Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Kassim Majaliwa Majaliwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, kwanza sina budi kuanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunijalia afya njema hadi leo ninaposimama katika kikao hiki cha sita cha Mkutano wa Kumi na Moja wa Bunge lako hili Tukufu kwa ajili ya kuhitimisha hoja ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu na mfuko wa Bunge kwa mwaka wa fedha 2018/ 2019. Naungana na wenzangu walionitangulia kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameendelea kukupa afya njema na kurudi hapa kuendelea na kazi yako ya kuongoza Bunge hili Tukufu Mungu ni mkubwa na aendelee kukupa afya njema zaidi. (Makofi)

Aidha, nikushukuru sana wewe mwenyewe Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti wote wa Bunge kuendelea kusimamia Bunge hili kwa michango iliyotolewa Waheshimiwa Wabunge, majadiliano na hasa hoja ya Waziri Mkuu na Mfuko wa Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kutumia nafasi hii pia kuwashukuru Wenyeviti na Wajumbe wote wa Kamati ya Kudumu ya Katiba na Sheria, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya masuala ya UKIMWI kwa taarifa nzuri walizoziwasilisha maoni na ushauri waliotoa kwa lengo la kuboresha utekelezaji wa majikumu ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge.

Vilevile nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa pongezi maoni, ushauri na hoja mbalimbali mlizozitoa wakati wa kuchangia hoja ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Napenda niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wenzangu kuwa Serikali hii ya Awamu ya Tano imepokea kwa mikono miwili pongezi zenu na michango yenu ambayo naamini itakuwa chachu ya kuongeza kasi ya utekelezaji wa mipango ya bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2018/2019.

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa naomba niwashukuru Waheshimiwa Mawaziri wa kisekta kwa maelezo ya ufafanuzi waliyoyatoa kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge. Aidha, namshukuru Mheshimiwa Jenista Johakimu Mhagama (Mbunge) Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Antony Peter Mavunde (Mbunge) Naibu Waziri wa Kazi Ajira na Vijana na Mheshimiwa Stella Alex Ikupa, (Mbunge) Naibu Waziri watu wenye Ulemavu kwa maelezo mazuri wakati wa kufafanua hoja mbalimbali za Waheshimiwa Wabunge zilizoelekezwa kwa Ofisi ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie pia fursa hii kuwapongeza sana Makatibu Wakuu wangu Mama Maimuna Tarishi, Profesa Kamuzora na Bwana Eric Shitindi kwa pamoja na Wenyeviti wa Tume wa Uchaguzi, Tume ya TACAIDS, Kamishina Jenerali, Madawa ya Kulevya, Msajili wa Vyama vya Siasa, Wakurugenzi wote na watendaji wote walio chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kazi nzuri ya uratibu wa hoja mbalimbali za Waheshimiwa Wabunge ambazo sasa tumeanza kuzijibu.

Mheshimiwa Spika, katika mjadala huu uliotumia siku tano Waheshimiwa Wabunge 124 walichangia kwa kuzungumza moja kwa moja hapa Bungeni na Waheshimiwa Wabunge 50 walichangia kwa njia ya maandishi.

Nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wenzangu wote mliochangia hoja yangu, hata hivyo kutokana na muda kutokuwa rafiki sana naomba nisiwataje kwa majina, lakini naomba majina yote ya Waheshimiwa Wabunge yaingizwe katika Hansard na ninayo hapa.

Mheshimiwa Spika, wakati wa kuchangia hoja Waheshimiwa Wabunge wengi wanakiri na kupongeza mafanikio yaliyopatikana kutokana nautendaji wa Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyo napenda nitumie nafasi hii ya awali kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa kuwapongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein Rais wa Serikali za Mapinduzi Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar kwa kusimamia ipasavyo utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi wa Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015.

Naendelea kutoa rai kwa viongozi na watendaji kuendelea kuifanyia kazi na kutekeleza kwa dhati falsafa ya Serikali ya Awamu ya Tano inayosema hapa kazi tu. Kwa mantiki hiyo viongozi, watendaji na wawakilishi tunaowajibu mkubwa sana wa kuwatumikia wananchi kwa kuwapokea, kuwasikiliza na kuwahudumia kama namna bora kabisa ya kutekeleza falsafa hiyo ya Mheshimwia Rais na Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pongezi mlizozitoa Waheshimiwa Wabunge kwa hakika si tu zimetutia moyo na kutupa nguvu zaidi ya kusonga mbele, bali pia zinatoa mwelekeo mzuri hususani pale zinapoainisha mafanikio muhimu ya kitaifa na kimataifa ambayo yamepatikana ndani ya kipindi cha takribani miaka miwili na nusu ya utendaji wa Serikali hii ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na michango maoni ushauri napongezi kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge naomba uridhie nitoe maelezo ya jumla kwa maeneo yafuatayo ambayo baadhi yetu walihitaji kujua faida za kwa nini tumetumia fedha kutekeleza miradi hiyo.

