Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Pia namshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kutupa fursa na sisi tutoe michango yetu kwenye hoja aliyoiweka mezani. Nampongeza zaidi yeye na Mawaziri waliopo kwenye Wizara yake kwa kazi nzuri ambayo wanaendelea kufanya na kwa miongozo mbalimbali ambayo wamekuwa wakitupa katika utekelezaji wa majukumu haya mazito tuliyopewa na Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitambue michango mingi ya Waheshimiwa Wabunge iliyotolewa kwenye sekta ya maliasili na utalii. Niseme tu kwamba michango yote tumeipokea, tunaifanyia kazi na zaidi maelezo ya kina tutayatoa wakati wa hotuba yetu ya bajeti ili kuwekana vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, naomba nitoe ufafanuzi kwenye mambo machache yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo kubwa lililojitokeza katika michango mbalimbali ya Waheshimiwa Wabunge ambalo napenda kulitolea ufafanuzi ni hoja iliyotolewa na Mheshimiwa Chegeni, Mheshimiwa Njalu, Mheshimiwa Gimbi na Waheshimiwa Wabunge wengine kuhusiana na migogoro ya wafugaji na Hifadhi za Taifa. Naomba hapa nizungumzie pia jambo zima linalohusiana na zoezi la mipaka na utatuzi wa migogoro hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kufuatia maelekezo ya Serikali yaliyopitia kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu kwenye mipaka yote ya maeneo yaliyohifadhiwa tumeweka vigingi (beacons) ambazo zinayatambua maeneo ya hifadhi na kuonesha maeneo ya vijiji yanaishia wapi. Mpaka sasa tumefanikiwa kuweka takribani vigingi 27,942 sawa na asilimia 79 ya malengo tuliyojiwekea ya kuweka vigingi katika maeneo yote yaliyohifadhiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kazi hii kubwa ambayo imefanyika, bado kuna changamoto zinajitokeza. Changamoto ya kwanza kubwa ambayo tunaipata ni kwamba kuna wananchi walikuwa wakiishi katika maeneo ya hifadhi ama wakifanya shughuli mbalimbali katika maeneo ya hifadhi wakiamini ni maeneo ya vijiji. Pamoja na mwongozo aliotupa Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba beacon ziwekwe tu kwanza halafu baadaye tutazungumza na wananchi nini litakuwa suluhisho kwa yale maeneo ambayo tayari wamekuwa wakiyatumia na sisi tumekuwa tukifanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa naomba nitumie fursa hii kuwaondoa wasiwasi Waheshimiwa Wabunge wote pamoja na wananchi kwa sababu tunafanya kazi sasa baada ya zoezi la kuweka vigingi kukamilika ya kupita kwenye maeneo hayo ambayo yanaonekana aidha vigingi vimeingia kwenye maeneo ambayo wananchi wamekuwa wakiyatumia ama kwenye yale maeneo ambapo hifadhi imeingia ndani zaidi kuliko ambavyo ilikuwa kabla hatujafanya zoezi la uhakiki wa mipaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hiyo tumeanza kuifanya na tunaifanya sisi wenyewe, mimi na mwenzangu Mheshimiwa Naibu Waziri hatua kwa hatua tunakwenda kwenye eneo moja baada ya lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, migogoro mingine unakuta eneo ambalo limehifadhiwa na linatumika kwa matumizi ya shughuli mbalimbali za kibinadamu ni dogo sana. Kibinadamu tumeanza kufikiria kufanya variation ya mipaka yetu na kuyaacha nje maeneo haya ili wananchi waweze kuyatumia kama tunaona kiikolojia hakuna madhara yoyote yale yatakayojitokeza ili tupunguze migogoro ambayo tumekuwa tukiipata baina ya wahifadhi na wananchi ambao ni majirani zetu kwenye maeneo yaliyohifadhiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, kuna