Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Hotuba ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza Seriakli yetu kwa kazi nzuri inayofanya, na hapa nitoe pongezi za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais kwa jitihada anazofanya katika kuwatetea wanyonge wa taifa hili; Waswahili wanasema kwamba mti wenye matunda ndiyo unaopigwa mawe na hili tunalishuhudia. Nimpongeze pia Waziri Mkuu, Makamu wa Rais, nimpongeze sana Dada yangu Jenista Mhagama kwa kazi nzuri anayoifanya pamoja na wasaidizi wake Mheshimiwa Ikupa pamoja na Mheshimiwa Mavunde.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuchangia hotuba hasa katika ukurasa wa 24 ambako kumezungumziwa huduma kwa watu wenye ulemavu. Tumeona jitihada za Seriakli katika kusaidia kundi hili la watu wenye ulemavu, na nitoe pongezi za dhati kwa jitihada zinazofanywa. Kwa mfano, tumeshuhudia kuanzia mwaka jana vifaa kwa ajili ya watoto wenye mahitaji maalum vimepelekwa katika shule mbalimbali ingawa bado uhitaji ni mkubwa, kwa hiyo, niisisitize tu kwamba Wizara kuendela kuangalia na hasa maeneo mengi ya vijijini kwa kweli bado uhitaji ni mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze pia kwa kuona umuhimu wa kuboresha vyuo vya watu weye ulemavu, kwa mfano Chuo cha Yombo ambacho kilikuwa ni msaada mkubwa sana katika kuwajengea uwezo, kuwapa ujuzi watu wenye ulemavu ambao walikuwa wakitoka hapo wanakwenda kujiajiri wao wenyewe na si kutegemea tena ajira.

Kwa hiyo, hiki chuo ni muhimu sana na niisisitize Wizara katika kuhakikisha kwamba kweli wanaboresha na kukirudisha katika ule ubora uliokuwepo pale awali na kuongezea pia na wakati huu tulionao hivi sasa wa karne ya sayansi na teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisisitize tu pia kwamba katika vyuo hivi mbali ya chuo hiki cha VETA, lakini tuone pia katika Vyuo vya VETA ambavyo tunaona kabisa kwamba vinazalisha vijana na vinawajengea uwezo. Katika vyuo hivi nitoe mfano tu ambapo katika kipindi kilichopita nilikuwa Mjumbe katika Kamati ya PIC ambako tuliweza pia kukutana na VETA. Mimi masikitiko yangu ni kwamba VETA kwa kweli hawana kipaumbele kwa ajili ya watu wenye ulemavu. Kwa hiyo, hapa nisisitize Serikali kuhakikisha kwamba vyuo vyote hivi vinajali kundi hili ili kuhakikisha kwamba tunawajengea uwezo kuwapa ujuzi wakitioka pale waweze kwenda kujiajiri wao wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu asilimia mbili; tangu jana pia tumeona hata katika maswali ya Waheshimiwa Wabunge tumeona uhitaji wa kundi hili. ni kweli kabisa kwamba katika bajeti ya mwaka jana, Waziri alitoa ahadi na alitoa tamko kwamba sasa ile asilimia 10; asilimia nne iende kwa wanawake na asilimia mbili iende kwa vijana na asilimia mbili kwa watu wenye ulemavu. Sasa hili lilikuwa ni tamko, ninasisitiza na kuona uhitaji kwamba Mheshimiwa Waziri utakapokuja hapa tunahitaji sheria, kwa sababu kukiwepo na sheria, sheria hii itatoa muongozo, itawaelekeza wakurugenzi na hakuna Mkurugenzi ambae sasa ambaye atafanya kwa utashi wake bali atafanya kwa kzuingatia kanuni, sheria na taratibu zilizopo kwa ajili ya watu hawa wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wenye ulemavu kwenye mabenki hawakopesheki na hawakopesheki kwa sababu dhana iliyopo miongoni mwetu bado watu wengi wana ile dhana potofu ya kuona kwamba huyu mwenye ulemavu hawezi kurudisha huo mkopo, kwa hiyo, hii asilimia mbili mimi nasisitiza tuone umuhimu kwamba hili ndilo kimbilio lao, ndilo tegemeo lao kwa kuwapa asilimia hii mbili waweze kujiajiri kwa kufanya biashara mbalimbali.