Mheshimiwa Spika, mradi wa kwanza ni ule mradi wa usimikaji wa mfumo wa rada. Mnamo tarehe 2 Aprili, 2018 Mheshimiwa Rais alizindua mradi wa usimikaji mfumo wa rada nne kwa ajili ya kuongoza ndege kwenye viwanja vyetu hapa nchini ambavyo ni vinne; uwanja wa Julius Kambarage Nyerere - Dar es Salaam, uwanja wa KIA kule Kilimanjaro, uwanja wa Mwanza na uwanja wa Songwe kule Mkoani Mbeya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, miradi hii yote imegharimu jumla ya shilingi bilioni 67.3. Hivi sasa nchi yetu rada moja tu ya kiraia iliyoko kwenye Uwanja wa Ndege wa Dar es Saalam ambayo uwezo wake wa kuona ndege ni asilimia 25 tu ya eneo ambalo linatakiwa kuona ndege. Aidha, uwezo wa rada hiyo ambayo ilinunuliwa mwaka 2002 ili itumike kwa miaka 12 kwa sasa imepungua uwezo wake kutokana na uchakavu ulionayo. Hali hiyo imesababisha baadhi ya mashirika ya ndege nchini kuhairisha kuja Tanzania kwa sababu hayaonwi, hakuna mawasiliano moja kwa moja na mahali petu Dar es Salaam, kwa maana Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mradi huu wa rada ni sehemu ya mipango ya Serikali ya kuimarisha usafiri wa anga nchini na ambao utakuwa na manufaa mwengi kwa Taifa letu. Miongoni mwa manufaa hayo sasa ni kuimarisha usalama wa nchi yetu kwa kuongeza uwezo wa kuhudumia anga yetu kutoka asilimia 25 ya sasa mpaka asilimia100 pindi zitakapokamilika na kuanza kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nataka tuanze kurejesha imani na mashirika ya ndege ambayo yaliahirisha kuingia nchini hiyo pia ni jambo muhimu. Lakini nataka turahisishe pia shughuli za kuongoza ndege zinazoingia hapa nchini kwa kuongeza pia mapato ya nchi yetu kutokana na tozo ambazo tutakuwa tunatoza kwa ndege zile kuingia na kuhudumiwa na rada zetu. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge hiyo ilikuwa ni faida za kwa nini mradi ule tumeutekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi wa pili ni kufufua Shirika la Ndege la Tanzania, ununuzi wa ndege hizi ni mipango ya Serikali ya kufufua shirika letu la ndege ambalo lilishakufa kabisa. Kama tulivyoshuhudia tarehe 2 Aprili, 2018 Mheshimiwa Rais akiongoza wana Dar es Salaam kwa niaba ya Watanzania kupokea ndege yetu ya tatu aina ya Bombardier Dash 8 Q400. Ni mwelekeo wa kulifufua shirika letu ambako sasa Serikali tumenunua ndege sita, ndege tatu zimeshaingia ndege tatu zingine zitaingia ambazo tunataka zitoe huduma ndani na nje ya nchi kwa lengo la kukuza na kama kichocheo cha ujenzi wa uchumi wa viwanda hususani viwanda vya usindikaji wa mazao kama vile matunda, usafirishaji wa maua, mbogamboga, samaki, na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, aidha, usafiri imara wa anga na wenye uhakikia utasaidia sana kukuza sekta ya maliasili na utalii. Kama ambavyo mnafahamu Watanzania wote kwamba watalii wengi zaidi ya asilimia 70 wanatumia usafiri wa ndege kuingia nchini na nchi yetu ni miongoni mwa nchi zinazoongoza kuwa na vivutio vingi ambavyo watalii wanavipenda sana. Kwa hiyo, tunataka moja kati ya malengo ni kuongeza idadi ya watalii nchini kutoka watalii milioni 1.3 ya sasa na ikiwezekana kuifikia milioni tano ifikapo mwaka 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nataka tuimarishe usafiri wa anga ndani ya nchi na ndiyo sababu sasa tunajenga viwanja vingi vya ndege katika kila mkoa ili kuwezesha ndege zetu kutua kila mkoa na kuweza kusafirisha vile ambao watakuwa wanaweza kusafiri. Lakini pia tunataka tufungue fursa za utalii kwenye mikoa hiyo ili watalii wetu waweze kusafiri kwa ndege wafike kwenye maeneo yetu, tuna vivutio vingi; Kigoma tuna eneo la sokwe ambako sasa wanaanza kufika kwa sababu ndege inakwenda sasa mpaka Kigoma na maeneo mengine mengi ambayo yana vivutio vya aina hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hili tunataka tukuze sekta nyingine ambazo zinahitaji usafiri wa ndege sekta ya kilimo lakini sekta ya mifugo, uvuvi. Lakini pia nataka tuongeze ajira nyingi ili wengine wafanye kazi kwenye shirika letu la ndege kwa kupitia maeneno yote ambayo tuliyonayo. Kwa hiyo, mradi wa ufufuaji wa shirika la ndege ulikuwa na malengo hayo kwa kifupi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, uko mradi mwingine wa kuanzisha uzalishaji wa umeme kwa wingi hii imetolewa maelezo mazuri sana na Waziri wa Nishati kwa nini tunaanzisha vyanzo vingi vya kuzalisha umeme na vyanzo hivi ni vingi tunataka kwenye maji, kwenye gesi asilia lakini kwenye upepo kwa kutumia hata pia takataka, uko uwekezaji unakuja muda mfupi wa kutumia takataka zetu kuzalisha umeme.

Mheshimiwa Spika, malengo yetu ni kupata umeme wa kutosha ili sasa uende sambamba na matakwa yetu ya kuboresha viwanda nchini ambavyo vitakuwa vinaendeshwa na umeme. Lakini pamoja na hiyo tunataka pia tuhakishe kwamba tunasambaza umeme tunapata umeme wa kutosha ili miradi yetu ya usambazaji wa umeme kwenda vijijini tupeleke umeme wa kutosha, umeme wa uhakika na umeme ambao tutakuwa tunajiridhisha kwamba tunao tunaweza pia kutumia umeme huo kwa wajasiliamali kutengeneza ajira nyingi hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia utatupatia mapato ya Serikali kupitia tozo hizo kidogo ambazo tutakuwa tunazipata kutokana na matumizi ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nieleze kwa kifupi sana kuhusu ujenzi wa mradi wa uzalishaji umeme ambao toka mwaka 1970 ndiyo ulikuwa umebuniwa na hakukua na mafanikio lakini azima yetu ya kuboresha eneo hili ndiyo kwa sababu tumeamua tutumie bonde lile la Mto Rufiji au maporomoko ya Mto Rufiji kuwa ndiyo maeneo ya kuzalishia umeme mwingi wa kutosha. Eneo hili tukishalianzisha kama alivyosema Mheshimiwa Waziri tutaongeza kiwango cha maji ambacho wanyama wetu kule msituni wataweza kutumia vizuri, lakini pia itasaidia kwenye umwagiliaji kwenye miji ambako watu wanaishi uko Ikwiriri na maeneo mengine ya Wilayani Rufiji na eneo lote linalopita mto huo pamoja na kuongeza mazalia ya samaki ambayo pia tunayo, na kuongeza sasa ubora wa hifadhi yetu ya Selous ambayo pia itakuwa inaembelewa na watalii wengi na maeneo haya yatakuwa ni kivutio. Kwa hiyo, miradi hii ikiwemo na huu wa maporomoko ya Mto Rufiji malengo yetu hasa ni hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna mradi mwingine ambao Waheshimiwa Wabunge walitaka kujua unafaida gani, ujenzi wa reli ya kisasa. Hatuna ubishi kwenye ujenzi wa reli ya kisasa kwamba reli hii kwa miaka mingi ilikuwa inapoteza uwezo wake lakini sasa kwa kuanzisha mradi huu wa reli ya kimataifa (standard gauge) utaweza kusafirisha mizigo na abiria kwa haraka zaidi na kwa sababu tunatumia umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kupitia mradi huu ambao tulitaka tujenge kwa kilometa 1219 utaweza kurahisisha pia kufanya biashara ya uhakika na nchi jirani kama Rwanda, Congo, Burundi na nchi yoyote ile ambayo itahitaji kutumia reli yetu kusafirisha mizigo yake. Kwa hiyo, tunauhakika kwamba kupitia reli hii tutaweza kupata fedha kupitia tozo mbalimbali za watumiaji wa reli hiyo kutoka nje ya nchi na ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia mnafahamu kwamba tunayo reli ambayo sasa inatumika tunaendelea kuiboresha ili iendelee kutoa huduma kwa sasa mpaka hapo tukapofanya mabadiliko na tunaendelea kupanua wigo kwa kuipeleka Tanga, tunaboresha kutoka Segera mpaka Arusha na kupitia Moshi na tunaendelea pia kuijenga/kuidumisha reli hiyo kutoka Tabora kuelekea Mpanda; na sasa nataka tuende mpaka Ziwa Tanganyika kule mpakani kabisa ili iendelee kutoa huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakapoanza sasa reli hii mpya itakuwa na uwezo wa kubeba mizigo zaidi ya tani 10,000 sawa na malori 250 ya tani 40/40 ambayo tutaondoa kwenye barabara. Kwa hiyo, faida nyingine kwamba tunataka tuimarishe barabara yetu iweze kutumika muda mrefu ili pia iweze kutumika na wengi. Lakini pia kupitia mradi huu sasa tunazalisha ajira za kutiosha ambazo tumeanza kuona Watanzania wengi wakienda kupata ajira na utakapokamilika tunatarajia takribani ajira 30,000 za moja kwa moja na nyingine 600 kwa ajili ya wajenzi, walinzi na sekta zote ambazo zinahitaji kuhudumia njia hiyo ya reli.