maeneo mengi ambayo yalitangazwa kama maeneo ya hifadhi ambayo yamekuwa yakitumika kwa muda mrefu sasa kwa shughuli mbalimbali za kibinadamu. Maeneo haya tumeshaamua kuyaachia, baadhi ya maeneo hayo yana Ranchi za Taifa, viwanja vya ndege na vijiji ambavyo vimetangazwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, katika ile ripoti tuliyopewa na wataalam wa tume iliyoundwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu, tayari kuna maeneo takribani 14 tumeyaachia lakini pia kuna maeneo mbalimbali kama alivyozungumza ndugu yangu Mheshimiwa Vuma tumepewa miongozo na viongozi wetu wakuu kwa mfano Mheshimiwa Rais alisema tuachie eneo la msitu wa kule Kagera Nkanda na tumeshaamua kuachia eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kinachofanyika sasa ni kufanya variation ya mipaka ili tuweze kutangaza rasmi lakini hatuna taarifa za wananchi kunyanyaswa katika maeneo ambayo tayari tumekwishatoa mwongozo wa kuyaachia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo hivyo kuna maeneo ya Mkungunero, kuna baadhi ya maeneo ambayo tumeona kwamba tunapaswa kufanya variation ya mipaka na kuyaachia ili wananchi ambao waliokuwa wanayatumia kwa muda mrefu waendelee kuyatumia kwa sababu hata kama kwa mujibu wa sheria siyo eneo lao, lakini wao wanaamini ni eneo lao. Kwa hivyo, mgogoro hautakwisha kwa sababu wahifadhi wataendelea kuamini kwamba wananchi wamevamia eneo lao, wakati na wananchi wanaendelea kuamini kwamba ni eneo lao hata ukiwaambia nini hawakuelewi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, katika jitihada za usuluhishi ambazo tunazifanya ni pamoja na kukubali kuachia baadhi ya maeneo au kubadilisha baadhi ya maeneo. Kwa mfano, kule Utete tumeachia eneo la Msitu wa Kale na tunafanya sasa taratibu za kurekebisha ili lirudi kwa wananchi lakini tumewaomba Halmashauri watupe eneo lingine lililopo mbali zaidi na mipaka ya mji ili tuweze kulihifadhi ku-compensate kwa eneo ambalo tumeliachia, kwa hivyo jitihada hizo zinaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuhusu migogoro baina ya wanyamapori ambao wanatoka katika maeneo ya hifadhi na kwenda kwenye maeneo ya wananchi. Kwanza hapa changamoto kubwa ambayo inajitokeza ni kwamba wananchi wengi katika miaka ya hivi karibuni wamekuwa wakifanya shughuli zao za kibinadamu aidha kwenye shoroba ambazo ni mapito ya wanyamapori ama kwenye maeneo ya karibu sana na buffer zone, eneo kinga la maeneo yaliyohifadhiwa ambazo ni mita 500 tu. Wanyama hawajui mipaka ambayo tuliojiwekea sisi binadamu wamekuwa wakitoka kwenda kwenye maeneo ya wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, tunatoa elimu ya wananchi kuzungusha mizinga ya nyuki kwenye maeneo ya mashamba yao kwa sababu wanyama kama tembo huwa wanaogopa uwepo wa mizinga ile na kurudi kwenye maeneo yaliyohifadhiwa ili wananchi waweze kuepukana na migogoro ambayo inayosababishwa na wanyama hao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunazidi kujenga madungu ama observation towers kwenye maeneo ya jirani na maeneo wanayoishi wananchi hususani maeneo korofi kwa mfano kule Itilima ambako juzi kumetokea maafa na kule Bunda kwenye Vijijji vya Kihumbu, Hunyali na Maliwanda ili askari wetu waweze kuwa-track wanyamapori aina ya tembo ambao wamekuwa wakizoea kwenda maeneo ya vijiji na kuweza kuwarudisha kwa kutumia teknolojia za kisasa kama teknolojia ya kutumia drones kwenye maeneo ya mipaka…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja.