Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia Hotuba ya Bajeti ya Waziri Mkuu. Kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunijalia na mimi niweze kuchangia katika Bunge lako hili Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Rais wangu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya, kwani naamini kabisa mwenye macho haambiwi tazama. Pia niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa, kwa kazi kubwa anayoifanya sambamba na kumpongeza Waziri Jenista pamoja na Timu yake Naibu Waziri Mheshimiwa Ikupa na Mheshimiwa Mavunde, kwani Watanzania wanaona kazi mnayoifanya hongereni sana. Sisi tunaamini hatuna cha kuwalipa ila Mwenyezi Mungu mwenyewe ndiye atajua cha kuwalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika kuchangia sasa. Wenzangu wameshachangia mambo ya bomba kutoka Hoima Uganda kuja Tanga. Niendelee kupongeza juhudi hizo za Mheshimiwa Rais kwani Mheshimiwa Rais anatupenda sana, naamini kabisa Watanzania sasa itakuwa ni fursa ya kupata ajira katika bomba lile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nipongeze kupanuliwa kwa Bandari au kuongezwa kina cha bandari pale Tanga, nimpongeze Rais wangu kwa kutupa pesa na kazi ile inaendelea kupanua bandari ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo niiombe Serikali yangu sasa Tukufu kwamba vitu vyote hivi viende sambamba na standard gauge hiyo ambayo itaanzia Tanga kwenda Arusha mpaka Musoma. Naomba Serikali yangu tukufu iende sambamba na reli hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo tuna uwanja wa ndege wa Tanga. Kwa kuwa tayari tuna Bombardier, kwa hiyo niiombe Serikali sasa Bombardier ile iweze kufika Tanga. Ianze Dar es Salaam iende Pemba ije Tanga hadi Mombasa, naamini hiyo sasa ni fursa yetu pamoja na upanuzi wa uwanja ule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kupongeza hayo niende moja kwa moja sasa kwenye suala la afya. Nimshukuru Rais wangu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kunitengea milioni mia saba kwa ajili ya Kituo cha Afya Mlola, milioni mia nne kwa ajili ya majengo na majengo yale tayari mpaka sasa hivi yako kwenye hatua nzuri, mengine yanapauliwa, mengine yanafanyiwa usafi na mengine yako kwenye mtambaa wa panya. Mheshimiwa Rais, ahsante sana Mungu akubariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hayo kuna juhudi za wananchi zinaendelea kufanyika kule, kuna vituo vya afya zaidi ya viwili vinajengwa pale; Kituo cha Afya Gare na Kituo cha Afya Ngwelo. Kwa hiyo, niiombe Serikali kwa kuwa vituo vile vinajengwa kwa nguvu za wananchi…

T A A R I F A . . .

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hiyo siikubali hata yeye anajua kwamba Rais ndiye Mkuu wa Nchi, ndiye mwenye maamuzi yote. Kwa hiyo wafu ngoja wakazike wafu wao, sisi tuendelee kutangaza injili. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vituo vya afya viwili ambavyo vinajengwa kwa nguvu za wananchi. Sasa niiombe Serikali iweze kupeleka pesa kwa ajili ya kumaliza vituo vya afya vile, ambavyo ni Kituo cha Afya Gare na Kituo cha Afya Ngwelo. Sambamba na hayo kuna Zahanati zaidi ya 19, zahanati zile ziko kwenye nanii tofauti tofauti. Kuna ambazo zinahitaji watumishi na kuna ambazo zinahitaji kumaliziwa, kwa hiyo niiombe Serikali yangu tukufu kwamba ipeleke mafungu sasa…

T A A R I F A . . .

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, saa nyingine hawa watu wakitoa taarifa usiwaruhusu kwa sababu Bunge ndilo linalotenga Bajeti Serikali inatekeleza. Kwa hiyo, mtu wa kwanza kabisa kutekeleza na kutoa maelekezo ni Rais.

T A A R I F A . . .