Mheshimiwa Spika, mradi mwingine ambao Waheshimiwa Wabunge walihitaji kujua kwa nini tumeutekeleza, ni ukuta kuzunguka Mradi wa Mererani.

Mheshimiwa Spika, wote mnajua kwamba Serikali ya Awamu ya Tano imeendelea kuhakikisha kuwa inalinda raslimali zetu, maliasili na madini. Ujenzi huu ambao umeshakamilika na umezinduliwa utasaidia sana kuhifadhi kulinda na maliasili ambazo ziko pale na Mheshimiwa Rais amefanya hili ilikuwa ni azma na hasa alidhamiria kufanya hivyo pale alipofanya ziara Mkoani Manyara na alikuwa anazindua barabara kutoka KIA kwenda Mererani na alipopata malamiko akaona ni muhimu sasa hayatekeleze.

Mheshimiwa Spika, nataka niwaambie ukuta huo wa kilometa 24.5 ambao umekamilika sasa utawezesha sasa mali zote kuzitambua pale ndani. Na ikumbukwe kwamba kabla ya ujenzi inakadiliwa kuwa kwa mujibu wa taarifa za Wataalam wetu inakadiliwa kuwa zaidi ya asilimia 40 ya uzalishaji ilikuwa inapotea tulikuwa hatuna manufaa nayo. Kwa hiyo, madini yetu ya Tanzanite sasa tunauhakika kwamba tunaweza kuyadhibiti na tukapata mapato yanayokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushahidi katika kipindi hiki kifupi ambacho tumeweka utaratibu wa ulinzi na huku ukuta unajengwa kuanzia Januari mpaka mwezi Machi, 2018 tumeingiza pato la milioni 714 kwa miezi mitatu tu ukilinganisha na pato ambalo tumelipata kuanzia Januari mapaka Disemba ya mwaka 2017 la milioni 147.1. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo muone namna ambavyo tulikuwa tunapoteza fedha nyingi na sasa ambavyo tunatarajia kupata pia fedha. Kwa hiyo, ukuta huu unafaida sana na tutaendelea kuimarsha na katika kuboresha tmeridhia ukuta ule na Mheshimiwa Rais ameridhia tumekaribisha Watanzania na wale wachimbaji na yoyote ambaye yuko kule jirani kuweka uwekezaji kule ndani, tutakuwa na maduka na nyumba ambazo za kupumuzika ili eneo lile kulifanya kuwa eneo la kivutio tutakuwa na nyumba za kufanyia mauzo ya hiyo Tanzanite kwenye eneo ambalo litakuwa kidogo linapandisha uchumi hata wenyeji wetu wa pale Mererani nao wataweza kunufaika na ujenzi wa ukuta huu wa pale Mererani.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na issue ya utambuzi wa mifugo, wengi walipoona kwenye risala yetu hawakuelewa tulikuwa tunalenga nini.

Waheshimiwa Wabunge, wote mnajua kwamba nchi yetu iliingia kwenye migogoro mingi sana ya wakulima na wafugaji na kukawa na ongezeko kubwa sana la mifugo nchini na mifugo mingine ilikuwa inatoka nje kuja kulisha ndani na kurudi nje ambayo sisi ilikuwa haitupi tija. Kwa hiyo, ili kudhibiti pia hata maliasili zetu zitumike na watanzania wenyewe kwanza, zoezi la kutambua mifugo maana yake linatuwezesha kutambua tuna mifugo mingapi, wapi na inamilikiwa na nani ili pia tuweze kuipangia utaratibu mzuri wa malisho wa namna nzuri ya huduma ya madawa lakini na huduma nyingine ikiwemo na jitihada tunazozifanya sasa za ujenzi wa viwanda ambavyo vitataka Watanzania wanufaike kupeleka ng’ombe, wauze, wapate fedha za kutosha ili waweze kujiendesha maisha yao. (Makofi)

Kwa hiyo, zoezi hili tumeendelea, lina faida nyingi na nawasihi tu Waheshimiwa Wabunge wenzangu tuendelee kushirikiana ili tukomeshe mauaji ya wakulima na wafugaji ambayo kwa sasa kumetulia kidogo na tungependa utulivu huu uendelee kwa kutokana na zoezi hili ambalo tunaendelea nalo.

Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge niseme tumepata faraja sana kuona utulivu huu, mauaji tena ya wakulima na wafugaji yamepungua na tutaendelea kuyadhibiti kadri ambavyo tutaweza kulisimamia zoezi hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kujibu hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge nao pia waliweza kuzieleza na sisi tulizichukua sasa ni muhimu kuzitolea majibu na baadhi ya hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge kwa Serikali zimejibiwa na Waheshimiwa Mawaziri wa kisekta, lakini Naibu Mawaziri nao wamejibu na zile hoja zilizosalia zitajibiwa kama ambavyo tumeendelea, ziko nyingine ambazo tutazijibu kwa maandishi na hoja ambazo pia zina mwelekeo wa kisekta zitatolewa ufafanuzi na baadhi ya Wizara ambazo zitakuja hapa kuja kuwasilisha bajeti zake na tayari tumewaagiza maswali yote na hoja zenu zote waziweke ili waje wazitolee majibu wakati wa hoja zao.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa mujibu wa Kanuni ya 99(13) ya Kanuni za Kudumu za Bunge Toleo la mwaka 2016 naomba sasa nitumie fursa hii ili kujibu sambamba na kutolea ufafanuzi kuhusu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge kama ambavyo zimetolewa.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria walitaka Serikali kudhibiti zabuni za ujenzi wa miradi ya maendeleo kwamba zabuni hizi za ujenzi wa miradi ya maendeleo zitolewe kwa uwazi. Lakini kipaumbele kitolewe kwa makampuni ya ndani ya nchi ya wakandarasi yanayokidhi vigezo na uwezo wa kutekeleza, kukamilisha miradi kwa wakati na kwa mujibu wa mikataba ya miradi husika.

Mhesghimiwa Spika, nataka nieleze kwa Watanzania kwamba tumeimarisha utoaji wa zabuni. Zabuni zetu zinatolewa kwa mujibu wa Sheria ya Ununuzi wa Umma Sura ya 410 ambayo wote wanapata zabuni zile ni wale wenye makampuni yaliyosajiliwa, yana sifa zote na yana uwezo wa kutekeleza miradi na zabuni hizi ni za wazi na mara nyingi tunashindanisha kwa makampuni ambayo yanahitaji kuomba nafasi hizo. Lakini pia tumeanza kutoa mwongozo wa ushirikishwaji wa Watanzania ili kupata zabuni zile (local content). Kwa hiyo, tuna uhakika sasa kwa utaratibu tuliojiwekea Watanzania wenye makampuni wataendelea kunufaika na zabuni za ndani ili pia waweze kufanya kazi za ndani tuweze kuwajengea uwezo wa kufanya kazi hizo na kuongeza kazi nyingi zaidi.

