Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kuchukua fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujalia kukutana hapa leo tukiwa na afya njema. Pili, na mimi nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii kuchangia hoja iliyoko mbele yetu, ambayo ni hoja ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuanzia ninaunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitachangia kupitia hoja mbalimbali ambazo zimewasilishwa na Waheshimiwa Wabunge kwa muda wa kipindi chote cha hoja ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu utagawanyika katika sehemu tatu muhimu; kwanza nitajikita zaidi kwenye usafiri wa anga, halafu nitakwenda kwenye usafiri wa majini, halafu nitazungumzia mwisho usafiri wa nchi kavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa usafiri wa anga kama unavyojua nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba, anga letu linakuwa salama ili Watanzania na wageni wetu mbalimbali waweze kusafiri kwa njia salama. Katika kutekeleza jambo hili kama mnavyojua, wiki moja iliyopita tulizindua mradi wa ujenzi wa rada nne za kisasa ambapo rada ya kwanza itajengwa pale Dar es Salaam, ya pili itajengwa Mwanza, ya tatu itajengwa huko Songwe na ya nne itajengwa huko KIA. Mradi ule utakuwa na gharama ya takribani dola za Kimarekani bilioni 67.3 na kazi inaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama mnavyojua mwaka jana peke yake katika viwanja vyetu vya ndege takribani wasafiri milioni 4.13 waliweza kusafiri, hiyo ikiwa ni Watanzania pia na watu wengine kutoka nje ambao wanakuja nchini kwetu kwa ajili ya utalii. Ili kuhakikisha kwamba tunajenga miundombinu ya kisasa kuvutia watu watumie kwa kiwango kikubwa usafiri wa anga pamoja na wageni wetu, tumeanzisha miradi takribani 11 sasa nchini ambayo tunafanya ukarabati wa viwanja vya ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukianzia pale Dar es Salaam tunajenga jengo la kisasa ambalo litakuwa na uwezo wa kuchukua abiria milioni 6.5 kwa mwaka na gharama yake ni shilingi bilioni 560 ukilinganisha na jengo lililoko sasa hivi ambalo lina uwezo wa kuchukua abiria milioni 2.5 kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa huko Mtwara tunakarabati uwanja wa Mtwara ambao tunaujenga sasa uwe na urefu wa kilometa 2.8 ambao ndege kubwa sasa kwa mfano Airbus A320, Airbus A330 ziweze kutua bila matatizo. Tayari mkandarasi tumeshampata ambaye ni Engineering Construction Engineering Company ambaye atafanya kazi hiyo kwa gharama ya takribani shilingi bilioni
53. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Mwanza tunaendele na ukarabati wa uwanja wa Mwanza ambao tayari sasa hivi tumeongeza eneo la kutua ndege ambalo sasa hivi limekuwa na urefu wa kilometa 3.5 na gharama ya kazi hiyo yote ni takribani bilioni 85. Kazi inayoendelea sasa hivi ni ujenzi wa jengo la control tower pamoja na maegesho ya ndege za abiria na ndege za mizigo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hivi mradi huo umefikia asilimia 68. Kazi tunayojipanga sasa ni kuhakikisha tunatafuta fedha kwa ajili ya kujenga jengo la abiria za kisasa lenye uwezo wa kuchukua takribani abiria milioni 2.5 kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mambo ya viwanja vya ndege tumeenda huko Sumbawanga ambako tayari tunataka kujenga uwanja wa ndege ambao una urefu wa kilometa 1.75 na utajengwa kwa gharama ya takribani shilingi bilioni 55.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hiyo vilevile inafanyika huko Shinyanga ambako sasa tutatanua uwanja wetu kufikia kilometa mbili ambayo itagharimu takribani bilioni 49.5 na kazi hiyo tayari mkandarasi tumeshampata. Pia huko Shinyanga tutajenga jengo la abiria.

