Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa siku ya leo kuchangia katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, napenda kupongeza hotuba nzuri ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, lakini napenda kupongeza kazi nzuri zinazofanywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi, ikiongonzwa na Rais wetu John Pombe Magufuli. Pamoja na pongezi hizo ningependa kutoa mapendekezo mawili, matatu, naomba sana kwenye hili Waziri wa Fedha anisikilize.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2009 Serikali iliamua kuanzisha export levy kwenye zao la korosho, katika hili kulikuwa na utaratibu na sheria ilieleza matumizi halisi ya ile export levy. Katika matumizi hayo mojawapo asilimia 65 itarudi kwa wananchi wenyewe na asilimia 35 itaenda Hazina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana naishukuru Serikali ilifanya vizuri ilitoa pembejeo za sulphur bure kwa wakulima wetu, ilitoa magunia kwa wakulima wetu bure. Lakini kisayansi tunaweza kusema kwamba siyo bure kwa sababu hakuna zao lolote la biashara ambalo linatoza export
levy. Lengo la export levy ilikuwa ni ku-discourage exportation of cashew na ku-incourage uzalishaji ubanguliwa wa korosho hapa nchini, hili lengo bado halijafa lipo kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli hiki ni kizungumkuti mpaka leo hii dalili ya sulphur hakuna wala magunia na ile pesa tukitaka tuzungumze ukweli, kila mkulima katika kilo moja ya korosho anachangia zaidi ya shilingi 500 jambo ambalo ni kubwa na kwa kila mkulima ukipiga hesabu mwaka huu uliopita tumepata zaidi ya bilioni 160. Ukipiga hesabu ya asilimia 65 ya bilioni 160 inatakiwa zaidi ya bilioni 100 irudi kwenye sekta ya korosho na huko kwenye sekta ya korosho tayari kuna sheria imesema matumizi ya ile pesa inaenda kwenye utafiti, inaenda kwenye ubanguaji, inaenda kuendeleza zao lenye na hata hizi korosho wanazopanda Singida, sijui wapi, Mbeya inatokana na pesa hii ambayo inazalisha mbegu wanapelekewa wenzetu ili kuzalisha korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa hili wenzetu na wenzangu tulioko kwenye Kanda ile tunayozalisha korosho ni kilio kikubwa na usione ajabu mwaka 2020 nusu ya hao wasirudi kwa sababu wakulima wanajua kwamba asilimia 15 au dola 160 kwa tani moja inakuwa charged kama export levy. Leo tunataka kuwanyima haki yao ya kuwapa pembejeo aidha kwa ruzuku au kama tulivyofanya mwaka jana kupewa bure. Naomba sana sheria ifuate mkondo wake, export levy imeeleza kwa urahisi, vizuri namna ya kutumia ile pesa kwenye zao la korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pesa ile siyo ya Serikali, pesa ile ni ya wakulima wa korosho. Kama nilivyosema mwanzo zaidi ya shilingi 500 kwa kilo moja imekuwa-charged kama export levy. Naomba sana jambo hili msitutwishe mzigo, wenzenu tutakuwa kwenye hali ngumu, biashara ya mwaka 2020 inataka kufia hapa kwa sababu jambo hili hakuna asiyelifahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nitaweza kuongelea pamoja na hilo kwenye kilimo ni suala la ushirika. Mwaka jana nililiongea sana hapa nashukuru Serikali ni sikivu tayari imeunda Tume ya Ushirika kwa upande wa Mwenyekiti na Makamishna, lakini Tume hii inaishia mikoani, kwenye Wilaya ambako ndiko usimamizi wa ushirika upo hatuna watendaji, tunategemea watendaji ambao wameajiriwa na Halmashauri na wale wanapewa kazi kubwa ya kukusanya mapato tu ya Halmashauri, kazi ya ushirika hii hawafanyi ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwa kuwa Serikali imedhamiria kufufua ushirika, basi ni vema Serikali iendeleze mtandao wa wafanyakazi mpaka maeneo ya Wilayani ili matatizo madogo yaliyotokana na mfumo wa stakabadhi ghalani inatokana na mfumo wetu mbovu wa kusimamia wanaushirika ndiyo maana tumefika hapo tulipo.