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ya Mheshimiwa Ulega naipokea kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema awali kwamba naomba sasa Serikali katika bajeti hii itenge pesa kwa ajili ya kwenda kumalizia vituo vile vya afya ambavyo ni Kituo cha Gare na Ngwelo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo, niende kwenye suala la umeme. Kwanza nimpongeze Waziri, Mheshimiwa Dokta Kalemani na Naibu Waziri, Mheshimiwa Subira Mgalu kwani wanafanya kazi kubwa sana. Watu wa REA, sisi tumepangiwa mkandarasi anaitwa DEM Contractors, huyu bwana alikuja mara moja tu mpaka leo hajaonekana na vijiji na vitongoji vyote ambavyo vimepangiwa bado hajavifanyia kazi, amekuja kupima kama vitongoji viwili, vitatu ameondoka moja kwa moja. Niiombe sasa Serikali Tukufu kwamba mkandarasi yule atafutwe popote alipo aende akatekeleze ile miadi ambayo wameahidiana na Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu.Kuna maboma mengi sana ya maabara yamejengwa lakini maboma yale mpaka sasa hivi yamekuwa ni magofu. Kwa hiyo, niiombe Serikali sasa ichukue hatua madhubuti kuhakikisha kwamba inakwenda kumaliza maboma yale kwani maboma yale yalikuwa yanajengwa na nguvu za wananchi, kwa hiyo tunapoyaacha vile yalivyo wananchi sasa hivi hata uwezo hawana. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu Tukufu sasa imalizie maboma yale ili watoto wetu waweze kusoma elimu kwa vitendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, Wilaya ya Lushoto tangu iumbwe ina wananchi wengi sana lakini haijawahi kupata Chuo cha VETA. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu, hususan Wizara; Waziri wa Elimu naomba atakaposimama pale aniambie lini atanitengea pesa za kujenga Chuo cha VETA Lushoto. Kuna sekondari zaidi ya 105, kwa hiyo nimwombe Waziri wangu atakapo-wind up hapo basi aniambie kwamba ni lini atatenga mafungu hayo kwa ajili ya kujenga Chuo cha VETA Lushoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo, niende kwenye barabara; wenzangu wameongea mambo ya TARURA, ni kweli lakini mimi nilichoona TARURA ni watu wazuri sana ila naamini bado hawajatengewa mafungu kwenda kule. Mfano mimi ninachoongea, barabara zangu pale Lushoto Mjini bado ni tatizo, kuna mashimo makubwa sana, hata nikipita pale wananchi wananiuliza hivi Mheshimiwa Mbunge upo, hivi hii hali unaiona? Kwa hiyo niiombe sasa Serikali ipeleke mafungu kwenye Taasisi ya TARURA iweze kujenga barabara zile sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, kuna barabara ambayo kila siku naiongelea hapa, Barabara kutoka Mlalo – Ngwelo – Mlola – Makanya – Mlingano hadi Mashewa ambayo ni kilometa 57.7, barabara hii imeshasemwa mara nyingi, kabla ya mimi kuingia Bungeni waliopita wameshaizungumzia barabara hii tangu 1995, lakini barabara hiyo mpaka sasa hivi bado haijapandishwa hadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwombe Waziri sasa, Mheshimiwa Profesa Mbarawa, atakapo-wind up hapo anipe majibu barabara ile itapandishwa hadhi lini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo kuna barabara ya mchepuko ambayo ni kilometa 16, inaanzia Dochi – Nguli hadi Mombo. Nimwombe sasa Waziri barabara ile iweze kutengenezwa kwani barabara ile ni barabara mbadala ambayo barabara hii kubwa ya kutoka Soni – Mombo ikiziba basi barabara ile inatusaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, twende kwenye walemavu, ukurasa wa 24; nimeona walemavu wametengewa vitu vingi kidogo, lakini upande wa vijijini walemavu hawa wamesahaulika. Niiombe Serikali yangu sasa itakapotenga pesa hizi basi ipeleke vijijini kwani vijijini kuna walemavu wengi sana ambao wamesahaulika, kwa hiyo niiombe Serikali yangu tukufu iweze kutenga pesa ili iweze kuzipeleka vijijini. Ukizingatia mazingira ya vijijini miundombinu si rafiki, mnaifahamu wenyewe hata Mwenyekiti naamini unaifahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la maji; kama unavyojua maji ni uhai na katika mwili wa binadamu maji ni asilimia 75. Kwanza niipongeze na niishukuru Serikali yangu kwa kunitengea milioni mia saba sabini kwa ajili ya Mamlaka ya Maji Mjini. Pia niendelee kuipongeza kunitengea milioni mia tano kwa ajili ya mradi wa Ngulu – Kwemashai na pia niipongeze Serikali kwa kunipa milioni mia nne hamsini kwa ajili ya maji Mlola.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna mradi ambao una miaka mingi sana, mradi wa kutoka Mtumbi kuja Kwekanga, kuja Malibwi kuja Kilole kwenda mpaka Mbwei, mradi huu ni wa miaka mingi sana, kwa hiyo niiombe Serikali yangu sasa iweze kutenga pesa awamu hii ili tuweze kutekeleza mradi ule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo, kuna mradi ambao unatoka Lushoto kwenda Mkuzi kupitia mpaka Kwemakande, mradi ule walishafanya feasibility study (upembuzi yakinifu), lakini mpaka sasa hakuna kinachoendelea ambapo mradi ule unagharimu shilingi bilioni moja na milioni mia sita, ambapo ukitekelezwa utatoa kabisa changamoto au utatatua matatizo ya maji katika maeneo hayo niliyoyataja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, mimi niko kwenye Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii; tulienda Mkoa wa Geita tukaenda mpaka Mkoa wa Kagera, nilikuwa na rafiki zangu Mheshimiwa Kalanga, Mheshimiwa Nassari na wengineo, tuliona pale Chato Uwanja wa Ndege Chato. Kwa hiyo niendelee kumpongeza Rais wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine walikuwa wanasema uwanja ule hauna maana, uwanja ule una mapori matatu wanaita BBK (Biharamulo, Burigi na Kimisi), kwa hiyo uwanja ule naamini kabisa utatoa fursa kubwa sana. Ningetegemea wenzangu hawa wamuunge mkono Rais kwamba juhudi alizozifanya ni juhudi ambazo zinatakiwa tumwombee dua, lakini… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.