Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kusema katika hotuba ya mtani wangu Waziri Mkuu kwa niaba ya wananchi wa Kilwa Kaskazini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na Maadhimisho ya Sherehe za Vita vya Majimaji. Historia inaeleza wazi kwamba Vita ya Majimaji ilianza Kilwa na sababu kubwa ya kwa nini Wahenga wetu wale walianzisha ile vita, ni kwa sababu walikuwa wanakataa kunyanyaswa, wanakataa kunyang’anywa ardhi yao, wanakataa uonevu, lakini walikuwa na ujasiri mkubwa wa kupambana na Mkoloni Mjerumani ambaye alikuwa anatisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi watu wa Pwani tuna misemo yetu ambayo ina maana na hekima kubwa. Watu wa Pwani tunasema, raha ya maji ya dafu yanywewe kwenye kifuu chake. Maji ya dafu yakinywewa kwenye bilauri hupoteza ladha. Yakinywewa kwenye bilauri hupoteza sifa na harufu yake. Tabia ya dafu ukilipasua ukatoa mzibulio, ukachokoa basi sharti unywe kwenye kifuu chake. Ukichukua yale maji kuyapeleka kwenye bilauri, ladha inapotea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ni nchi inayojitambua. Siamini kama inafanya mambo yake hovyo hovyo. Kila linalotokea ni historia! Katika hali ya mshangazo, watu wa Kilwa tunashangaa kwa nini Sherehe za Vita ya Majimaji zinazogharamiwa na bajeti ya Serikali zinafanyika Songea na siyo Kilwa, Nandete? Hatuelewi! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, waandishi mbalimbali wanazungumzia Vita ya Majimaji. Mwandishi Clement Gwasa anasema, Vita ya Majimaji ilikuwa planned na sababu zake zilianza toka mwaka 1903 na kuja kupigana mwaka 1905. It was very, very planned. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwa ninajiuliza, hivi ni vigezo gani vilivyotumika kuzipeleka zile sherehe zinazotambuliwa na Serikali Songea? Kwa sababu kama hoja ni watu kunyongwa, hata sisi viongozi wetu wa Kilwa walinyongwa. Kinjekitile alinyongwa; na Hassan Omar Makunganya alinyongwa. Ukisoma kitabu cha The Majimaji Uprising kinasema, kiongozi wa ndugu zangu, watani zangu akina Mheshimiwa Jenista, Wangoni wa wakati huo, aliposhawishiwa ajiunge na kumwondoa Mkoloni Mjerumani, yeye alisema hana muda kwa sababu Mjerumani ni rafiki yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilipofikia wakati wa Vita ya Majimaji, Chabruma aliamua tu kujiunga na mapambano ya Vita ya Majimaji kwa sababu binafsi na sababu yenyewe aligundua kwamba mke wake, Bi mdogo, si mwaminifu katika ndoa. Kwa sababu hiyo akaamua kwenda kwa DC kwenda kulalamika. DC akamwambia kama hivyo ndivyo, basi naomba uniletee ushahidi. Huyu kiongozi Chabruma alishindwa kupeleka ushahidi kwa DC, ndipo basi akaona kumbe hawa Wajerumani hawafai, basi na mimi nitaungana na Wamatumbi kumwondoa Mjerumani. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama sisi tuliamua kupambana vita kwa sababu ya kutetea Utaifa wetu, ardhi yetu na umoja wetu, hivi nani sasa anastahili kupewa heshima kitaifa? Ni yule aliyejiunga na Vita ya Majimaji kwa sababu binafsi au sisi tuliokuwa tuna lengo la kuwaunganisha Watanzania? Haya mambo yanaumiza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania tumefanya mambo mengi, sisi ndiyo Taifa ambalo tulithubutu kuhakikisha kwamba nchi zote kusini mwa Afrika zinapata uhuru. Mwalimu Nyerere kwa sababu zake binafsi akaona hapana, lazima hawa wenzangu wapate uhuru. Sasa kama itatokea mtu akasema heshima hii ya sisi kuthubutu ipelekwe Rwanda, ni kitu ambacho hakieleweki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwa najisikia kutetemeka ninapomwona Mkuu wa Majeshi anaenda pale Songea eti kwamba wale ndio majemedari wa Vita ya Maji Maji. Haieleweki! Naomba mtani wangu, Mheshimiwa Jenista, kalifanyie kazi hili, watu wa Kilwa tupate haki yetu kwa sababu ya ujasiri wa kuthubutu kumwondoa mtawala mkali sana, Mjerumani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri hilo litaeleweka. Nilishauliza maswali hapa, ndugu yangu Mheshimiwa Mwinyi akanijibu vizuri sana, nikataka ufanyike upembuzi wa kihistoria, lakini kuna hoja pia ya sisi waathirika wa Vita ya Majimaji tulipwe fidia kama ambavyo wenzetu wa Kenya wamelipwa, wenzetu wa Namibia wamelipwa. Hakuna chochote kimefanyika, naomba hili lizingatiwe kwa sababu historia ni jambo muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende sasa kwenye suala la watu wenye ulemavu; ukurasa wa 24 na 25 katika hotuba ya Waziri Mkuu anazungumzia suala la watu wenye ulemavu. Anaeleza kwamba Serikali pamoja na wadau wamechangia vifaa kwa watu wenye ulemavu. Amesema wametoa viti mwendo 240, wamechangia magongo ya kutembelea 350, bajaji sita, kofia pana 128, fimbo nyeupe 175, miwani maalum 70, shime sikio 20, vyerehani vinane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wenye ulemavu Tanzania na idadi hii ya vifaa vilivyotolewa na Serikali, nafikiri ni utani kwa watu wenye ulemavu. Walemavu wana mahitaji maalum kutokana na aina ya ulemavu walionao. Kuwa mlemavu siyo planned, ni suala linalotokea kwa bahati mbaya. Serikali bado haijaangalia mahitaji muhimu ya walemavu kutokana na aina yao ya ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mlemavu wa ngozi hakuchagua kuwa mlemavu wa ngozi; na hitaji lake maalum kulingana na aina yake ya ulemavu, ni kupata mafuta maalum ambayo yatamsaidia kupambana na athari za miale ya jua. Sasa kama haya mahitaji hayatolewi bure na Serikali, mimi bado sielewi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mlemavu asiyeona apate fimbo maalum; mlemavu kiziwi apate shime sikio; mlemavu wa viungo apate viungo bandia. Katika hali ya kushangaza, kati ya vitu vinavyouzwa kwa bei ya juu ni pamoja na viungo bandia. Vifaa hivi ni hitaji maalum kwa walemavu kulingana na aina yao ya ulemavu, vitolewe bure na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye ajira ya Watendaji wa Vijiji wa darasa la saba. Kadri siku zinavyozidi kwenda mbele kasi ya watumishi wa Serikali hasa wa kada ya chini kuichukia Serikali inaongezeka. Ni kwa sababu Serikali haijajipanga katika kuhakikisha haki za watendaji wa chini zinazingatiwa. Watendaji wa vijiji wameondolewa kienyeji eti kwa sababu wao ni darasa la saba... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)