Aidha, kazi kama hiyo itafanyika Kigoma na Tabora ambako kwa maeneo hayo mawili tutajenga mjengo ya abiria na pesa zipo. Sasa hivi tunatafuta mkandarasi kwa upande wa Kigoma, lakini kwa upande wa Tabora tayari mkandarasi wa kazi hiyo ameshapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Kiwanja cha Ndege cha Musoma tayari mkandarasi tumempata na sasa hivi tuko katika mazungumzo ya kuweza kufikia mapatano.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa kiwanja cha ndege cha huko Songwe kazi ya ujenzi wa jengo la abiria unaendelea na vilevile tunajaribu kutafuta au tayari tumeshampata mkandarasi kwa ajili ya kuweka taa sasa za kuongozea ndege ambapo ndege sasa zitaweza kutua saa 24 kwa siku, siku saba kwa wiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, gharama ya kazi hiyo ni takribani shilingi bilioni 4.8. Tayari mkandarasi yupo na tunaendelea na mazungumzo yake kuona lini tutasaini mkataba ili kazi hiyo ianze mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna kazi ambayo inaendelea vile vile huko Songea pamoja na kiwanja cha ndege cha Iringa. Tunaamini hivi karibuni na huko tutaweza kupata mkandarasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama unavyoelewa kwamba, unaweza kuwa na viwanja vya ndege vizuri, lakini kama huna ndege zako inakuwa si jambo zuri sana. Kwa kulijua hilo Serikali imenunua ndege sita kama wote mnavyojua, ndege tatu sasa hivi ziko mjini hapa Tanzania na zinafanya safari zake za kwenda Dar es Salaam, Dodoma, Tabora, Kigoma, Mwanza, Bukoba, Kilimanjaro, Zanzibar na Songea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni tutaanza safari za Mpanda pamoja na Tanga. Vilevile tutaanza safari za kwenda Entebe huko Uganda, Bujumbura, Burundi na Nairobi, Kenya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo kwa ufupi ndiyo kuhusu usafiri wa anga. Sasa naomba kwa ufupi niende kwenye usafiri wa majini...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waziri Mbarawa, muda wako umekwisha, lakini naona Wabunge wote wanataka kuendelea kukusikiliza hapa, kwa hiyo, ngoja nikuongezee dakika chache umalizie hayo maeneo mawili yaliyobaki. (Makofi)

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa muda huo na fursa hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa eneo la usafiri wa majini tuna maziwa makubwa, Ziwa Tanganyika na vilevile tuna Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Ziwa Tanganyika tayari tuna utaratibu tumeshaanzisha wa kununua meli ya abiria ambayo itachukua abiria 600 na mizigo tani 400 ambapo tunaendelea kumtafuta Mkandarasi. Vilevile tunafanya ukarabati wa MV Liemba ambapo tayari tumeshapata kampuni ya kutoka Denmark na tumetenga takribani bilioni 3.4 kwa kuanzia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Lake Vicktoria, kama mnavyojua tunataka kujenga meli ya kisasa. Bado tunaendelea na mazungumzo kutoka Korea. Meli hii itakuwa na uwezo wa kuchukua abiria 1,200 na mizigo tani 200 na magari 25 kwa vile itakuwa ni meli ya kisasa. Tunaamini hivi karibuni tutafikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikigusia kidogo kuhusu usafiri wa Kisiwa cha Mafia, najua muda mrefu wananchi kule wamelalamika. Sasa hivi tunataka kujenga land craft ambayo ni boti ya kisasa yenye uwezo wa kupeleka abiria kutoka Dar es Salaam kwenda Mafia. Bajeti inayokuja tutatenga takriban shilingi bilioni tatu kwa kuanzia tunaamini baadaye huko mbele tunaweza kumalizia ili wananchi wale sasa na wao tuweze kuendelea au kuwatatulia changamoto inayowakabili kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la mwisho kama nilivyosema ni kuhusu usafiri wa nchi kavu. Hapa kuna Wabunge wengi walitoa hoja zao, nikianzia kwa Mheshimiwa Mbunge hapa ambaye yeye alikuwa anazungumzia barabara yake kutoka Kidahwe - Kasulu yenye urefu wa kilomita 63. Kazi inaendelea na tunatafuta hela ili mkandarasi sasa asiweze kusimama kuhakikisha kazi ile inamalizika kwa muda unaostahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tuna mradi ambao unaendelea sasa hivi wa ujenzi wa barabara ya kutoka Mafinga - Igawa yenye urefu wa kilomita 137.9, kazi inaendelea vizuri. Pia huko Njombe tunaenda mpaka Makete kwa ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilomita 107.4 na kazi inaendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna miradi mingi lakini kwa vile bajeti yetu inakuja, naomba niishie hapa na wakati wa bajeti tutazungumza mengi, Mungu akitujalia. Ahsanteni sana.