Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika msimu huu wa kilimo zao kuu la chakula mahindi linapata pigo kubwa kutokana na kushambuliwa na viwavi (fall army worms). Wadudu hao wavamizi wameshambulia zao hili katika maeneo mengi ya Mikoa ya Arusha, Manyara, Tanga, Kilimanjaro, Simiyu, Mara wakati mimea iko katika hali ya kuota na palizi na cha kutisha ni kuwa dawa nyingi zimeshindwa kuwatokomeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Karatu wakulima wake wengi wameathirika hadi hivi sasa wakati mahindi yako katika stage ya kutoa maua bado hao viwavi ni tishio kubwa. Hali hii isipodhibitiwa uzalishaji wa zao hilo utapungua sana na upungufu wa chakula utakuwepo. Naiomba Serikali ipeleke timu ya wataalam ili kupambana na wavamizi hao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chemchem za maji za Qangded zilizoko Mangola - Karatu ni chanzo muhimu sana cha kilimo cha umwagiliaji kwa wakulima wa bonde la Eyasi (vijiji saba). Chemchem hizo zipo katika hatua ya kutoweka kutokana na kuingiliwa na shughuli za kibinadamu. Waziri Mkuu alipofanya ziara katika Wilaya ya Karatu mwishoni mwa mwaka 2016 wananchi hao walimlilia na hatimaye aliagiza chemchem hizo zipimwe mipaka yake kwa mita 100 na zihifadhiwe. Hadi wa leo chemchem hizo hazijapimwa na ziko katika hali mbaya sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimkumbushe Mheshimiwa Waziri Mkuu kuwa agizo lake bado halijatekelezwa na chemchem za Qangded bado zinaathirika sana. Mvua za mwaka huu zimesababisha mafuriko ambayo yameziharibu sana chemchem hizo. Niombe Serikali ipeleke timu ya wataalam kushauri namna bora ya kuhifadhi vyanzo hivyo lakini fedha pia kwa ajili ya kukarabati miundombinu iliyoharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna migogoro ya ardhi inayosababishwa na mipaka tatanishi hasa kati ya wananchi na hifadhi za wanyama ambayo imeendelea kuwa kero. Kutokana na agizo la Serikali wataalam wameendelea kuweka alama za mipaka katika maeneo bila kuwashirikisha wananchi, malalamiko ni mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali kumaliza mgogoro wa mpaka kati ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (WCAA) na Wilaya ya Karatu hususani katika maeneo ya Lositete, Endamaghang, Upper Kitete, pia mgogoro kati ya TANAPA na wananchi wa Bugei katika Wilaya ya Karatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA imeanzishwa kuwa mtengenezaji wa barabara za vijiji na mjini. Katika umri wake wa karibu mwaka mmoja bado hatujaona sana matunda. Barabara nyingi katika Wilaya ya Karatu hasa katika kipindi hiki cha mvua zimeharibika na TARURA wameshindwa kurudisha mawasiliano. Naomba Serikali kutenga fedha za kutosha kuwezesha TARURA kufanya kazi yake.