Mheshimiwa Spika, na tumeanza kushuhudia makampuni mengi ya Kitanzania yakifanya kazi hizo, lakini pia hata Serikali imetoa nafasi ya kuzungumza na private sectors (sekta binafsi) ili kusikia changamoto wanazozikabili na sisi kuwaambia yale ambayo wanatakiwa waboreshe ili tuendelee pia kuimarisha kwenye maeneo hayo. Lengo letu la kukutana nao ni kutaka tu kuhakikisha kwamba na wao wananufaika na zabuni za ndani ya nchi ili fedha ambayo inalipwa iendelee kubaki nchini na pale ambapo inabidi kupata makampuni ya nje mara chache ndiyo wanaweza kupata nafasi kwa kadri ya ushindani utakavyojitokeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ambayo Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria kwa pamoja na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI iliitoa inayotaka Serikali kuimarisha ukusanyaji wa mapato, udhibiti wa matumizi ya Serikali na ufuatiliaji wa miradi yetu ya maendeleo. Wanataka Serikali ihakikishe kuwa fedha zote za miradi ya maendeleo zinatumika kwa tija na kwa kuzingata thamani ya fedha ya miradi husika (value for money).

Mheshimiwa Spika, lakini pia wanataka Serikali iweke mpango mkakati wa kupata vyanzo zaidi vya mapato ili viweze kutekeleza miradi yote ya maendeleo. Kwenye hoja hii nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali imepokea maoni haya na kwamba tutaendelea kuyafanyia kazi kupitia mkakati ambao tumeuweka wa kwanza, kubainisha vyanzo vyote vya mapato kwa kila sekta. (Makofi)

Mbili, ukusanyaji wa mapato hayo na kwenye ukusanyaji wa mapato haya tumetaka ukusanyaji wote uwe wa kielektroniki ili kudhibiti mianya ya kupoteza fedha na tumeanza kuona tija kwa kutumia elektroniki tunapata mabadiliko makubwa sana ya fedha ambayo tunaikusanya. Lakini pia baada ya kuwa tumekusanya fedha hizi, tumeweka mfumo wa kudhibiti matumizi yake na tumesisitiza kwa watumishi wenye dhamana ya matumizi ya fedha hizi za umma ni lazima wawe waadilifu na waaminifu na tumesimamia hili pia kwa kupeleka kaguzi za mara kwa mara kuona kama fedha hizi kweli zinakusanywa, zinatumika vizuri baada ya kuwa tumeetoa maelekezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na hii pia tumeelekeza hata kwenye Halmashauri zetu. Halmashauri zote zibainishe vyanzo vya mapato, Halmashauri zijikite katika kukusanya mapato yake, lakini baada ya mipango kupitia Baraza la Madiwani lazima tusimamie matumizi na tumewaasa Baraza la Madiwani lisimamie kikamilifu matumizi ya fedha hizi badala ya kuwaachia Wakuu wa Idara pekee na pale kwenye uovu taarifa itolewe na kupitia kaguzi za ndani na wakaguzi wa nje nao watabaini na pale ambako kuna tatizo tunachukua hatua mara moja kwa wale wote ambao siyo waaminifu katika kuhifadhi fedha hizi na kuzitumia.

Mheshimiwa Spika, na Halmashauri tumezipa malengo. Tunataka kila Halmashauri mwishoni mwa mwaka wawe wamekusanya kwa asilimia 80. Mkakati huu bado unaendelea na kwenye Halmashauri zetu mtakapoingia kwenye Mabaraza ya Madiwani endeleeni kusisitiza na kwa kufanya hilo inawapa fursa Waheshimiwa Wabunge kupanga mipango ya maendeleo kwenye Halmashauri zenu vilevile na Waheshimiwa Madiwani.

Kwa hiyo, tuungane pamoja katika kudhibiti jambo hili la ukusanyaji wa mapato lakini pia namna ya kutumia fedha zile na zote tuhakikishe zinakwenda kweye miradi ya maendeleo ya wananchi ambayo italeta tija kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja inayohusu usimamizi na matumizi ya fedha za umma ambayo nimeieleza vizuri na mimi nasema kwenye eneo hili tumeanza kupata report ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Fedha za Ndani za Serikali ambayo ilikabidhiwa kwa Mheshimiwa Rais hivi karibuni na tutakuja kuileta Bungeni ili pia tuweze kufanya mapitia kwa pamoja. Nataka niwahakikishie hiyo ni njia mojawapo ya kudhibiti matumizi haya ya fedha za umma na tutaendelea kudhibiti matumizi ya umma na tumeendelea kuchukua hatua kwenye maeneo ambayo udhibiti wake una udhaifu.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo tumepata taarifa na wote mnajua kwenye ukaguzi wa mwaka wa fedha 2016/2017 Kurugenzi tatu tu ndiyo zimepata hati chafu nchini kati ya Halmashauri zote 180 na ngapi na hatua kali zimechukuliwa dhidi yao na hilo ni fundisho kwa Wakurugenzi wengine kwamba lazima wasimamie matumizi sahihi ya fedha za Serikali na Waheshimiwa Madiwani waendelee kutusaidia kubainisha matatizo ya matumizi ya fedha kwenye Halmashauri hizo na Waheshimiwa Wabunge wenzangu na ninyi ni sehemu ya wategemewa wetu kwamba mtatuambia wapi kuna tatizo na ili tuweze kuchukua hatua kwa lengo la kunusuru fedha hizi za umma ziende kwa wananchi kutekeleza miradi wanayoitaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja nyingine ya miradi ya maji vijijini, hoja imeitaka Serikali ikubali kuanzisha Wakala wa Maji Vijijini pamoja na kuongeza tozo za shilingi 50 kwenye mafuta ya petroli na dizeli ili kutunisha Mfuko wa Maji kwa lengo la kutatua tatizo la maji ambalo linagusa maneo mengi hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nieleze kwamba Serikali yetu ya Awamu ya Tano imedhamiria kwa dhati kuhakikisha kwamba tunatoa huduma za maji kwenye miji yetu na vijijini na Mheshimiwa Rais katika hili amewekea msisitizo na amehakikisha kwamba maeneo yote ya miji na vijijini kunakuwa na miradi ya maji na ameanzisha kampeni ya kumtua ndoo mama kichwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kampeni hii maana yake ni kuhakikisha kila kijiji wanakuwa na eneo la kuchota maji ili kumwezesha mwanakijiji asizagae hovyo bila kujua wapi mahali pa kupata maji. Kwa hiyo, Wizara ya Maji imeendelea kufanya vizuri sana, Waziri na Naibu Waziri wanafanya kazi yao vizuri, Katibu Mkuu na wote kwenye Ofisi ile kuhakikisha kwamba miradi yote inaratibiwa vizuri na inakwenda vijijini na kwa bahati nzuri na mimi nimefanya ziara kwenye maeneo niliyopita kila Halmashauri ya Wilaya ina miradi ya maji. Mahitaji ya maji ni makubwa, lakini nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba zoezi letu la kuhakikisha tunatoa huduma ya maji linaendelea. Malengo yetu kufikia mwaka 2020 maeneo ya miji yawe yamefikia asilimia 95 na maeneo ya vijijini angalau tuwe tumefikia asilimia 85 ya huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tutaenedelea kutafuta vyanzo zaidi vya kuhakikisha kwamba tunaanzisha miradi mingi ya maji kwa ajili ya matumizi ya vijijini. Kwa hiyo, wazo lenu la Serikali iendelee kutafakari kwa makini namna ya kupata fedha hasa kwa kuingiza tozo ya shilingi 50 kwenye mafuta ya petroli na dizeli tunaendelea kutafakari na tutawaambia hatua tuliyoifikia baada ya kuona miradi hii tuliyoiweka, miradi ambayo tumeipanga na tumeipeleka vijijini; tumeshapeleka vijiji vingapi, miji mingapi na miji mingapi na vijiji vingapi bado havijapata huduma ya maji na gharama ya miradi inayotakiwa ni ya kiasi gani.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa kila Halmashauri tumeagiza kila kijiji kifanyiwe upembuzi yakinifu kuona wapi tunaweza kupata chanzo cha maji ili tutoe huduma ya maji kwenye Hamashauri hiyo.

