Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi, tunakukaribisha tena nyumbani namshukuru Mungu aliye kukurudisha salama, karibu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza Serikali kwa uamuzi ambao umewasilishwa hapa na Mheshimiwa Waziri wa Utumishi Baba yangu Mzee Mkuchika. Nadhani mmefanya jambo jema kuona hali halisi na kuchukua hatua. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali kwa uamuzi waliouchukua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulipopiga kura mwaka 2015 Mikoa ya Lindi na Mtwara, moja ya sababu tuliamini sana kwamba uchumi wa gesi wa Mikoa ya Lindi na Mtwara ni ukombozi mkubwa na uko salama mikononi mwa Rais Magufuli na Serikali ya Awamu ya Tano. Tulipopiga kura ndiyo ulikuwa mkataba wetu siyo, kwa maneno lakini iliwekwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Spika, ukurasa wa 76 na 77 inaanzia ukurasa wa 75, eneo kubwa sana limezungumzwa uchumi wa gesi, suala la gesi na imeandikwa mafuta na gesi asilia. Kwa hiyo, kura nyingi alizozipata Magufuli ni kwa sababu ya makubaliano haya yaliyoko kwenye hii Ilani ya Uchaguzi kwamba atakwenda kuyaendeleza.

Mheshimiwa Spika, kwa summary, moja ilikuwa ni kuendela miundombinu ambayo ita-facilitate huu uchumi wa gesi wa Lindi na Mtwara. Pili, ilikuwa ni kuwandaa wananchi wanufaike na kufaidika kwa gesi na mafuta kwa Mikoa ya Lindi na Mtwara. Lipo jambo specific la ujenzi wa mradi wa LNG plant kwa Mikoa ya Lindi, kwa hiyo hili limo kweye ilani ya uchaguzi. Pili, kwenye mpango wa miaka mitano na mpango ambao umekuwa ukiwasilishwa hapa mwaka hadi mwaka.

Mheshimiwa Spika, nasikitika sana nilipoangalia hotuba ya Waziri Mkuu kuanzia ukurasa wa kwanza mpaka wa mwisho hakuna neno gesi kabisa. Inaonekana ukienda hata site kwenyewe, shughuli mbalimblai zinazoendana na gesi kwa Lindi na Mtwara ni kama vile zimeanza kufungwa na zimesimama kabisa.

Swali langu la kwanza, hivi ni bahati mbaya hotuba ya Waziri Mkuu imeshindwa kuliona jambo hili kuwa ni kubwa na ikaamua kuliacha au Serikali imeamua kuachana nalo? Kwa sababu naona jitihada kubwa zinaanza kwenda kwenye Stieglers (umeme wa maji) mimi sina matatizo nalo inawezekana ndiyo maamuzi lakini Stieglers kwenye Ilani haimo. Ilani tumezungumza nishati ya gesi tena kwa sehemu kubwa sana na hii ndiyo ilikuwa imani ya wananchi wa Lindi na Mtwara kwa Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zilikuwepo jitihada zilifanywa na Mzee Mwinyi mpaka tukapata Songosongo, jitihada zikafanywa na Mzee Mkapa, Awamu ya Nne ikaja kwenye jitihada hizi za huu uchumi ambao tulianza kupata matumaini nao.

