Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, AJIRA NA VIJANA): Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kukushukuru kwa nafasi. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujalia uzima na afya Waheshimiwa Wabunge wote. Pia nichukue fursa hii kusimama mbele ya Bunge hili Tukufu ili kuchangia hoja ya Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu iliyowasilishwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiwa Naibu Waziri ninayeshughulikia masuala ya kazi, vijana na ajira, naomba nitumie fursa hii kwanza kabisa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli; Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan; Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa; Waziri wangu Mheshimiwa Jenista Mhagama kwa ushirikiano na miongozo ambayo wamekuwa wakinipa kuniwezesha kutekeleza majukumu yangu lakini pia nisimsahau Mheshimiwa Naibu Stella Ikupa kwa ushirikiano anaonipa katika utekelezaji wa majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nichukue fursa hii kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Dodoma Mjini nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa azma yake ya kutekeleza kwa vitendo Serikali kuhamia Dodoma ambako hivi sasa tumeshuhudia maendeleo mengi sana katika Jimbo la Dodoma Mjini ambayo yanatokana na uamuzi huo mkubwa wa Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kutokana na uamuzi huo wa Mheshimiwa Rais, kwa sababu asilimia kubwa hapa ya Waheshimiwa Wabunge mnaishi Dodoma na mimi ni Mbunge wenu kwa namna moja ama nyingine, nataka tu nitoe ufafanuzi katika baadhi ya mambo ambayo mmekuwa mkikutana nayo huko mtaani mojawapo ikiwa ni katika zile barabara ambazo zinawaletea tabu kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ujio huu wa makao makuu hapa Dodoma tayari hata wahisani wenyewe wameanza kuona namna ya kuboresha mji wetu. Tumepata fedha za ziada na hivi sasa kuanzia Julai barabara nyingi sana za kwetu zitakuwa na lami. Pia tuna mradi mkubwa wa Storm Water Drainage katika eneo la Ilazo ambalo limekuwa kikwazo kikubwa sana kwa watu kufika kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kutokana na azma hii ya Serikali Dodoma sasa inakwenda kujengwa soko kubwa la kisasa ambalo litakuwa ni kubwa na lenye ubora kuliko mengi sana Afrika Mashariki na Kati. Vilevile tunakwenda kujenga stendi kubwa ya kisasa ambayo itakuwa ina maegesho ya zaidi magari 600 kwa wakati mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia utakwenda kujengwa uwanja mkubwa wa kimataifa wa mpira wa miguu ambao utatoa fursa nyingi katika Jimbo letu la Dodoma Mjini. Haya yote yanatokana na kazi kubwa ambayo imefanywa na Mheshimiwa Rais ya kuhamishia Dodoma kama sehemu ya makao makuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo kama maneno ya utangulizi, kwa heshima na taadhima naomba sasa nijibu hoja ambazo zimewasilishwa na Waheshimiwa Wabunge waliokuwa wakichangia katika bajeti ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza kubwa lililojitokeza hapa ni kuhusiana na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi ambapo Waheshimiwa Wabunge wamechangia kwa kuiomba Serikali kuhakikisha kwamba elimu ya kutosha inatolewa kwa wafanyakazi na waajiri na kuhakikisha kwamba sheria hii inazingatiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi umeanzishwa kwa mujibu wa sheria ya mwaka 2008 ambayo lengo lake ni kuhakikisha kwamba wale wafanyakazi wote wanaopata matatizo yanayotokana na kazi zao waweze kufidiwa na mfuko huo. Sheria hii ilipita
hapa Bungeni na ndani ya sheria imetaka waajiri wote nchini wajisajili katika Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi ili mfanyakazi yeyote anayepata matatizo akiwa kazini, mwajiri tumuachie kazi yake ya kimsingi ya shughuli anayoifanya na kazi ya kumhudumia mfanyakazi aliyeumia ifanywe na Mfuko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hii ilitungwa hapa na kuwataka waajiri wote wajisajili na kabla ya kuanza kufuatilia waajiri wangapi wamejisajili, Mfuko ulifanya kazi ya kutoa elimu ya kutosha kwa kwenda katika kanda mbalimbali kuwaelimisha waajiri juu ya umuhimu wa huu Mfuko. Baadaye Mheshimiwa