Mheshimiwa Spika, eneo la nne, ni elimu msingi bila malipo. Utekelezaji wa mpango huu bila malipo toka ulipoanzishwa tumeanza kuona mafanikio makubwa. Moja imeongeza idadi ya usajili, imepunguza kero za wazazi za kuchangia ile michango ile holela holela, hapa tunazungumzia ile michango holela na michango ile ingawa pamoja ilikuwa ina tija, Serikali ilichofanya ni kupeleka fedha badala ya kuwachangisha wananchi na tumeshaeleza mara kadhaa na hapa narudia tu kueleza kwamba tunaendelea kutuma fedha kwenye Halmashauri zetu na zinaenda kwenye shule za msingi na sekondari na jumla ya bilioni 18.5 zinakwenda pamoja na fedha ambazo tumezipeleka sasa fedha majukumu kwa ajili ya Maafisa Elimu, Wakuu wa Shule na Waratibu Elimu Kata nazo pia zinaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai mwaka 2017 mpaka mwezi Machi 2018, jumla ya shilingi bilioni 187 zimetumika kupeleka kwenye shule zetu ili kuendelea kuwapunguzia wazazi wa kuchangia ile michango midogo midogo. Suala la michango limeratibiwa vizuri, hatujazuia michango kwa wananchi, lakini tumeliondoa kwenye ngazi ya shule kwa sababu ya kuogopa kuwa huru wa kuchangisha michango mingi kwa kisingizio kwamba wamekaa na kamati za shule, wamekaa na bodi za shule na hatimaye kurudisha tena kero kwa wazazi badala yake michango hii sasa itaratibiwa na Mkurugenzi kwenye Halmashauri. Mkurugenzi anayo fursa au kwa kuanzisha Mfuko wa Elimu kwenye Halmashauri na kuwataka wazazi wachangie ili kupeleka huduma kwenye maneo mengine inaweza kuwa miundombinu au vinginevyo.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia sana suala la upatikanaji wa chakula kwenye shule zetu ambazo wanafunzi wetu wanahitaji kupata chakula. Jambo hili linaweza kuratibiwa vilevile lakini lazima lisimamiwe na Mkurugenzi kwa sababu tunapokuwa na shule mbili jirani kwenye kijiji, shule moja imekuwa na ubunifu wamepata chakula, shule nyingine hawana ubunifu, hawana chakula tunaleta mgongano pale kijijini na ndiyo maana tumesema Mkurugenzi aratibu vizuri michango. Suala la chakula shuleni ni muhimu kwa hiyo muhimu zaidi ni kwamba Wakurugenzi wote waendele na ubunifu, watenge fedha kwenye bajeti zao za halmashauri, wajue wana shule ngapi zinahitaji kuhudumiwa kwa chakula na hasa zile ambazo ziko pembeni sana na vijiji ambazo hazimuwezeshi mwanafunzi kurudi nyumbani. Kwa hiyo michango yote sasa itaratibiwa na Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ili ngazi ya shule waendelee na kazi yao ya utoaji wa taaluma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaendelea kuimarisha kutoa huduma kwa kupeleka fedha kadri tunavyozipata na kwa kadri ya mahitaji kule shuleni ili jambo hili tuweze kuwaondolea kero wazazi walioko kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, eneo la tano, ni uzalishaji wa mazao ya biashara ambayo tumezungumza mara kadhaa na utekelezaji wake tumeuona, manufaa kadhaa tumeyaona, lakini tulianza na mazao matano; kahawa, chai, tumbaku, korosho na pamba. Tumesimamia kutoka kilimo chake mpaka masoko yake, lakini siyo kwamba ndiyo mwisho, tunaendelea kuratibu mazo mengine. Tunatambua tuna alizeti, ufuta, mbaazi, karafuu kule Zanzibar, tuna mazao mengine kama ya jamii ya kunde, mazao haya yote yanaendelea kuratibiwa na Wizara ya Kilimo na mimi nawataka Wizara ya Kilimo sasa muharakishe uratibu wa mazao haya ili nayo pia yaingie kwenye mpango bora wa kilimo na tukashirikisha Maafisa wa Kilimo wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nini tumekifanya Serikali? Kwanza tumeimarisha ugani kwenye ngazi za vijiji na Kata na kupitia ugani pia tumeimarisha vyuo vya utafiti ili viweze kutafiti mazao haya kutoka ardhi inayofaa kupandwa kwenye maeneo haya lakini namna ya kulihudumia zao lenyewe.

Mheshimiwa Spika, lakini mwisho, tunaendelea kuimarisha ushirika kwa maana ya sekta ya masoko ili kuweza kuweka mfumo mzuri wa kumwezesha mkulima kuuza mazao yake na tuna uhakika maeneo haya tutayaimarisha. Lakini tuna zao la mkonge ambalo pia nalo sasa linaanza kutuletea tija na lina bei inapanda juu ambalo linalimwa maeneo machache hasa Mkoa wa Tanga, Kilimanjaro maeneo Same na maeneo machache sana kama mkoani Morogoro. Tumeendelea pia nalo kuratibu vizuri na tumeshaoweka Afisa Zao la Katani ndani ya Wizara ili ashirikiane na wakulima wa mzao haya ambayo kilimo chake kinahitaji zaidi ya ukubwa wa hekari tano, 10 na kuendelea. Kwa hiyo, tumeimarisha mfumo wa kilimo kwa ujumla wake na mimi nina uhakika hatua tunayoifikia sasa itatusaidia sana kuhakikisha kwamba wakulima wetu wanapata tija.

