Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Juma Kombo Hamad

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Wingwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipatia dakika tano hizi na naomba niseme machache. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia kupata muda huu wa dakika chache na nianze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Katiba na Sheria kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 133 na Ibara ya 134, inazungumzia uwepo wa Tume ya Fedha ya Pamoja na Akaunti ya Pamoja ya Fedha ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tume hii ilianzishwa mwaka 1996 na ilizinduliwa rasmi mwaka 2003.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja atuambie je, Tume hii ipo na kama ipo inafanya kazi gani? Naomba hili suala liwekwe sawa, kwa sababu uwepo wa Kamati ya Pamoja ya Fedha na Tume ya Pamoja ya Fedha au Akaunti ya Pamoja ya Fedha bila shaka ingetufanya sisi Watanzania tukawa na mgawanyo sahihi wa mapato ya Muungano na Tume hii ingetusaidia sisi kuondoa na ikawa ndiyo kimbilio la kuondoa changamoto zote zinazogusa maslahi ya pande mbili za Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa sababu Tume hii haipo ingawa imezungumzwa kwenye Katiba, ni suala la Kikatiba, lakini kwa sababu haipo na haijaundwa tunaamini kwamba kero za Muungano ambazo tokea juzi zimekuwa zikitawala kwenye Wizara hizi mbili za Katiba na Sheria na Wizara inayoshughulikia mambo ya Muungano zitaendelea kuwepo na haziwezi kutatuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatujui ni sababu zipi ambazo au kuna changamoto zipi ambazo zimepelekea Tume hii ya Pamoja ya Fedha mpaka leo iwe haipo na haijaanzishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo naomba nilizungumze ni Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya nne (4) ambayo imezungumzia mamlaka mbili za Serikali ikiwemo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Katiba imezungumzia Mamlaka mbili za Mahakama; Mahakama ya Tanzania Bara au Mahakama ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lakini imezungumzia Mahakama ya Zanzibar ambazo Taasisi hizi mbili zote zina mamlaka sawa ya kiutendaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mamlaka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano inatekeleza matakwa na masuala yanayohusu Muungano na Mamlaka ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatakiwa isimamie masuala yanayohusu Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Kumekua na mwingiliano mkubwa wa utekelezaji wa majukumu haya.

Mhesimiwa Mwenyekiti, ambacho nataka kukisema hapa kwamba tumekuwa tukizungumzia malalamiko mengi na masuala mengi yanayohusu utekelezwaji wa Mamlaka hizi mbili kwamba kumekuwa na mwingiliano na kumekuwa na kutokuaminiana katika utekelezaji wa majukumu. Tunachokizungumza hapa ni kwamba, Wizara ituweke wazi na akija Mheshimiwa Waziri atuweke wazi juu ya Mamlaka hizi mbili zinatendaje majukumu yake.

Mheshimiwa Mwneyekiti, kubwa, Zanzibar imekuwa ikipigania mara nyingi kujiunga na Taasisi ambazo ingeruhusiwa kujiunga, lakini Mamlaka moja imekuwa ikichukua fursa ya kuiamuru Mamlaka nyingine kwamba hamna haki ya kujiunga na Taasisi hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukishirikiana katika masuala pengine ya Zanzibar kujiunga na FIFA, Zanzibar kujiunga na CAF, lakini tumeambiwa au tunaelezwa kwamba tunashirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili Zanzibar ijiunge na vyombo .

Mheshimiwa Mwenyekiti, masikitiko makubwa ni pale Zanzibar ilipokuja kuruhusiwa kujiunga na OIC kwa nini iliambiwa ijitoe? Halafu leo tunajikomba tunakuja kusema kwamba tunaisaidia Zanzibar ili ijiunge na FIFA, ili ijiunge na CAF huu si uongo kweli?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunapigania kujiunga na vyombo hivi kwa nini leo tusiiruhusu Zanzibar kwa sababu ina uwezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo naomba nizungumze, nalielekeza kwa Mkurugenzi wa Mashtaka. Kila siku tumekuwa tukilalamika kuna kesi zimechukua muda mwingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale Masheikh wa Uamsho na wale Masheikh waliokamatwa katika Mji wa Arusha, tunaomba kama Ofisi hii ya Mkurugenzi wa Mashtaka imeshindwa kupeleka ushahidi wale ni Watanzania, wale ni Wazanzibari tunaumia na lazima tuwasemee kwa sababu hawana mtu wa kuwasemea, lazima tutasimama Bungeni, tutaendelea kusema, tutaendelea kupiga kelele. Kama Serikali kupitia Ofisi hii imeshindwa kuthibitisha kwamba wale watu wana hatia basi waachiwe huru waende kwenye familia zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie na Tume ya Haki za Binadamu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.