Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kuwapa pole wananchi wa Mkoa wa Lindi na wana CCM wote wa Mkoa wa Lindi kwa msiba mkubwa uliotupata wa Mzee wetu Alhaji Ally Mtopa. Mwenyezi Mungu amuweke mahali pema peponi, amina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi lakini nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anazozifanya za kuwatumikia Watanzania na kazi zake zinaonekana. Niwapongeze pia Waheshimiwa Naibu Mawaziri wake kwa kazi ambazo wanamsaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze pia hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ambayo inaelezea mapitio na mwelekeo wa kazi katika kipindi cha 2018/2019. Vile vile niipongeze sana Serikali yangu kwa kazi kubwa inayoifanya katika kutekeleza mambo mbalimbali na mambo yote yaliyotekelezwa kwa kweli yameleta mafanikio makubwa katika nchi yetu na mambo yote yanaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mafanikio makubwa ambayo yamepatikana katika utekelezaji kwa kipindi hiki cha 2017/2018, bado tunazo changamoto mbalimbali. Nizungumzie upande wa barabara zetu. Katika bajeti hii ambayo tunategemea itaishia mwezi huu Juni, katika Mkoa wetu wa Lindi tulibahatika kupitisha bajeti ya ujenzi wa kiwango cha lami kutoka Nanganga – Luchelegwa – Nachingwea -Masasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba sana Mheshimiwa Waziri husika atakapofanya windup atueleze mpango huu wa ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami umefikia wapi maana hatuoni utekelezaji na kipindi cha mwaka huu kinakwisha bado robo moja tu tutamaliza mwaka. Pia ningependa kujua, tulitenga pia bajeti ya kufanya uthamini wa barabara inayotoka Nangurukuru - Liwale - Nachingwea nayo pia atueleze imefikia wapi katika utekelezaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nitumie nafasi hii kwa dhati kabisa kwa niaba ya wananchi wa Mkoa wa Lindi kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutekeleza ahadi yake ya kutuletea kivuko pale Lindi. Tumepokea kivuko MV Kitunda, Mheshimiwa Rais aliahidi kutoa na ameweza kutekeleza. Kwa hiyo, tunashukuru sana na tunampongeza, tunamwombea dua njema ili aweze kutekeleza mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo changamoto kubwa ya barabara inayotoka Dar es Salam – Lindi – Mtwara. Barabara hii ni mkombozi sana wa wananchi wa Mikoa hii Kusini lakini bado kuna changamoto kubwa ya barabara kuwa na mashimo mengi lakini TANROADS wanashindwa kufanya ukarabati kwa kukosa fedha. Naiomba Serikali itenge fedha kwa ajili ya kufanya ukarabati wa barabara hizi. Barabara ya Kusini ni mkombozi wa watu wa Kusini na kutuletea maendeleo wananchi wa Kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tumeona katika taarifa ya Mheshimiwa Waziri wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania namna ambavyo kilimo sasa kimeleta tija kubwa katika nchi yetu lakini bado tunaona Serikali imejipanga vizuri katika kuhakikisha inaendeleza kilimo katika nchi yetu. Ukiangalia zao la korosho ambalo sasa hivi limeendelezwa katika mikoa mingi nchini Tanzania lakini bado tuna Sheria ya Korosho ambapo kabla haijasafirishwa inatozwa export levy ambapo mapato yake asilimia 65 yanaenda katika Bodi ya Korosho na asilimia 35 inabaki katika Mfuko Mkuu wa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika fedha hizi Bodi ya Korosho inanunua pembejeo na kufika kwa wakati kwa wakulima lakini pia inanunua magunia, inazalisha mbegu bora ya korosho na inafanya mambo mbalimbali ya kuendeleza zao hili la korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016/2017 shilingi bilioni 88 zilipatikana na mwaka 2017/2018 zaidi ya shilingi bilioni 133 ziliweza kupatikana lakini fedha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja lakini naiomba Serikali irudishe fedha hizi katika chombo chetu cha Bodi ya Korosho ili iweze kufanya kazi. Ahsante sana.