Mheshimiwa Spika, kwa wafanyabiashara kwenye eneo hili nao pia hatujawaacha nyuma, tumeendelea kukaa nao vikao mbalimbali kuwaonesha njia nzuri ya kupata uwezo wa kununua mazao yetu ili mazao haya yapate masoko mazuri. Najua saa hizi tunahangaika na soko la mbaazi ambako ni nchi pekee ambayo inatumia mbaazi kwa wingi ni nchi ya India na India kwa miaka yote hiyo walikuwa wanalima zao hilo na kwa bahati nzuri kwao na mbaya kwetu, ilipofikia mwaka 2017 walikuwa wamezalisha mbaazi zaidi ya asilimia 30 ya uwezo wa kawaida, kwa hiyo, wamezuia kuingiza mbaazi kutoka nchi nyingine kwa sababu wana mbaazi nyingi zinatosha. Hata hivyo tunaendelea kuzungumza nao na tuliwahi kusema hapa mbele yenu bado niendelee kuwahakikishia kwamba mazungumzo yanaendelea ili kuhakikisha kwamba tunapata masoko ya mazao yetu ili yaweze kupata tija. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wa sita ambao kwangu mimi nahitaji kuueleza ni hii miradi mikubwa; ni namna ambavyo Serikali inatakiwa kuimarisha ajira kwa Watanzania kupitia miradi ambayo tunaitekeleza.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kujihakikishia kwamba fursa hizi za kuanzisha miradi hii mikubwa ni fursa ambazo pia zitatoa nafasi ya ajira kwa Watanzania na tumejiwekea malengo kwenye miradi hii mikubwa, idadi ya wageni ambao wanatakiwa kufanyakazi katika maeneo yale. Tunajua tuna wataalam na tunajua pia na sisi tumekosa utalaam baadhi ya maeneo, kwa hiyo, tumetoa fursa kwa wageni lakini kwa uratibu mzuri sana kuona ni wangapi na utaalamu gani unatakiwa ambao sisi hatuna ndiyo tunawpaa fursa, vinginevyo idadi kubwa ya waajiriwa ni watanzania wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna miradi mikubwa mingi tu ila yote niliyoitaja awali; reli, viwanja vya ndege, ujenzi wa mitambo ya umeme, lakini hata bomba pia la Tanga - Hoima nayo ni sehemu ya ajira na litachukua sehemu kubwa sana, kwa hiyo, tuendelee kuwapa matumaini Watanzania kwamba tunahitaji sasa kupanua wigo wa kupata ajira. Na kwa taarifa tulizonazo sasa kwenye miradi hii zaidi ya asilimia 80 ya kila mradi uliopo ni Watanzania wenyewe kwahiyo tunaleta faraja, nataka niwahakikishie tutaendelea kuimarisha/kuongeza idadi ya miradi ili watanzania wengi wapate fursa ya kuweza kuajiriwa na kufanyakazi waweze kupata vipato vyao.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee kusisitiza tu kwamba miradi hii mikubwa, moja kati ya faida kubwa tunayoipata ni kupunguza kilio cha ajira na uzuri wa miradi hii yote inachukua ajira za watu wa ngazo zote, za elimu zote; asiyesoma kabisa, wa darasa la saba, kidato cha nne mpaka hao waliomaliza ma-degree wanapata fursa ya kufanyakazi kwenye sekta hizo. Na Serikali pia imeandaa utaratibu au programu maalum ya kitaifa ya kukuza ujuzi, kuwawezesha Watanzania kufanyakazi kwenye maeneo hayo ili wawe na sifa na programu hizi zinaendelea na Serikali imetenga fedha za kugharamia mafunzo hayo, lakini tumehamasisha wale Watanzania wanaoendesha miradi hii au wanaoendesha sekta za kibiashara kuwapokea Watanzania wetu kwenda kupata ujuzi kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, na mafunzo haya tumeyapa asilimia 60/70 wanatumia mafunzo kazini zaidi halafu asilimia 40/30 wanatumia kwa kupata maelekezo na tumeanza kushuhudia vijana wetu wakimaliza wanapata ujuzi wanapata na ajira pia. Kwa hiyo, tumetengeneza utaratibu ambao Watanzania wanaendelea kupata ajira kwenye maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja ya saba inayotaka Waziri Mkuu kufanya ziara katika maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wenzangu nitafanya ziara mikoa yote nchini na si tu kwenye mikoa, nataka nifike kwenye Wilaya na majimbo yenu nakuja kuona kazi zinazoendelea, kuja kuona changamoto zilizopo, lakini kutatua changamoto zilizopo na maeneo tuliyopita tumefanya haya.

Kwa hiyo, wale ambao mikoa yao bado sijagusa baada ya Bunge tunakuja kuona miradi yenu na hizi ziara hizi ndio zinaongeza na nani kwenu kwa hiyo tutaendelea kuja kuwatembelea ili muweze kupata fursa ya kuonyesha miradi mliyoitekeleza katika kipindi chote ambacho mpo na tutaendelea kuwaunga mkono kuhakikisha kwamba mnafanya kazi vizuri wakati wote kwenye majimbo yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ya nane Waheshimiwa Wabunge walisema Serikali iendelee kusimamia amani, umoja na mshikamano wa kitaifa. Jambo hili ni muhimu sana na ninapolizungumza niseme tu kwamba tutaendelea kusimamia kwamba nchi hii inaendelea kuwa na amani, umoja na mshikamano wa kitaifa na tunapotumia kupata nafasi hizi ni lazima tuendelee kukumbushana Watanzania wote kwamba nchi hii ili tupate maendeleo ambayo tunayalilia ambayo Waheshimiwa Wabunge wanaelezea wanaruhusu fedha zitumike kwanza lazima tuwe na amani ili pia tuweze kufanya hayo maendeleo ambayo tunayahitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapozungumzia maendeleo ya maji lazima tuwe na amani, elimu tuwe na amani, kilimo tuwe na amani nchi zote zenye vita watu hawana nafasi ya kuoga hamna mtu anafuata maji kila mmoja anakimbia huko anakojua alikotizama hajui kama huko kuna huduma au la ilimradi ameokoa maisha yake. Mmeshuhudia nchi mbalimbali tena nchi nyingi zinakimbilia Tanzania, sasa je, Watanzania tukianza kukurupushana hapa ndani tunakimbilia wapi? Kama wao wanakuja hapa sisi tunaenda wapi? Kwa hiyo, ni muhimu sana tukasimamia amani yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kutoa wito kila mmoja kwa nafasi yake aendelee kuimba amani, aendelee kuimba msisitizo na utulivu wa nchi ili tuweze kufanya maendeleo ambayo tunakusudia. Nitoe wito kwa kila mmoja kutekeleza adhima hii ili pia tuweze kusimamia amani yetu hapa nchini ni jambo muhimu sana tupambane na yale yote ambayo yanaleta uchokozi wa amani wa kuvunja amani nchini ili pia kila mmoja aweze kuwajibika namna ambavyo tunataka tuweze kuimarisha amani ambayo tunayo kila mmoja ajaribu kuepuka matatizo yanayopelekea nchi hii kuwa isitawalike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo ambalo limezungumzwa sana jana kwa masikitiko makubwa ni suala la Muungano nieleze sana masikitiko yangu juu ya mjadala ulioendelea jana sikuridhika sijaridhishwa na mjadala wa jana najua ziko hoja, lakini mjadala wa jana kwa namna nilivyojifunza ni migogoro ya mtu na mtu, kundi na kundi jambo ambalo halileti tija wala afya hapa kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, natambua kwamba Muungano wetu unaendelea vizuri, lakini natambua pia yako mapungufu na viongozi wetu wote Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais wa Serikali za Mapinduzi Zanzibar wote wameapa kusimamia Muungano huu na sisi jukumu letu pia kuhakikisha kwamba tunaunga mkono ili tuulinde Muungano wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunajua kwamba kutokana na kuingia madarakani na sasa Serikali ya Jamhuri ya Muungano ina miaka miwili, yako maboresho Serikali ya Mapinduzi Zanzibar yako maboresho. Maboresho haya yanaweza kuathiri mfumo wa kawaida ambao tulianza nao ambao tunaumaliza kupitia vikao ambavyo tulivyonavyo, inawezekana jambo hilo baada ya mabadiliko linahitaji harmonization ya kisheria. Kwa hiyo, jukumu hilo ni jukumu la Kamati ambayo inasimamiwa na Makamu wa Rais ambaye pia naye ndio anahitisha kikao cha pamoja ili tuweze kuzungumza. Lakini kwa namna ambavyo mjadala umeendelea jana na watakao na niwasihi sana Waheshimiwa Wabunge wenzangu hakuna afya kwenye mjadala kama ule wa jana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatuzuii Mbunge yeyote kuuliza swali lolote juu ya ufafanuzi juu ya mwenendo wa Muungano lakini majibishano ya mtu mmoja na mmoja hayo hayana afya. Lakini tumeanza kulifanyia kazi na hatutatoa mwanya wa Wabunge kujibishana kupeana maneno makali kwa sababu ya mwenendo wa Muungano Serikali tumejipanga vizuri tutasimamia Muungano wetu, tutatoa kero zetu ili tuende vizuri pande zote mbili tuweze kufurahia Muungano wetu ambao sasa tunao.

