Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mungano na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Juma Kombo Hamad

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Wingwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mungano na Mazingira kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipatia hizi dakika tano niseme machache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muda mrefu tulikuwa tunazungumzia juu ya suala la Muungano na hizi zinazoitwa kero za Muungano, lakini sasa ni dhahiri kwamba imenoga. Imenoga kwa sababu pande zote hususan za Wabunge kutoka Zanzibar sasa wameungana na wamekutana kwenye angle moja ya kusemea namna kero hizi za Muungano zinavyoathiri maendeleo na uchumi wa Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wa Zanzibar ni uchumi wa visiwa, uchumi wa visiwa siku zote unategemea zaidi biashara, biashara za fedha, benki na biashara nyingine. Leo biashara hizi zote kwa kutumia kivuli cha Muungano zimekufa na uchumi wa Zanzibar tayari ni kusema kwamba tayari ni sawa na kusema umekufa kwa sababu umesimama na biashara Zanzibar haziendi kwa sababu ya mfumo mbovu wa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisikitike sana, leo wafanyabiashara kutoka Tanzania Bara wameona bora kwenda kuchukua bidhaa Mombasa, Uganda na Kongo kuliko kusafiri kwenda Zanzibar kuchukua bidhaa kama ilivyokuwa zamani kwa sababu tu ya mifumo mibovu ya kodi, kuna nini hapa? Ni kutokana na ukiritimba na mfumo mbovu wa kodi na mfumo mzima wa mzunguko wa biashara hasa katika Tanzania yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze suala la pili, Zanzibar ilikuwa na system ya kusajili meli, miezi miwili mitatu nyuma mfumo huu wa usajili meli umezuiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nikwambie Zanzibar kwa mwezi ilikuwa inakusanya jumla ya dola 79, jumla ya shilingi milioni 333 kwa mwezi. Nikwambie sasa ninavyozungumza Zanzibar mpaka inazuiwa ilikuwa imesajili meli 457. Leo kwa sababu Zanzibar imezuiwa na vikwazo vile vimewekwa leo zimebakia meli 350 tu, watu mmoja mmoja waliosajili meli zao wanaondoka kwa sababu ya vikwazo ambavyo vimewekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme usajili wa meli, Zanzibar toka miaka kumi iliyopita, Zanzibar zimekamatwa meli mbili kwa hizo sababu zilizotajwa kwamba ni sababu ya unga, lakini kuna nchi mwezi mmoja zinakamatwa meli zisizopungua 27, Zanzibar miaka 10 zimekamatwa meli mbili? hivi kuna sababu ipi kwamba Zanzibar zimekamatwa meli ipi na iwekewe vikwazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa zilizopo sasa ni wazi na ni dhahiri kwamba Zanzibar inanyang’anywa usajili wa meli na usajili wa meli sasa unawekwa kwa jina la Tanzania. Huu ni uonevu na ni uonevu ambao haukubaliki, Muungano huu ambao tunauhubiri kila dakika na kila wakati kwa kweli umekuwa ni tatizo kwa uchumi wa Zanzibar na kwa kweli umekuwa ni kilio kikubwa kwa uchumi wa Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukisikitikia mifumo hii ya kodi ambayo tumekuwa tukizungumza, kila Mzanzibar anaenyanyuka analilia mfumo wa kodi. Mimi binafsi nimewahi kumfuata Waziri wa Fedha tukazungumza kirafiki kabisa, nimemfuata Naibu Waziri wa Fedha nikamfuata nikazungumza naye, lakini kwa masikitiko majibu ninayoyapata ni ya aibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unafika Waziri wa Fedha au Naibu wake anakujibu na anakwambia hasa kwamba wewe nia yako Bandari ya Tanzania Bara ife, sasa ndio maana nikamuuliza tu ina maana wewe umeridhika baada ya kuua Bandari ya Zanzibar, kwa sababu Bandari ya Zanzibar ni kama vile imekufa, biashara hakuna lakini yeye ameridhika kwamba Bandari ya Zanzibar ife, lakini amefurahi kuinyanyua Bandari ya Tanganyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali hii haikubaliki, lazima tuwe na mkakati na msimamo imara wa kuhakikisha kwamba bandari zote mbili zinatumika na tunaziimarisha kwa maslahi ya uchumi wa pande zote mbili, Tanzania Bara na Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuwa na Waziri wa Fedha au Waziri wa aina yoyote ambaye ana-favor upande mmoja na kuukandamiza upande mwingine, hii haikubaliki na haitokubalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme wazi kama kuna watu ambao watavunja Muungano ni watu wanaowadanganya wananchi kwamba tunatatua kero za Muungano, lakini tukitizama kero za Muungano kila uchwao zinazidi, uchumi wa upande mmoja kila uchwao unanyanyuka na uchumi wa upande mwingine kila uchwao unakufa. Sababu hii kizazi kinachokuja hakitokubali na nina kuhakikishia Muungano huu utaenda kuvunjika bila ridhaa na mitazamo ya watu. Ahsante sana.