Waziri wa Nchi alitoa maelekezo kwamba sasa ufanyike utaratibu kuhakikisha kwamba waajiri wote wanasajiliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hiyo imefanyika na hata baada ya kikao cha juzi cha Baraza la Biashara la Taifa ambalo lilikuwa chini ya Uenyekiti wa Mheshimiwa Rais, maelekezo yalitoka kwamba zile kero ndogo ndogo ambazo zinawakabili waajiri Serikali tukae nao na tuweze kutafuta namna nzuri ya kufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba tayari sisi katika Ofisi ya Waziri Mkuu maelekezo hayo tumeshayafanyia kazi na elimu inaendelea katika baadhi ya kanda tunakutana na waajiri ili kuwaambia umuhimu wa Mfuko huu wa Fidia kwa Wafanyakazi ambao ni mkombozi kwa wafanyakazi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine iliyojitokeza katika michango ya Wabunge ni kwamba tuhakikishe wafanyakazi wetu wengi wanaofanya kazi katika maeneo mbalimbali ya viwanda na maeneo mengine wanapatiwa vifaa kinga kwa mujibu wa sheria. Sisi kama Wizara kupitia Wakala wa Afya na Usalama Pahala pa Kazi (OSHA), tumekuwa tukifanya kaguzi mbalimbali kuhakikisha kwamba wafanyakazi wote wanapatiwa vifaa kinga ili itusaidie pia kuwakinga na madhara mbalimbali ambayo yanatokana na kazi na mwisho wa siku kumfanya mfanyakazi wa Kitanzania afanye kazi katika mazingira ambayo ni rafiki na kulinda na afya yake pia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hii inafanyika na niwashukuru sana na kuwapongeza OSHA kwa kufanya kazi hii kwa weledi mkubwa. Naamini kabisa kwamba tutaendelea kufanya kazi hii ya ukaguzi ili kulinda nguvu kazi ya Taifa hili isipate madhara au maonjwa kutokana na kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ilizungumzwa hoja na Waheshimiwa Wabunge hapa ya kuitaka Serikali kuboresha kilimo ili kuongeza ajira kwa vijana na vilevile kuwapatia mikopo washiriki katika shughuli za kilimo. Sisi kama Wizara tuliona kwamba ni kweli, ukisoma katika tafiti ya Integrated Labour Force Survey ya mwaka 2014 inazungumza kuhusu idadi kubwa ya vijana wanaoshiriki katika shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda mrefu sana shughuli ya kilimo haikuwa inapewa kipaumbele sana kwa miaka ya nyuma. Sisi kama Serikali tukaona kwamba moja kati ya eneo ambalo linaweza likaajiri vijana wengi kwa wakati mmoja ni katika kilimo hasa kilimo biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulianza kwanza kwa kujaribu kubadilisha mitizamo (mindset) ya vijana juu ya suala zima la kilimo. Asilimia kubwa ya vijana walikuwa wanachukulia kilimo kama ni shughuli ya kufanya baada ya kukosa shughuli ya kufanya ni kama ni last resort. Kwa hiyo, sisi kama Wizara tukaitafsiri tukasema kwamba kwa mujibu wa Sera yetu ya Ajira inasema ajira ni shughuli yoyote halali inayompatia mtu kipato ikiwemo kilimo. Kwa hiyo, tukaanza kuhamasisha vijana kushiriki katika kilimo. Hii tunaifanya pamoja na Wizara ya Kilimo tukiwa tuna mpango mkakati wa kitaifa wa kuwahusisha vijana katika kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunao vijana wa kwanza wa mfano ambao tumekuwa tukiwatumia ambao ni vijana waliotoka Chuo Kikuu cha Sokoine wanaoitwa SUGECO. Vijana hawa wali-graduate Chuo Kikuu cha Sokoine wakaziweka degree zao pembeni kwa kile walichokisomea, wakakaa sawasawa katika kilimo, leo hivi navyozungumza wale vijana wanatoa mafunzo kwa vijana wenzao lakini vilevile kilimo hiki sasa kimewafanya wasifikirie ajira nyingine. Hivi ninavyozungumza wameingia kwenye mipango mikubwa ya kidunia ikiwemo mpango wa Bill and Melinda Gates ambao kwa nchi za Afrika ni Tanzania na Nigeria tu ndiyo tumepata nafasi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia sisi kama Ofisi ya Waziri Mkuu, katika mpango wa kukuza ujuzi wa miaka mitano wenye lengo la kuwafikia vijana takribani milioni 4.4, moja ya programu tuliyonayo ni Programu ya Kitalu Shamba. Katika mwaka ujao wa fedha tumeshaagiza mamlaka za mikoa waombe kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu maombi ya vitalu shamba, tutawafundisha vijana wa Kitanzania kutengeneza vitalu shamba na tutatoa vitalu shamba ili wafanye kilimo biashara cha kisasa. Lengo ni kuhakikisha kwamba vijana