Tumeshuhudia; hizi zitawawezesha wao kuondokana na hali ngumu ya maisha na wakati wenyewe uliopo hivi sasa. Kwa hiyo nasisitiza umuhimu na ninaomba sana dada yangu mpendwa, dada mkubwa Jenista Mhagama utakapokuja hapa basi uje kutupa majibu na nitafurahi nikisikia ni tamko na utueleze kama ni sheria au kanuni na taratibu zitaandaliwa lini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza pia Wizara hasa Ofisi yangu hii ya Dada yangu Jenista Mhagama kwa jitihada wanazofanya kwa kuhakikisha kwamba kundi la vijana linawezeshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia kilimo, kilimo hiki tunaangalia ni kwa namna gani tunawawezesha vijana, vijana ndiyo nguvukazi ya Taifa. Vijana hawa mikopo ambayo ipo na tumeona kwamba mikopo hiyo baadhi wamekuwa wamefaidika na vijana wengi hivi sasa wanahamasika tuone sasa ni kwa jinsi gani tutawajengea hawa vijana na kuwapa hii mikopo wajiingize kwenye kilimo. Kilimo chenyewe ambacho tunakihitaji hivi sasa ni kilimo cha kisasa, kilimo biashara. Kilimo hiki biashara kitawawezesha vijana waweze kujiajiri wao wenyewe na kupunguza basi lile tatizo la ajira. Kwa mfano, hizi green house ni muhimu sana, vijana wengi tumeshuhudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wakiwezeshwa kwa kupitia hii mikopo na vijana hawa wakaandaliwa mafunzo kupitia ujasiriamali mbalimbali wataweza wao wenyewe, kwa sababu kikubwa kinachohitajika pia ni elimu. Katika kilimo wakiwezeshwa; tunaona kwamba kuna ufugaji wa kuku, kuna ufugaji wa samaki vyote vinaingia katika kilimo biashara. Kwa hiyo naisisitiza sana na naiomba sana Serikali tuone umuhimu wa kuwawezesha vijana hawakwa kuwapatia hiyo mitaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona pia kwamba program ya kuwawzesha vijana katika Vyuo vya VETA, tuangalie sasa, tunapokwenda katika sekta ya utalii kwa wenzetu utaratibu mzuri wanaoweka ni haa kuhakikisha kwamba vijana hawa kwa mfano, wanaofanyakazi katika sekta hii ya utalii wanapata elimu ambayo customer care ni muhimu sana. Ukienda nchi za Kenya jinsi ambavyo wenzetu wanavyoweza kuhudumia ile customer care ni muhimu sana; kwa hiyo na sisi huku kwetu kama tumedhamiria kuona kwamba tunawawezesha vijana wetu kwenda katika mafunzo hayo kwa mfano kupitia programu ya Chuo cha Utalii, vijana wetu watumike kupata ujuzi lakini pia wafundishwe jinsi ya ule ukarimu wa kuwapokea wageni wanaofika hapa. Tunafahamu sekta ya utalii ni pana na inaongeza pato katika nchi hii, kwa hiyo, tuwawezeshe katika hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hilo tu, kuwepo na programu, kwa mfano; Wizara hii husika kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu hata madereva taxi wapatiwe mafunzo, kwa mfano wanapokwenda kumpokea mteja ajue ile namna gani ya kuweza kumpokea mteja kwa ukarimu ili kwamba anapoondoka ibaki ile sifa yetu kuwa Watanzania kama ilivyo kwamba sisi ni wakarimu. Kwa hiyo, kwa kupewa mafunzo hayo hata hawa madereva taxi watajua, hata mgeni kama anasahau kitu kwenye gari ni rahisi sana kuangalia ni kwa namna gani ya kuweza kumsaidia huyo mgeni anayefika hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie katika ukurasa wa 18, suala la ajira. Ninasisitiza ni kazi nzuri, mpango mzuri ambao umeandaliwa wa kukusanya kanzidata kwa wahitimu wenye mahitaji maalum. Nasisitiza tena kwamba wapo vijanaa wengi wamemaliza vyuo vikuu wenye ulemavu, wasioona, viziwi na wengine wengi tuone kwamba ile asilimia tatu inazingatiwa siyo kwa Taasisi za Serikali tu hata katika private sector. Sasa hivi tupo katika suala zima la viwanda, katika viwanda hivi je, tunawaandaaje watu wenye ulemavu ili na wao basi waweze kuingia huko, wapate ajira na kuweza kufanyakazi huko kuhakikisha kwamba tunawaondoa katika dimbwi kubwa la umaskini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Ofisi ya Waziri Mkuu itusaidie katika Mkoa wa Arusha, Wilaya ya Arumeru katika kijiji, Kata ya Oldonyowasi maji yenye fluoride yanatuumiza watu wa kule. Ukienda kule utakuta watoto wanapinda miguu na wazazi/wamama na vikongwe wanapinda migongo. Naomba sana watalaam mbalimbali wameshafanya utafiti tatizo ni kubwa naomba sana. Na Mheshimiwa Dada yangu Jenista utakapokuja naomba pia utueleze kwa sababu mwaka jana tumeona Waziri Mkuu kweli ametupatia mradi na kwa mara ya kwanza ndani ya miaka 50 tumepata maji. Kwa hiyo, naomba sasa katika Kata hii ya Oldonyowasi tuone ni kwa jinsi gani tunaweza kupunguza tatizo la madini ya fluoride. Ahsante sana.