ni mmoja kati ya majasusi wa CHADEMA. Nataka niwaambie, kwa sababu watu wamepotea hapa watu wameuawa hapa, Serikali mnamsikia Ndugu Musiba mnakaa kimya, hamumchukulii hatua, mimi nataka nijenge hoja kwamba Serikali mnawajua wauaji, kwa sababu Musiba anawatamka hamchukui hatua, ni mtu wenu. Vinginevyo, njooni hapa mtuambie huyu Musiba ni nani na mchukue hatua dhidi yake. Vinginevyo, kujenga nyumba ni jambo gumu lakini kuibomoa ni kwa siku moja; (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taifa hili waasisi walilijenga kwa nguvu, kwa shida kubwa, lakini watu kama akina Musiba kwa sababu ya kutafuta political mileage, wanalivunja. Kwa sababu kama ataniua mimi, mimi nina ukoo wangu, mimi nina ndugu zangu, nina rafiki zangu, hicho kisasi mtakibebea wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.