Mheshimiwa Spika, mimi niseme tu kwamba Muungano wetu ambao huwa tunakutana mara kadhaa katika kujadili vitu ambavyo vinahitaji kufanyiwa mabadiliko Makamu wa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan ndio Mwenyekiti wetu na sisi watendaji wa chini, mimi ni mjumbe na Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar ni mjumbe na Mawaziri walioko kwenye Wizara zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuwa tumefanya mabadiliko kadhaa ndani ya Serikali na namna ya kuendesha sekta mbalimbali ni kweli yako maeneo ambayo yanahitaji kubadilisha pia na sheria na vitu vingine, mijadala yetu inaendelea na tarehe 28 hapa tunakutana na tunafanya/ tunaendelea na mjadala huu wa maeneo yote ambayo yanaweza kuleta manung’uniko. Kwa hiyo, nawasihi Waheshimiwa Wabunge wenzangu jambo hili tuliendeshe kwa lugha nzuri za kiistarabu si vyema tukafanya tukarudia tena kama ilivyotokea jana, haifurahishi kundi moja likakasirika lakini kwa sababu mtu mmoja au wawili kuwakasirisha watu wengine jambo hili si jema sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini yote hii imetokana na issue ya sukari na mimi nataka nieleze nchi yetu inahitaji sukari kwa sababu hatuna viwanda vinavyotosha kuzalisha sukari. Zanzibar tunahitaji sukari, Bara tunahitaji sukari; na kwa kuwa Zanzibar wana kiwanda kimoja, Bara tuna viwanda vitano, viwanda hivi vitano vyote havitoshi kupeleka sukari hata kule Zanzibar kutoka huku mpaka kule Zanzibar hata kila Kiwanda cha Mahonda kiwe na uwezo wa kuzalisha sukari ikatosha Zanzibar pia na huku kwa hiyo tunachofanya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupitia Wizara ya Biashara ndio inayoratibu uletaji wa sukari Zanzibar na Serikali ile inatoa fursa wafanyabiashara kuleta sukari nchini pale Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, huku Bara tumeunda chombo kinaitwa Bodi ya Sukari ndio inaratibu kuleta sukari iwe kutoka ndani kupitia viwanda vyetu au kutoka nje ya nchi sasa sukari ya Bara kupitia viwanda vyake na huu ni mkakati wa kitaifa wa kulinda viwanda vya ndani, tunapolinda viwanda vya ndani tumebana uingizaji holela wa sukari ndani ya nchi ili tusije tukaathiri uzalishaji wa ndani. Huku tukiwa tunaendelea ku-harmonize kodi zake na nini, utakuta sukari ya nje inayoingia nchini ni ya bei rahisi kuliko sukari inayozalishwa ndani ya nchi na kwa maana hiyo kiwango cha sukari inayozalishwa ndani gharama yake inakuwa kubwa viwanda vya Bara hata kila cha Zanzibar gharama yake ni kubwa, kwa hiyo, ukileta sukari kutoka nje maana yake sukari ya ndani haiwezi kuuzika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa jambo ambalo najua Mawaziri tunahitaji pia tuwe tunawapa taarifa Watanzania na Waheshimiwa Wabunge wakiwepo ni kwamba mpango wa sukari kwa Tanzania Bara hata ile gape sugar tuwe tunapotoa matangazo kutaka watu na kuwapa vibali walete hatuchagui kama tumempa kibali ni wa Bara au wa Zanzibar wote wanapata sukari, nataka niwaambie mimi ndio natoa vibali mwaka 2016 tulipoingia madarakani tulikuwa na gape sugar ya tani 140000 kwenye tani 140000 kati ya wafanyabiashara ambao tumewapa vibali wa Zanzibar wawili na watanzania Bara watatu lakini kiwanda hicho cha Mahonda nilikipa kibali kikaingiza tani 390. Naeleza hili ili muone kwamba tunafanya kazi kwa pamoja mwaka 2017 sukari ambayo tumeingiza gape sugar ni tani 140000 walioleta sukari Tanzania ni Wazanzibar wawili na wa Bara wawili. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, muone namna ambavyo tunashirikiana na wale Wazanzibar mmoja ni agent wa hiyo Mahonda. Nataka niwaambie ukweli ili muone kwamba tunapotoa vibali hivi hatuangalii sura, hatuangalii huyu mtu anatoka wapi, ili mradi mfanyabiashara Mtanzania tunatoa vibali. Ni mwaka huu tu sasa tume-improve zaidi tumesema sukari mwaka huu ebu tuwape wazalishaji wenyewe na kibali cha gape sugar ya tani 135,000 tumewapa viwanda vyenyewe na tayari wameshaagiza na sasa sukari imeshaanza kuingia tulitaka tuwahi hata Mfungo wa Ramadhani ili nchi nzima iwe na sukari ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hasa mwaka huu peke yake ndio haijafanya Wazanzibari kuingia wala Watanzania kupata vibali wafanyabiashara wengine kwa sababu inaletwa na viwanda vyenyewe. Kwa hiyo, kama kuna malalamiko yaliyopitia hapa Bungeni yakaletwa hapa kwamba hakuna vibali ni kutokana na nature hiyo. Na mimi naamini wakati huo tunafanya majaribio, lakini mkakati wetu tunavitaka viwanda hivi vizalishe sukari ya kutosha ili nchi ijitegemee yenyewe na tukiruhusu sukari nyingi kuingia kwa uingzaji holela viwanda hivi sukari yao itabaki viwandani haitanunulika kwa sababu sukari ya ndani ina gharama kubwa kuliko sukari ya nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kauli hii Mawaziri wa biashara wote wa Bara na Visiwani kama tutaiangalia vizuri hata kule Zanzibar kiwanda cha Mahonda hicho kiwango cha uzalishaji wake ile gape sugar ndio tutoe vibali badala ya kuacha watu wanaingiza holela vitafunika soko la ndani.

