Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Grace Victor Tendega

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachangia katika suala la kazi na wafanyakazi hasa Watendaji wa Vijiji ambao wameondolewa kazini kwa sababu ya kiwango chao cha elimu, yaani darasa la saba. Wafanyakazi hawa wamelitumikia Taifa letu wakati likiwa kwenye uhaba mkubwa wa watumishi na wengine walishindwa kujiendeleza kwa sababu ya mazingira halisi ya maslahi yao. Kuwaondoa bila hata kupata marupurupu siyo haki kwao. Nashauri Serikali itazame upya suala hili, kwani linaleta chuki kwa Serikali yao, kama hawatarudishwa kazini, basi wapewe stahiki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la viwanda. Viwanda 3,000 ambavyo inasemekana vipo, ni vema vikaainishwa ili Watanzania waweze kutambua vipi ni viwanda vikubwa, vya kati na viwanda vidogo. Vilevile tujulishwe viko wapi kwa ajili ya utambuzi. Nashauri pia Serikali iweke mazingira tulivu ya uwekezaji ili kupata wawekezaji wengi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niongelee kuhusu suala la walemavu. Pamoja na kwamba hatua mbalimbali zimekuwa zikifanywa kuwawekea mazingira mazuri watu wenye ulemavu, bado kuna tatizo la tengeo la fedha hasa kwa ajili ya vifaa tiba vya albino (mafuta) pamoja na huduma za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali ifanye utafiti wa kina ili kubaini watu wenye ulemavu wasio na uwezo wa kujitibu wapatiwe matibabu bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa ushauri kwa Serikali kwamba suala la kuhamisha Walimu wa Shule za Sekondari kwenda Shule za Msingi liangaliwe kwa jicho la kipekee, kwani kuna changamoto katika utekelezaji wake. Walimu hao wapewe fedha za uhamisho, wapatiwe mafunzo ya kufundisha elimu ya msingi (child psychology), saikolojia ya mtoto ili wakafundishe kwa ufanisi. Vinginevyo, badala ya kujenga, tutabomoa.