wengi zaidi wanafanya shughuli ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali pia kupitia Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, pale Morogoro tuna shamba la miwa la Mkulazi kwenye kiwanda cha sukari, asilimia kubwa ya tuliowachukua kushiriki katika uchumi ule ni vijana ambao ndiyo out growers na pale kuna hekari 63,000. Vijana wa Morogoro na maeneo ya karibu watapata fursa kushiriki katika uchumi huu wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ilijitokeza hoja nyingine hapa kwamba Serikali ihakikishe ajira hizi katika miradi hii mikubwa kama ya bomba la mafuta, mradi wa reli huu mkubwa inawagusa na kuwanufaisha Watanzania. Sisi kama Ofisi ya Waziri Mkuu tuliliona jambo hili, tulichokifanya awali ni kuhakikisha kwamba wataalam wetu wanakaa na kuona ni nafasi na ujuzi gani unaohitajika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshafanya coordination ndani na hivi sasa ninavyozungumza Wakala wetu wa Huduma za Ajira anafanya kazi hiyo kuhakikisha kwamba Watanzania wengi zaidi hasa vijana wanapata fursa ya kushiriki katika uchumi huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano katika hili bomba la mafuta, mpaka hivi sasa maombi ya vijana yaliyokuja ni takribani 23,650 ambapo uhakiki unaendelea ili kuwa-link na zile fursa. Lengo letu vijana wengi zaidi wapate nafasi za ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ilijitokeza hoja moja hapa ya kwamba Mfuko wa Maendeleo ya Vijana unatoa mikopo kwa ubaguzi wa itikadi ya vyama vya siasa. Naomba niliweke hili sawasawa, Mfuko wa Maendeleo wa Vijana (YDF) upo kwa mujibu wa sheria na una mwongozo wa nani anatakiwa kupewa mkopo akikidhi masharti gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, mle hakuna sharti linalosema uambatanishe na kadi yako ya chama za siasa, hakuna. Sharti ni kwamba lazima kila Halmashauri iunde SACCOS ya vijana ndiyo itakopesha vikundi katika eneo husika. Kwa hiyo, niondoe hofu Waheshimiwa Wabunge kwamba mikopo hii ni kwa ajili ya vijana wote wa Kitanzania wanaokidhi masharti ya mwongozo ambao umewekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ilijitokeza pia hoja ya Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) ambapo Wabunge wali-raise concern tu kwamba yale maeneo yao wanayotumia especially kule Dar es Salaam hawana vyumba vya kutosha na wanafanya kazi katika mazingira magumu. Nichukue fursa hii kulitangazia Bunge lako Tukufu kwamba tumefanya mawasiliano na zile Wizara ambazo zinatoka kule Dar es Salaam ambazo zimeacha Ofisi wazi, hivi sasa Tume hii ipo katika hatua za mwisho za kupata majengo mengine ambayo yatawafanya wafanye kazi kwa uhuru na ufanisi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya mwisho ni kuhusu Nembo ya Taifa na ilisemwa kwamba nembo ile jinsi ilivyo haiakisi mazingira ya Tanzania na kwamba mtu akiiona anaweza akapata picha tofauti kwa sababu kuna mwanamke anaonekana pale ana kama nywele ambazo sio za Kitanzania kwa maana ya wig. Naomba niliweke wazi tu kabisa suala hili, Nembo ya Taifa imeanzishwa kwa mujibu wa National Emblems Act, Sura ya 10 na ukiangalia siyo kweli kwamba haiakisi mazingira yetu kama inavyoonekana hapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nembo hii ni moja kati ya alama za Taifa na ukiangalia hapo, huyo anayeonekana kama kavaa wig, kile ni kilemba cha kuonesha kwamba huyu ni mwanamke wa Kitanzania na ndiyo mazingira yetu. Pia kuna Mlima Kilimanjaro ambao upo peke yake Tanzania, hakuna mlima mwingine wowote Afrika na duniani, hicho ni kielelezo kingine pekee. Pia kuna mawimbi pale kuonesha bahari, mito na maziwa yetu lakini pale chini ukiwaangalia wamekanyaga karafuu na pamba kuonyesha kwamba haya ni mazao makuu yaliyopo katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwaondolee hofu Waheshimiwa Wabunge kwamba siyo kweli nembo hii haiakisi mazingira ya Taifa letu la Tanzania. Ukiona yenyewe inasema jinsi ilivyo, wanasheria wana lugha moja wanasema res ipsa loquitur, kwamba mambo yanaongea yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema haya sasa, naomba nitamke rasmi naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Ahsante sana.