Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kurejea kidogo kwenye Kitabu cha Wakristo kinachoitwa Biblia, Kitabu Kitakatifu kwenye Kitabu cha Nehemia, Sura ya 1-4. Nehemia alianza kazi ya kujenga ukuta wa Yerusalemu. Wakati ameanza kujenga ukafika ngazi fulani walitokea watu waliokuwa wakiitwa akina Sanbalati na Tobia wakaanza kusema ukuta wenyewe anaojenga hata mbweha akipanda hapo unaanguka mara moja. Kwa hiyo, wakaanza kumdhihaki, kumdharau na mambo mengine mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda tu kumwambia Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Makamu wa Rais na Mheshimiwa Rais mwenyewe wajenge ukuta wa Yerusalemu, ni wakati wao sasa wa kujenga ukuta wa Yerusalemu bila kujali makelele yanayopigwa na akina Tobia na Sanbalati, kwa sababu wakiwasikiliza hawataweza kufanya cha maana kwenye nchi hii, lakini huu ni wakati waou Mungu amewapa wafanye kazi ambayo iko mbele yenu kwa ajili ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa maana wakiendelea kuwasikiliza hawatafanya kitu; wakinunua ndege watasema ndege yenyewe wananunua kwa cash wangekopa, wakikopa watasema wanaongeza deni la Taifa, wanaongeza mzigo kwa wananchi, wakijenga viwanda watasema viwanda vyenyewe vinavyojengwa ni mashine za kusaga unga na kadhalika, kwa hiyo, wakiwasikiliza watawatoa kwenye reli. Nawaambia viongozi wangu kwamba ni wakati wao mzuri, wajenge Taifa hili na wako kwenye mwelekeo mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza, niende kwenye huduma za jamii hasa upande wa maji. Mkoa wa Simiyu tuna mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria; leo ni kama miaka mwili mradi huu ulishapitishwa lakini mgogoro upo kwenye eneo litakalowekwa tanki kubwa ambalo litasambaza maji kwenye Mkoa wa Simiyu kuanzia Wilaya ya Bariadi, Itilima, Meatu na Maswa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mahali ambapo kutajengwa tenki hilo ni mahali ambapo kuna madini ya nickel, kizungumkuti kiko hapo. Mheshimiwa Rais aliwahi kuja Mkoa wa Simiyu, akasema tenki lijengwe kwenye Mlima Ngasamo mahali ambapo mwekezaji anataka kuchimba nickel, lakini bado uamuzi wa kujenga tenki hilo haujafanyika. Sasa sielewi tumsikilize nani Mheshimiwa Rais, mwekezaji au nani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikia kibali kinatafutwa kutoka kwa Kamishna wa Madini, sasa huyu Kamishna wa Madini anakaa nchi gani kwamba ameshindwa kuandika kibali ili mkandarasi aweze kuanza? Maana najua mkandarasi alishatafutwa, amepatikana na pesa zipo lakini kazi haifanyiki leo ni kama mwaka mmoja na zaidi mradi huu haujaanza. Naomba sana mradi huu wa maji sasa uanze na kama ni kibali kinachotakiwa kutolewa kutoka kwa huyo Kamishna wa Madini, basi kifuatiliwe haraka kipatikane ili mradi uweze kuanza na sisi watu wa Mkoa wa Simiyu tuweze kupata maji yaliyo safi na salama na ya uhakika zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la huduma za kiuchumi lakini niende moja kwa moja kwenye awamu ya tatu ya Mradi ya REA. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Nishati Mheshimiwa Kalemani pamoja na Naibu wake kwa sababu wanajitahidi sana kuhakikisha kwamba REA awamu ya tatu inafanya kazi yake kama ilivyotarajiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, nina tatizo kidogo kwenye Wilaya yangu ya Maswa mkandarasi aliyepangwa Mkoa wa Simiyu ambaye pia yupo Wilaya ya Maswa amepewa kilomita kidogo kulinganisha na vijiji alivyonavyo. Utakuta kwenye vijiji anapokwenda kuweka umeme anaweka kitongoji kimoja kwa sababu anasema kijiji hiki nimepewa kilomita moja na nusu au kilomita mbili, kwa hiyo, inatosha kupeleka umeme kwenye kitongoji kimoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii imezua ugomvi kwenye vijiji vyetu, kitongoji kimoja kinapata umeme vitongoji vinne kwenye kijiji hicho havipati umeme. Wananchi kwenye vijiji vinavyobaki wanauliza wao ni wananchi wa nchi gani? Wanauliza wao ni wananchi wa wapi mbona kitongoji kimoja tu kinapata umeme?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana mikataba hii ambayo Wizara ya Nishati wameingia na wakandarasi hawa hebu iangaliwe upya, vinginevyo itaacha ugomvi mkubwa kwenye vijiji vyetu kwa sababu maeneo machache tu yatapata umeme na maeneo mengine yatakuwa hayajapata umeme sasa inatuletea ugomvi sisi viongozi tunakuwa kama tumewabagua watu wetu. Kwa hiyo, naomba sana suala hili liweze kuangaliwa hasa kwenye REA awamu ya tatu hii inayoendelea lirekebishwe kwa haraka ili kwamba kama umeme unaenda kwenye kijiji basi uende kwenye vitongoji vyote. Hii habari ya kilomita mbili kwenye kijiji haitusaidii itatuletea ugomvi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye eneo la sekta binafsi lakini upande wa wafanyabiashara. Nashukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa sababu amekwishakutana na wafanyabiashara wa nchi hii na kuzungumza nao kujaribu kutatua changamoto ambazo wanazo. Najua hakika ya kwamba kuanzia Waziri Mkuu, Makamu wa Rais na Rais mwenyewe wana nia nzuri kabisa na wafanyabiashara, lakini tatizo liko kwa watendaji wa Serikali katika kutekeleza maelekezo na kazi wanazotakiwa kuzifanya ili biashara ziweze kwenda kwenye nchi hii. Watendaji wa Serikali sijui hawaelewi kitu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi wafanyabiashara kutoka kwenye Wilaya yangu wanafanya biashara ya ng’ombe wanavusha ng’ombe kutoka kwetu kwenda Dar es Salaam wamefika hapa Dodoma wanasimamishwa halafu wanaulizwa leseni yenu iko wapi, leseni wanaionesha, kisha wanaulizwa mwenye leseni yuko wapi, mwenye leseni hayupo tunawapiga faini Sh.500,000. Sasa najiuliza mwenye leseni ya kupeleka ng’ombe Dar es Salaam naye apande kwenye gari ambalo limepakia ng’ombe? (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vitu ambavyo kwa kweli havieleweki kwa hawa watendaji wetu. Huyo mwenye kufanya hiyo biashara na mwenye leseni ana watu wake wanaowasafirisha wale ng’ombe na yeye mnataka apande kwenye hilo roli?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naunga mkono hoja.