Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa mafanikio makubwa ya kiuchumi na kijamii katika kipindi kifupi cha takriban miaka miwili na nusu. Napenda pia, kumpongeza Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Mbunge, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia, napenda kumpongeza Waziri na Manaibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu na wataalam wote kwa kazi nzuri yenye mafanikio makubwa kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ni miongoni mwa nchi tatu barani Afrika ambazo uchumi wake unakua kwa kasi. Pamoja na jitihada za kukuza uchumi napendekeza kuimarisha mikakati ya kuboresha miundombinu ya bandari zetu, reli pamoja na barabara wakati tunaendelea kwa kasi na ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha SGR na kuboresha bandari ya Dar es Salaam, Serikali iweke mkakati wa kulinda biashara ya bandari zetu kwa kuboresha reli ya TAZARA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miradi mikubwa inayoendelea ya kuboresha bandari na reli za nchi jirani kama mradi wa The New Port of Nacal Development Corridor Project ya Msumbiji. Mradi huu unalenga kuifanya Msumbiji kuwa lango kuu la kibiashara za kimataifa kwa nchi za Malawi na hata Zambia, Zimbabwe na DR Congo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, reli ya TAZARA ina umuhimu wa kipekee katika kuinua uchumi, kilimo, madini, utalii, ikiwa ni pamoja na kulinda biashara ya Bandari ya Dar es Salaam, ili kuwa lango la kibiashara za kimataifa kwa nchi jirani. TAZARA ilijengwa kuwa na uwezo wa kuhimili treni ya spidi ya kilomita 110 kwa saa, ikiwa na uwezo mkubwa wa kusafirisha mizigo ya kilimo, mbolea, madini kwa nchi za Tanzania, Zambia, Malawi na hata DRC na Zimbabwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuboresha pia, ijengwe bandari kavu ya Mbeya. Aidha, imebainika kuwa, Reli ya TAZARA inaendeshwa kwa hasara na kusababisha inatumia kodi ya wananchi badala ya kujiendesha yenyewe na kwa faida. Nashauri Serikali za Tanzania na Zambia kuweka mtaji mpya, pia kuimarisha uongozi wa TAZARA, ikiwa ni pamoja na kutekeleza ushauri wa kitaalam wa mfumo bora wa kuendesha reli hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri ya utekelezaji wa miradi ikiwemo miradi ya maji. Pamoja na ujenzi wa miradi ya maji bado kuna mahitaji makubwa ya maji na huku kukiwa na tishio la tabianchi. Nashauri Serikali iweke mkakati wa kuvuna maji ya mvua kwa matumizi ya kilimo na matumizi ya kibinadamu. Uvunaji wa maji ya mvua umefanyika kwa mafanikio makubwa kwa nchi za Kusini mwa Afrika ambazo zinafanana kijiografia na Tanzania. Nchi hizi zimefanikiwa hata kuuza maji ya mabwawa hayo kwa nchi jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Serikali kwa kuboresha sekta ya afya ikiwemo ujenzi wa vituo vya afya na hospitali za wilaya. Pamoja na ujenzi wa miundombinu napendekeza Serikali iweke mkakati wa kuhamasisha Watanzania wote kuwa na bima ya afya, NHIF au CHF. Kuwepo kwa bima ya afya kwa Watanzania kwa wingi wetu kutawezesha sekta ya afya kujitegemea na kuwepo kwa huduma bora za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.