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nimeisifu sana hotuba ya Waziri Mkuu, imesema ina dhamira ya dhati kwenye mazao makuu ya biashara kuweka mfumo wa stakabadhi ghalani. Hakuna asiyejua ndani humu leo tunazungumza vizuri Mtwara, tunazungumza vizuri Lindi, Tunduru kwa sababu ya mfumo wa stakabadhi ghalani. Wakulima wananeemeka sana kwa bei nzuri kwa sababu ya mfumo wa stakabadhi ghalani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri Mkuu usikate tamaa pamoja na Waziri wa Kilimo. Mtwara haikuwa kazi rahisi watu kuwageuza kufika kwenye mfumo wa stakabadhi ghalani. Utapata vijembe kwa sababu inakata mirija ya wale wote ambao walikuwa wanafaidika na mfumo ule holela. Naomba sana ili kumsaidia mkulima wa kahawa, tumbaku, pamba kama ilivyofanywa kule Mtwara basi mazao hayo kama dhamira ilivyo yaingie kwenye mfumo wa stakabadhi ghalani.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ningependa kuliongelea ni suala la afya. Naishukuru Serikali nimepata kituo kimoja cha afya kinaendelea kujengwa, naishukuru sana Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Lakini pamoja na hayo nina kata 15, katika kata 15 nina zahanati 21 na katika hizo kata 15 nina vituo vya afya vitano tu, mtu anatembea zaidi ya kilometa 15 kufuata huduma ya afya. Naomba sana hii mikoa ya pembezoni hebu tuangalieni tuna hali ngumu sana kwenye afya. Tunapakana na Msumbiji wateja wengi wanaohudumiwa na zahanati zile wanatoka Msumbiji. Kwa hiyo tunaomba sana jitihada ziendelee kufanyika kuhakikisha kwamba haya maeneo ambayo yako pembezoni yanapewa huduma za afya ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo vituo vyangu hivyo 22 kila kituo au zahanati ina watumishi wawili au mmoja. Kwa hiyo, mmoja akiugua anaenda hospitali maana yake kituo kinafungwa, mmoja akifuata mshahara mjini maana yake kituo kinafungwa. Mwaka jana alikuja Naibu Waziri ambaye sasa hivi ni Waziri kamili wa TAMISEMI Mheshimiwa Selemani Jafo aliona matatizo ya upungufu wa wafanyakazi Tunduru na alituahidi akasema mko miongoni mwa wale sita ambao mna tatizo kubwa la wafanyakazi. Ukweli afya ya Tunduru inalegalega kwa sababu hatuna wahudumu, tuna ukosefu zaidi ya wafanyakazi 700 wa afya. Sasa hili jambo ni tatizo kubwa na halileti afya kwenye utawala wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo suala la elimu, nitaendelea kushukuru elimu bure lakini nitaeleza mapungufu ambayo yamejitokeza na elimu bure. Tumesajili watoto wengi, wako madarasani, ukitembea huko vijijini utakuta darasa moja kuna madarasa mawili huku 120 huku mi120 wameweka pazia katikati. Huku wanafundisha darasa la kwanza huku wanafundisha darasa la pili, kwa kweli majengo ni tatizo. Hata hayo yaliyokuwepo yamejengwa miaka ya 1975/1970 utawala wa Nyerere, mpaka leo yanauliza tuue lini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na majengo hayo vyoo ndiyo kabisa hakuna. Nyumba za walimu ni mtihani, katika hili nashukuru Mkuu wa Mkoa aliyepita alihamasisha sana ufyatuaji wa tofali katika kila kijiji kuwa na tofali laki moja. Lakini tuliwaahidi kwamba mkiwa na tofali Halmashauri itatoa fedha kununua vile vitu vya madukani, lakini kwa kuwa Halmashauri ile ni kubwa ina jumla ya kata 39 Halmashauri inashindwa. Yale matofali yanageuka kuwa kichuguu, hivi inakuwa mbogo kwetu hata unavyoenda kwenye mikutano ya hadhara swali la kwanza unaulizwa matofali haya yatatumika lini.

Kwa hiyo, naomba sana kwa kuthamini ule mchango wa wananchi wale waliofyatua tofali zile nyingi basi Serikali ione namna ya kusaidia wananchi hawa waweze kupata fedha ili madarasa, vyoo na nyumba za walimu ziweze kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho katika hili ni suala la afya ni suala la wagonjwa wa UKIMWI. Kama nilivyozungumza mwanzo zahanati ziko chache, vituo vya afya viko vichache hata vituo vyenyewe vinavyotoa huduma ya wagonjwa wa UKIMWI ni tatizo. Mgonjwa anatembea zaidi ya kilomita ishirini, kumi na tano kufuata dawa. Nadhani imefika mahala pamoja na kwamba misaada inapungua basi tufikirie nilisikia jana hapa kuna marekebisho ambayo yanaweza kufanyika kwenye masharti inayoonesha namna ya kutumia asilimia kumi, basi naomba katika hilo hata angalau mtakapoweka walemavu asilimia mbili au moja basi na hawa wagonjwa wa UKIMWI muwatengee asilimia moja au mbili waweze kujikimu ili waweze kufanya kazi zao vizuri, wapunguze stress za maisha.