Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Grace Sindato Kiwelu

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii kuchangia machache katika bajeti hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukizungumzia suala la amani kila siku, inawezekana sielewi amani inayozungumziwa ni ipi katika Taifa letu, kwani yameendelea kutokea matukio mbalimbali ya kutisha, watu wamekuwa wakiokotwa kwenye fukwe zetu za bahari wakiwa wamekufa; wengine wamepotea katika mazingira ya kutatanisha, wengine wamekuwa wakitekwa na watu wasiojulikana; pia waandishi wa habari wamekuwa wakipigwa na kutekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, habari zilizoko mitaani zinadai kuwa Waandishi hao hufanyiwa hivyo kwa sababu ya kuandika mambo yasiyofurahisha wakubwa. Naomba kujua Serikali inachukua hatua gani kwa haya mambo yanayoendelea katika nchi yetu ambayo tunadai nchi yetu ni ya amani na utulivu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza viongozi wa dini; Maskofu kwa waraka wao waliotoa kuonesha hali ya nchi ilivyo kwa sasa. Naishauri Serikali badala ya kuubeza waraka huu tukae chini kama Taifa, tujadiliane haya kwa maslahi ya Taifa letu. Viongozi hawa wa dini wamekuwa wakituombea katika shughuli zetu za kila siku. Hivyo tusiwapuuze tu kwa sababu wamesema ukweli kuhusu hali ya nchi ilivyo, kwa sababu tusiombe tu kuombewa lakini pale wanapoona nchi haiendi vizuri wakisema, mnasema wametumwa na Wapinzani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba kama Taifa, kuna kila sababu ya kuzungumza kuhusu Taifa letu linavyokwenda kwa maslahi ya nchi yetu ya Tanzania, tusitengeneze Taifa la chuki na visasi. Naomba sana Serikali itutafutie hawa watu wasiojulikana ni akina nani na wako wapi? Tusiache hali hii ya wasiojulikana kuendelea kutesa na kuwa hakuna aliye salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mipaka ya nchi yetu haiko salama sana. Naishauri Serikali kuhakikisha tunafanya mazungumzo na nchi tunazopakana nazo ili kukabiliana na uwekaji wa mipaka hiyo. Kamati yetu ilitembelea mpaka wa Uganda na Tanzania, hali siyo nzuri. Wananchi wa Uganda wameingia ndani ya nchi yetu kwa kuvuka alama za mipaka iliyoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nampongeza DC wa Wilaya ya Misenyi kwa kazi nzuri anayoifanya pamoja na Kamati yake ya Ulinzi na Usalama ya kuhakikisha wananchi na mali zao ziko salama, ingawa wako baadhi ya wananchi wetu waliokufa, waliopigwa na kunyang’anywa mali zao. Naishauri Serikali kuweka barabara katika maeneo ya mipaka yetu ili kuweza kuwarahisishia Watendaji wetu kufika kwenye maeneo hayo pale yanapotokea matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la barabara ni kubwa sana. Hivyo ni muhimu tukachukua hatua za haraka kuondoa kero hiyo. Wenzetu upande wa pili; Uganda, wana barabara inayopitika vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo ndiyo machache niliyokuwa nayo kwa leo.