Mheshimiwa Spika, wakati jitihada zinafanyika watu watakumbuka, kuna watu walipoteza maisha Lindi na Mtwara, kuna watu walipata majeraha na vilema Lindi na Mtwara, kuna mali za watu lakini tukaamini kuna neema kesho. Kwa hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na bahati mbaya tulimkabidhi Mheshimiwa Magufuli tukaamini liko salama, alipotupa Mheshimiwa Majaliwa tukaamini tuko salama zaidi, kwa sababu Waziri Mkuu ametoka kwetu. Sasa ni bahati mbaya sana kwamba humu ndani hakuna kabisa, maana yake ni kwamba hili jambo pengine limeanza kuachwa sasa twende kwenye Stieglers. Je, hatusaliti Ilani ya Uchaguzi ya CCM? Je, hatuwasaliti wananchi wa Lindi na Mtwara waliotupa kura na kutuamini kwamba gesi yao na uchumi wao uko salama? Hili ni bomu kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati wa mchakato hali ya kisiasa, hali ya kijamii Lindi na Mtwara kulikuwa na taabu, sasa imetulia tukiamini neema ipo, kiuchumi baada ya harakati za gesi na mafuta Kusini watu walianza kuja kuwekeza uchumi wa Lindi na Mtwara ukaanza kukua, watu wakaanza kuwekeza. Hali ilivyo sasa hivi watu wameanza kuondoka, uchumi wa Lindi na Mtwara unadorora, hali yetu ni ngumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nimuombe Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa unyenyekevu sana asikubali suala la gesi lifie mikononi mwake akiwa Waziri Mkuu wa Tanzani, siyo sawa. Nimeuliza maswali hapa mara moja, mara mbili Serikai imeendelea kusisitiza, mchakato unaendelea lakini huo mchakato ambao hauwi reflected kwenye hotuba nzima ya Waziri Mkuu, mimi nadhani tuambieni ukweli, kama limeshindikana hili hebu tujue ukweli, tusiwasaliti wananchi wa Lindi na Mtwara siyo sawa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili ukiacha gesi na mafuta, Lindi na Mtwara ni korosho. Mwaka jana kuna jitihada zimefanyika mambo yameenda vizuri, lakini Serikali ikafanya uamuzi, ikachukua kazi iliyokuwa inafanywa na Mfuko wa Pembejeo na Waziri anajua, wakasema ipelekwe kwenye Bodi ya Korosho na pembejeo hasa sulphur itagawanywa bure. Kulikuwa na mapungufu yalitokea lakini tukafumba macho kwa sababu ndiyo mara ya kwanza tukasema fanyeni uchunguzi, mlikokosea mrekebishe. Hali inavyoenda sasa hivi mwaka huu hali itakuwa mbaya kuliko tunavyodhani, kwa sababu mpaka mwezi huu wa nne wakulima hawajui chochote. Mheshimiwa Waziri, Jimbo langu mwezi huu watu wanaanza kupuliza dawa leo hawajaambiwa chochote.

Mheshimiwa Spika, wakati mnachukua mfuko ulikuwa na zaidi ya shilingi bilioni 49, walikuwa na uwezo wangeendelea nao, mkatuaminisha na tukawaamini, lakini hali inavyoendelea mbaya sana, kwa hiyo, tumaini peke yake lililokuwa limebaki Kusini ilikuwa korosho. Mnajua mbaazi imekwenda kutoka shilingi 200 mpaka shilingi 100, kuna wakulima wameacha mbaazi shambani wamesema bora zifie huko, sasa na korosho mnatupeleka huko, siyo sawa jamani! Ukiacha Lindi na Mtwara twende wapi, tuishi vipi sasa? Hili ni kutusaliti. Tulipotoa kura tuliwekeza tukaamini mtatusaidia, mkiendelea kufanya hivi mnatusaliti Mheshimiwa Waziri Mkuu na siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama imeshindikana rudisheni kwenye mfuko wa pembejeo tulikuwa tunakwenda vizuri. Kuna dhana ya kudhani kila mtu mwizi, siyo sawa, Mfuko wa Pembejeo ulienda vizuri sana. Mmebeba tumewaachieni bado mnakwenda vibaya kuliko hata mlivyochukua, hapa ni kutunyonga na siyo sawa sawa mtakuwa mnatusaliti sana watu wa Lindi na Mtwara (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri wa Kilimo anajua kuna watu bado wanadia mpaka leo malipo ya korosho. Kuna wakati fulani tulizungumza hapa, Ushirika ndiyo mkono wenu wa kusaidia kushirikiana na wakulima kuhakikisha wanapata soko, bei na mfumo mzima wa mazao yao. Hali ilivyo kule tumeweka watu, bahati mbaya elimu yao ndogo, sasa kuna mahali walikuja watu wamepata hasara ya zaidi shilingi milioni 400 na hawajui imepatikanaje, kwa nini? Wako watu wamechaguliwa uwezo hawana, sasa kwa nini tusibadilishe mfumo kwenye wale wa kuchanguliwa haya tusijali elimu yao, lakini tupate watu wa kusimamia, haya ni mabilioni ya hela yanasimamiwa na darasa la saba anashindwa kupiga hesabu, anakuja analia anatakiwa akamatwe, apelekwe Mahakamani, ukimuuliza umepotezaje hajui! Sasa kama tunashindwa hata hili la kuimarisha ushirika kwa sababau mapesa yapo, kwa nini tusiajiri watu wenye uwezo, waliosoma wakasimamia hela zetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda mpaka leo loss ni kubwa matokeo yake ni nini? Wakulima wanaambiwa wakubaliane wachangie loss inayopatikana, lakini hii loss inasababishwa na nani? Inasababishwa na wakubwa kwenye mabenki na wakubwa kwenye Ushirika ngazi ya juu, siyo hawa wa chini, hawa wa chini hawajui chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ushauri wangu kwa Serikali, la kwanza, tupitie upya mfumo wa ushirika. Pamoja na kuchaguana demokrasia safi, lakini ni vizuri tupate watu wa kuajiriwa wenye elimu ya utunzaji wa mahesabu wakashirikiane kusaidia.

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.