Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, (WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Awali ya yote, napenda nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipatia kibali cha kuweza tena kuzungumza ndani ya Bunge lako Tukufu na ikiwa ni mara yangu ya kwanza kuchangia hoja ya bajeti ya Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kama ambavyo imewasilishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Mheshimiwa Jenista Mhagama ambaye ndiye Waziri wangu na dada yangu mpendwa kwa miongozo ambayo wameendelea kunipatia ambayo inaniwezesha kutekeleza majukumu yangu ya kila siku nikiwa kama Naibu Waziri ninayeshughulikia masuala ya watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo naomba pia nimshukuru sana Mheshimiwa Antony Peter Mavunde, Naibu Waziri mwenzangu. Kiukweli ushirikiano anaonipatia unaniwezesha kutekeleza majukumu yangu kila iitwapo leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niende moja kwa moja kuchangia hotuba hii na sana sana nitajikita katika kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge lakini ufafanuzi mwingine utatolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri mwenzangu pamoja na Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Waziri Mkuu mwenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa kuna hoja ya uanzishwaji wa Mfuko wa Taifa wa Watu Wenye Ulemavu. Uanzishwaji wa mfuko huu ni hitaji la kisheria, Sheria Na.9 ya mwaka 2010 inaeleza wazi kwamba ni lazima kuwe na Mfuko ambao unashughulikia maendeleo ya watu wenye ulemavu. Mfuko huu una faida nyingi ikiwa ni pamoja na kusaidia kufanya tafiti za watu wenye ulemavu, lakini pia elimu ya watu wenye ulemavu pamoja na mafunzo yaani vocational training kwa watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vyanzo vya fedha vya Mfuko huu ni pamoja na fedha ambayo inatengwa na Bunge lako Tukufu, lakini pia fedha ambayo inatokana na wadau mbalimbali. Serikali yetu sikivu inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli mwaka huu wa fedha tayari imekwishatenga fedha ambazo zitasaidia sana katika uanzishwaji wa huu Mfuko.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara taratibu zitakapokamilika za kuanzishwa kwa huu Mfuko utazinduliwa rasmi. Nitoe rai kwa wadau mbalimbali wa masuala ya watu wenye ulemavu kwamba Mfuko huu utakapokamilika kuanzishwa basi wajitokeze kuuchangia kwa sababu chanzo kimojawapo cha fedha za huu Mfuko ni wadau mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ilijitokeza pia hoja kwamba tunapoelekea kwenye uchumi wa viwanda basi Serikali ihakikishe inajali kundi la watu wenye ulemavu kuona kwamba wanapatiwa ajira. Pia hili ni takwa la kisheria. Sheria Na.9 ya mwaka 2010 kifungu cha 31 kinaeleza wazi kwamba waajiri wanatakiwa kuajiri watu wenye ulemavu yaani mwajiri ambaye anakuwa na waajiriwa kuanzia 20 na kuendelea basi ahakikishe kwamba asilimia tatu inakuwa ni watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi niseme tu kama Serikali imepokea ushauri huu na itaendelea kusimamia sheria hii kuona kwamba waajiri wanaajiri watu wenye ulemavu kwenye viwanda vyao ili na wao waweze kufaidi keki yetu ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, nitoe rai sana kwa waanzishaji wa viwanda kwamba wazingatie miundombinu rafiki kwa watu wenye ulemavu. Tunaposema miundombinu rafiki kwa watu wenye ulemavu hatumaanishi tu kwamba zile ramp maana yake tukisema miundombinu watu wanafikiria kwamba inakuwa tu ni ramp. Unapokuwa umeanzisha kiwanda chako na uka-install zile mashine zako kwa jinsi ambavyo mtu mwenye ulemavu hawezi kuzitumia tayari umeshamwekea kikwazo. Kwa hiyo, niombe sana waanzishaji wa hivi viwanda wazingatie miundombinu ambayo itakuwa ni rafiki ili watu wenye ulemavu waweze kuajiriwa katika viwanda vyao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kama ambavyo tumesikia kwenye hotuba yake imeanzisha kanzidata ambayo itakuwa