Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa nafasi uliyonipa na wa kweli ni dakika saba muda mfupi. Niseme tu kwamba maelezo zaidi ya kina yatapatikana wakati wa hotuba yangu nitakayowasilisha hapa Bungeni. Sasa kwa muda huo mfupi niongelee mambo machache ambayo yanawezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lililozungumzwa kubwa hasa lilihusu migogoro ya watumiaji ardhi ikiwemo mifugo pamoja na upatikanaji wa malisho kwa ajili ya wafugaji. Ilifikia hatua Waheshimiwa Wabunge wakamshauri Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba aweze kuliingilia kati suala hili kwa sababu ni suala kubwa, wafugaji wanahangaika huku na kule kutafuta malisho, wafugaji wameingia kwenye migogoro mikubwa na watumiaji wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, narejea kusema kwamba kumekuwa na tatizo kubwa la wafugaji mahali pote ambapo wamekuwa wakilalamikiwa suala la kuingilia kwa wafugaji katika maeneo mbalimbali ya watumiaji wengine wa ardhi na kuleta adha kubwa sana kwa wafugaji katika kitendo hicho cha kukosa malisho na kutafuta maji huku na kule. Ikafika mahali Waheshimiwa Wabunge wakamuomba Mheshimiwa Waziri Mkuu aweze kuingilia kati suala hili ili kuweza kutafuta suluhisho lake.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu tayari ameshalishughulikia suala hili kwa kiwango kikubwa. Wizara tano zilipewa jukumu la kuhakikisha kwamba zinapitia maeneo mbalimbali kuona kwamba suluhisho la migogoro, kukomesha migogoro kati ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi kama kilimo, hifadhi na maeneo mengine na tayari Kamati hiyo imeshamaliza kazi yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba mambo yaliyopendekezwa kwenye hii Kamati yatakuwa ni suluhisho kubwa la migogoro kwa wafugaji wetu; litakuwa suluhisho kubwa la migogoro ya wafugaji pamoja na watumiaji wengine wa ardhi. Upande wangu mimi yale yaliyoshauriwa kwenye Wizara yangu kuyatekeleza niseme tu hapa kwamba haitafika mwezi Desemba, 2018, nitakuwa nimemaliza mapendekezo yote ya Kamati yaliyowasilishwa kwangu kuyatekeleza, ili wafugaji hawa waweze kupata ahueni katika nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala lingine ambalo linazungumzia sana suala la Ranchi zetu za Taifa ambazo zinamilikiwa na Shirika letu la NARCO. Ugawaji wake, jinsi ulivyogawiwa na wafugaji wengi kuendelea kukosa maeneo ya malisho.

Mheshimiwa Naibu Spika niombe tu kutoa taarifa kwamba nililiambia Bunge lako kwamba, tunafanya tathmini; tayari tathmini tumeshamaliza ya mashamba yote ya kwetu tuliyonayo, Ranchi za Taifa zote, holding grounds zote na hata LMUs zote. Tumemaliza kufanya tathmini na sasa tunaingia kwenye kupanga matumizi sahihi ya mashamba haya. Nikuhakikishie kwamba, baadhi ya wafugaji wetu wanaotangatanga huku na kule watapata maeneo ya kulishia mifugo yao katika maeneo haya katika mashamba haya ya taifa ambapo tutawaondoa wale wawekezaji ambao wamekuwa matapeli katika mashamba haya na kuweka wafugaji ambao wanahangaika huku na kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika tathmini hiyo bado tuna mashamba mengine ambayo yapo yanamilikiwa na Serikali ambayo nayo tunafikiria kwamba baadhi ya wafugaji wengi tutawaondoa katika maeneo mbalimbali na kuwaweka kwenye mashamba haya. Hivyo tatizo la malisho kwa kiwango kikubwa, tukitekeleza haya tuliyoshauriwa na Kamati, lakini na taasisi nyingine zinazohusika, kama mwenzangu wa maliasili na utalii akitekeleza na yeye yale aliyoshauriwa na Kamati tatizo la malisho kwa wafugaji wetu litapungua kwa kiwango kikubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na hili tatizo ambalo linani-face hapa, la muda labda nizungumzie suala lingine lilizungumzwa suala la upigaji chapa, kwamba je, katika hotuba ya Waziri Mkuu limeoekana tu suala la upigaji chapa. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge wasubiri kwa sababu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi itakuja na hotuba yake hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, na labda nimalizie hili suala lililozungumzwa, linalohusu, naona kengele ya kwanza, suala la uvuvi haramu. Suala la uvuvi haramu niombe jambo moja kwa Bunge hili, jambo hili ni kubwa, tunaendesha operation zaidi ya tatu za uvuvi haramu. Kuna Operation Sangara 2018, kuna Operation MAT na una Operation Jodari.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni mambo makubwa ambayo yamefanyika katika hatua za utekelezaji wa mambo haya. Kwa sababu Wabunge wengi wameonesha nia ya kutaka kuelewa jambo hili na kwa sababu Wabunge wengi wameuliza maswali mengi sana katika eneo hili, ilinilazimisha/ nililazimika; na Kamati yangu ya Maji, Kilimo na Mifugo iliniagiza kwamba nifanye semina kwa Wabunge wote ili tuweze kuelezana kwa kina nini kinachotokea katika suala la uvuvi hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati yangu maelekezo yao waliponipa tayari nimeshaomba kibali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu, nimeomba kibali kwa Mheshimiwa Spika, ili akubali tarehe ya 21 Aprili 2018 tuweze kutoa semina ili tuwaambie Waheshimiwa Wabunge ili tuwaambie Watanzania jinsi gani rasilimali za taifa ambavyo zimekuwa zikifujwa na watu mbalimbali wasiolitakia mema taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niseme yapo mambo ambayo yameshauriwa na Wabunge ambayo ni madogo ya uboreshaji. Mimi yale sina tatizo katika uboreshaji na ndiyo maana hata katika lile Bunge nilisema kwamba Mbunge yeyote mwenye hoja yoyote, mwenye ushahidi wowote atuletee sisi ili tuweze kuchukua hatua.

Naomba kutoa taarifa kwamba tayari tumeshasimamisha kazi watumishi tisa ambao walihusika kwa namna ile au nyingine katika kuhujumu zoezi hili, katika kujinufaisha binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile kuna mambo yalijitokeza ikafikia wananchi kwamba, hata wanapotaka kubeba samaki wao tu wa kula nyumbani, ka-box kake ka samaki 10, samaki watano wanazuiliwa kwamba hairuhusiwi kisheria, hapana. Nimekataa na nimetoa maelekezo kwa watendaji wote wa Serikali lazima wajue kwamba samaki hawa lazima watasafirishwa kwa njia ya usafiri kuwafikia walaji. Na hili haliwezi kuendelea kutokea.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kamba, tayari tumeshatoa maelekezo mambo haya yanafanyika, sasa hakuna tena kuzuiliwa wananchi kusafirisha samaki kwa ajili ya kitoweo. Hata hivyo hii isigeuzwe tena ikawa loop hole ya watu kutumia mabasi ya abiria kwa ajili ya kufanya biashara.