Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Ezekiel Magolyo Maige

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Msalala

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, naomba nianze kwanza kwa kupongeza sana hatua nzuri au kazi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wengi na Taifa linafahamu tuna bahati sana kipindi hiki kupata Rais mwenye maamuzi, kupata Rais ambaye analitumikia Taifa kwa dhati kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi mingi ambayo inafanyika sasa hivi ni miradi ambayo imekuwa ni ndoto ya Watanzania ya muda mrefu na ninaamini kabisa baada ya kukamilika kwa miradi hii hakika tutakuwa Tanzania ambayo itakuwa na uchumi wa kati, uchumi ambao utakuwa unaendeshwa kwa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana sasa Waheshimiwa Mawaziri ambao hasa ndio wanamsaidia Mheshimiwa Waziri Mkuu na Rais, mtusaidie pamoja na sisi wenyewe katika kuunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais, katika kuhakikisha tunafikia malengo ambayo tunajiwekea. Nitazungumzia mambo mawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni suala la upelekaji wa fedha kwenye miradi ya maendeleo. Katika ahadi tulizozitoa kwenye sekta ya afya pamoja na elimu, tulisema kwamba tutajenga vituo vya afya kila kata pamoja na zahanati kila kijiji. Baada tu ya kuwa tumewaahidi hivyo kwa mfano wananchi Jimbo langu la Msalala wameitikia vizuri sana na kama ambavyo wengi mlisikia hata hapa juzi Naibu Waziri wa TAMISEMI alitambua kazi iliyofanyika kule kwamba hivi tunavyozungumza tuna maboma zaidi ya 50 ya zahanati na vituo vya afya; mengi yana miaka miwili na zaidi, wananchi wameshafanya kazi lakini fedha za ukamilishaji haziletwi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri Mkuu Wizara zote ziko yako, wasaidie Watanzania hasa ambao ni wananchi wa kawaida waliojitikia na kuchangia nguvu zao kuinua maboma haya ili fedha za ukamilishaji ziweze kutolewa kwa wakati. Imefika wakati kwa mfano kuna sehemu ambapo wananchi tunawahimiza waanzishe miradi mingine wanasita kuchangia kwa sababu tayari kuna miradi ambayo wameshaianzisha imekamilika kwa kukamilika maboma, lakini fedha za ukamilishaji haziletwi kwa hiyo, wanaona kwamba yanaenda kubomoka au kuharibika na nguvu zao kupotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimuombe sana Serikali itoe fedha za ukamilishaji wa maboma ya zahanati na vyumba vya madarasa pale ambapo majengo hayo yameshakamilika na tayari tulishaandika andiko la kuleta taarifa rasmi Serikalini kuhusu suala hili kwa maana ya Msalala peke yake basi nilikuwa naomba Serikali itusaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nilitaka kutoa ushauri kwa Mawaziri tupunguze sana kugongana na wananchi pasipo sababu za msingi. Nitatoa mfano wa suala mifugo na uvuvi. Operation iliyofanyika juzi ya uvuvi kudhibiti makokoro ni jambo jema, lakini nilitaka kumshauri sana Mheshimiwa Waziri Mpina bahati nzuri yuko hapa kwamba sasa tujaribu kuwasaidia Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tufahamu kwamba vyazo vya asili vya samaki haviwezi vikatosheleza Watanzania milioni 50 tulionao hivi sasa. Duniani kote nchi zinazosafirisha samaki wengi au mazao ya samaki kwa wingi zimeweka nguvu kubwa kwenye fish farming. Eneo hili la uvuvi wa ufugaji wa samaki hatujaliwekea maanani sana.

Mheshimiwa Mweyekiti, Nchi kama Vietnam ambayo ni nchi ya nne kwa usafirishaji wa mazao ya samaki duniani, asilimia 70 ya samaki wanaosafirishwa nje ni wale wanaofugwa sio wale wanaovuliwa kwenye bahari kuu au kwenye maziwa na mito. Ninaamini ziwa victoria ambalo limekuwepo miaka yote limekuwa likihudumia wananchi karibia milioni nanewa miaka ya nyuma, leo hii watanzania wanaozunguka eneo hili wamefika zaidi ya milioni 20. Hauwezi ukatarajia hata ukifanya vipi mahitaji ya samaki au mahitaji ya mazao ya samaki yataendelea kuwa makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano, kwa mfano kwenye suala la kuku miaka nyuma tulipokuwa tukitegemea kuku kawaida wa kienyeji wa kutoka Singida ilikuwa ni tatizo. Lakini baada ya kuanzisha ufugaji wa kuku wa kisasa hawa broilers, leo pressure ya mahitaji ya kuku wa kienyeji si kubwa kama ambavyo ingeweza kuwa kama tusingeweka nguvu katika ufugaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwingine ni kwenye suala la maliasili, ukiangalia tungeendelea kupambana na wananchi, tungeendelea kupambana na wananchi wanaovuna kwenye misitu ya asili tusingeweza kama tusingeweka nguvu katika…

(Hapa palitokea hitilafu ya umeme ndani ya ukumbi wa Bunge na kusababisha moshi kutaanda ukumbini)

MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante sana, naomba niwape Waheshimiwa pole Waheshimiwa Wabunge kwa tafrani hii lakini naamini sasa hali ipo shwari tuendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nazungumzia suala la kuwasaidia Watanzania waweze kuzalisha rasilimali ambazo zinatokana na kufanya kazi. Nilikuwa nasema kwa upande wa uvuvi, pengine itakuwa ni jambo la busara sana Wizara ya Mifugo na Uvuvi kusaidia wananchi waingize nguvu au wafanye kazi ya kufanya fish farming. Kwa kufanya hivyo tutaweza kupunguza migogoro ya wananchi badala ya kuelekeza nguvu katika kudhibiti wananchi kuwadhibiti wasivue samaki kwenye maziwa ya asili na mito vyovyote vile production au uzalishaji samaki kwenye maziwa ya asili utakuwa umepungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nilikuwa ninaiomba sana Serikali kwa upande wa mifugo vilevile tumeshatambua mifugo yetu, tumeshaitia alama sasa kinachotakiwa ni kuwasaidia wakulima au wafugaji kwa maana hiyo waweze kuwa na masoko ya mifugo yao. Wafugaji tumepambana nao tumewatoa kwenye maeneo ya hifadhi. Wanauliza swali la msingi kwamba sawa tumetoka hifadhini tuende wapi? Kuna mkulima mfugaji mmoja kuna wakati alikuwa ananiuliza kwamba hivi hawa ng’ombe mnataka…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha muda wa Mzungumzaji)