inajumuisha wale wahitimu wote wenye ulemavu ambao wamehitimu kutoka kwenye vyuo mbalimbali. Kanzidata hii itasaidia sana kuweka mfumo rahisi kwa watu wenye ulemavu kuweza kuajiriwa na kupata ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu inaendesha Programu ya Kukuza na Kurasimisha Ujuzi na katika programu hii na watu wenye ulemavu pia ni miongoni mwa watu ambao ni wanufaika na wataendelea kunufaika. Kupitia programu hii watu wenye ulemavu wataweza kukuziwa ujuzi wao na kurasimishiwa ujuzi ambao utawawezesha kujiajiri na kuajiriwa maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kulikuwa kuna hoja ya uboreshaji wa vyuo vya watu wenye ulemavu. Hivi vyuo ni vile vyuo ambavyo vinatoa mafunzo kwa watu wenye ulemavu, Serikali imeendelea kuviboresha vyuo hivi. Kama tunavyofahamu kwamba vyuo vilikuwa vingi na kama vinne hivi bado havifanyi kazi, lakini Serikali imejikita kuhakikisha kwamba Chuo cha Yombo na Singida kinapewa miundombinu ambayo inakuwa ni rafiki kwa kukarabatiwa kupitia Serikali yenyewe kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ukarabati unaendelea kufanyika lakini pia Serikali inahakikisha kwamba vyuo hivi vinakuwa na vifaa ambavyo vinatakiwa, vifaa saidizi, vifaa vya kujifunzia na kufundishia ili sasa iwe rahisi kwa watu wenye ulemavu kuweza kupata mafunzo stahiki sambamba na mahitaji yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba niongelee hoja ambayo imetolewa na Waheshimiwa Wabunge ya upungufu wa Walimu, walezi, wapishi pamoja na walinzi kwenye shule zetu za watoto wenye ulemavu. Nikiri wazi kama Serikali kwamba ni kweli tatizo hili lipo ama upungufu huu upo. Hata hivyo, Serikali yetu sikivu tayari Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Ofisi ya Mheshimiwa Rais – TAMISEMI ilishafanya kikao Januari, 2018 ambapo tulijadili changamoto nyingi ambazo zinawakabili watu wenye ulemavu ikiwemo changamoto hii ambayo imezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba changamoto hii imechukuliwa na inafanyiwa kazi na Serikali yetu sikivu. Kutokana na ukubwa wa tatizo si kama hili tatizo litakuwa solved kwa muda mfupi, lakini Serikali yetu tayari imeshaanza kulifanyia kazi kuona kwamba hawa walimu, wapishi pamoja na walezi na walinzi basi wanaweza kupatikana katika haya maeneo ambayo yameainishwa kwa maana ya shule za watoto wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa pia kuna hoja kwamba Serikali sasa ilete sheria kwa sababu matamko yamekuwa ni mengi kwa ile asilimia 10. Niseme kwamba ushauri huu Serikali imeupokea na itaufanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kulikuwa kuna hoja kwamba vifaa saidizi kwa watu wenye ulemavu viendelee kutolewa maeneo mbalimbali ikiwemo maeneo ya vijijini kwa sababu maeneo ya vijijini yameonesha kwamba yana uhitaji mkubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba Serikali yetu sikivu imelichukua hili na itaendelea kusambaza vifaa hivi kama ambavyo tumeona katika shule mbalimbali ikiwemo shule za vijijini vifaa hivi vimeendelea kusambazwa kwa wanafunzi. Pia nafasi inapopatikana tumeona kwamba vifaa hivi vimekuwa vikitolewa hata kwa watu wenye ulemavu ambao pia siyo wanafunzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee pia pendekezo kwamba VETA itoe kipaumbele kwa watu wenye ulemavu kwa ajili ya kupata zile stadi za mafunzo. Niseme kwamba kama Serikali tumelichukua pendekezo hili na tutalifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kulikuwa na hoja kwamba kuna idadi kubwa ya watu wenye ulemavu ambao wanakaa vijijini, hivyo Serikali iangalie jinsi gani ya kuwawezesha kwa kuwatengea fedha. Hilo kama Serikali pia tumelichukua kama ushauri na tutalifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri kwa hoja ambazo nilikuwa nazo nimeweza kuzikamilisha na niseme kwamba naunga mkono hoja iliyopo mbele yetu ya hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kama ambavyo imewasilishwa. Ahsante sana.