Mheshimiwa Spika, mimi nilishafika Zanzibar nimeshazungumza na Waziri wa Biashara, nimeshazungumza na Waziri wa Kilimo wakati ule Mheshimiwa Hamad Rashid, yule mfanyabiashara wa Mahonda amekuwa na matatizo mengi sana, miwa yake mara nyingi imekuwa ikichomwa, haifikii uzalishaji na leo kiwanda kile kimefungwa hakizalishi.

Mheshimiwa Spika, ni jukumu letu sisi kuhakikisha tunamlinda mwekezaji yule na mtaji aliouweka pale ili aweze kupata mtaji hakuna sababu Waheshimiwa Wabunge kulumbana hapa suala la sukari, sukari imeratibiwa vizuri, lakini uratibu huo tunalinda viwanda vya ndani, tunataka viwanda hivi vizalishe, viongeze uwezo, viongeze mtaji ili viweze kutosheleza mahitaji ya ndani tunaweza kusema nchi nzima tuna viwanda sita tu Kilombero, Kagera Sugar, Mtibwa, Manyara Sugar lakini pia tuna hiyo Mahonda ni viwanda hivyo tu tunaongeza kiwanda kimoja Bagamoyo Sugar wameshaanza kujenga, tunaongeza kiwanda pale Mbigili, Mkulazi malengo yetu tuongeze sukari. Tuna shamba Kigoma kubwa sana tunataka tulime sukari, pale Manyara tunataka tupanue lile shamba nimeshakwenda pale kiwandani kuona wana eneo kubwa tu wanaweza kupanua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kazi yetu sasa ni kuwezesha viwanda hivi na wawekezaji kupata mtaji wa kupanua viwanda ili sukari iingie hapa ndani yaani tuzalishe ndani, ijitosheleze hapa ndani. Kwa hiyo, nataka niseme Waheshimiwa Wabunge msigombane bure, sukari tumetaka viwanda vya ndani viwe na uwezo wa kuzalisha vifikie malengo, hatuhitaji kuagiza mara kwa mara, kwanza sukari nyingi tukiileta watu wa TFDA wanasema rudisha kwa sababu labda inakosa ubora na vitu vya namna hiyo. Lazima tujiridhishe sukari inayoingia nchini ina ubora, kwa hiyo, naamini baada ya kauli hii mgogoro huu wa sukari sitousikia tena hapa ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nakaribisha maoni ya namna ya kuboresha sekta hii na bado Wizara ya Kilimo itakuja kwa hiyo, mnaweza mkatoa pia maoni yenu si tutakuwa hapa tunasikiliza tutapokea maoni yenu Waheshimiwa Wabunge. Kwa hiyo, jambo hili la sukari lisivuruge Muungano wetu, jambo hili la migogoro mingine, mapungufu mengine kwenye Muungano wala lisiwe jambo kubwa kwa sababu Kamati ipo na sisi tuko tayari tutasimamia mapungufu yote, tutayaondoa Bara na Zanzibar ni nchi moja ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kila mmoja, ni kila mmoja ndani ya nchi.

Mheshimiwa Spika, kwa kusema haya nadhani kwenye eneo hili ambalo nimetumia muda mrefu nitakuwa nimeeleweka na naomba niwasihi mnielewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba baada ya kusema haya sasa naomba nihitimishe na nikiri kwamba hoja zote za Waheshimiwa Wabunge zilizowasilishwa na kuzungumzwa moja kwa moja hapa Bungeni na zile za maandishi zote ni za msingi na ni muhimu na hivyo Serikali inazipokea na tutazifanyia kazi. Kama nilivyoeleza katika hotuba yangu ya bajeti Serikali imeadhimia kwa dhati kabisa kuhakikisha kwamba utekelezaji wa miradi kuimarisha utendaji, usimamizi makini wa rasilimali na nidhamu ili kukidhi dhumuni rasmi la Serikali katika kuwafikishia wananchi huduma za kuwaletea maendeleo hili tutalisimamia kikamilifu, tunataka watanzania wanufaike na huduma zote za nchi.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea pia kutenga fedha ili kukabiliana na changamoto mbalimbali zilizopo katika sekta zote na msukumo utawekwa katika kusimamia utekelezaji wa mageuzi yaliyobaki katika sekta mbalimbali ikiwemo ya kilimo, mifugo, uvuvi, maji na miradi mikubwa yote ya kielelezo ili ikikamilika na ikamilike kwa haraka na ianze kuleta mafao ambayo tunayatarajia kuyapata au manufaa tunayotarajia kuyapata ikiwemo na ajira kutoka kwa Watanzania, muhimu pia hapa ni kukumbuka kuwa bajeti ni chombo muhimu cha kutekeleza sera na malengo yaliyowekwa kupitia Serikali iliyopo madarakani na mimi naamini kama ilivyotangulia kuelezwa hapo awali muda hautoshi kujibu kila hoja ningeweza kutoa ufafanuzi yote lakini yote yameelezwa menigne yote yameelezwa na Wabunge na kwa sababu tuko hapa miezi mitatu kadri jambo linapozaliwa mko huru kuja kwa consultation halafu tuweze kutoa ufafanuzi.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa tuendelee kuunga mkono jitihada za viongozi wetu na hasa kiongozi wetu Mkuu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa juhudi zake kubwa anazozifanya katika kuimarisha ulinzi wa rasilimali za Taifa ikiwemo madini na tumeongeza ukusanyaji wa mapato ambayo yametuwezesha sasa kutekeleza mafanikio haya ambayo tumeyaeleza kwenye hotuba yetu yote na yale ambayo yatakuja kuzungumzwa na sekta husika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kusisitiza tena kwamba suala la kuwahudumia Watanzania, kuwaletea maendeleo pamoja na kuhakikisha nchi yetu inafikia uchumi wa kati unaoongozwa na viwanda mafanikio yake hayo yatatoka mikononi mwetu sisi sote. Kwa hiyo, ni muhimu sana sasa wote tuunge mkono jitihada za Serikali ili tuweze kuwafikia wananchi wetu huko waliko kwa kuwapelekea miradi ya maendeleo ni muhimu sana pia kwa wadau wote kufanya kazi zaidi kwa kuwa na nidhamu zaidi katika kila jambo umnalolifanya ili uweze kupata matokeo mazuri, na hii sasa tuendelee sasa kuunga mkono falsafa hii ya awamu ya tano ya hapa kazi tu ndio italeta majibu ya haya yote tunayosema.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.