Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi kutoa mchango wangu katika Wizara hii ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Nachukua fursa hii pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara ya Kilimo kwa hotuba yao nzuri na mikakati waliyoiweka katika mipango yao ya kilimo. Kwanza, nachukua fursa hii kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, lakini nina ushauri kidogo wa kuongezea nyama katika mipango ya kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na Mheshimiwa Waziri anaposema kwamba ukitaka mali utaipata shambani na anasema vijana wengi tuelekee huko ndiko tutakapoipata mali. Nimkumbushe Mheshimiwa Waziri, mali hiyo huko inapatikana ukiwa na ardhi tu na miongoni mwa matatizo makubwa yaliyopo sasa hivi nchini kwetu ni migogoro ya ardhi hasa kwa wakulima na wafugaji, kama alivyoielezea vizuri katika kitabu chake, lakini kwa bahati mbaya, na ninaisema kwa bahati mbaya kwa sababu naujua umahiri wa Mheshimiwa Waziri, lakini hakuiwekea mikakati wala mipango kwa ajili ya kutatua tatizo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango hii mizuri yote ambayo mmeiweka bila kutatua tatizo la wakulima na wafugaji, yote ni sifuri kwa sababu tuna tatizo kubwa sana huko vijijini na waliosabisha tatizo hili la wakulima na wafugaji ni Wizara ambao wanahusika kwa namna moja au nyingine. Wanatoa hatimiliki, wanauza mashamba bila kuzingatia hali halisi ya field ikoje. Unakuta wananchi kwenye sehemu husika wameishi miaka 12, 15, zaidi ya 20 lakini anakuja mtu anapewa hatimiliki, ndiye mmiliki halali. Mifano iko mingi, hasa nichukulie Jimbo langu, labda ndipo unaweza kunielewa Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shamba la Kidago ambalo zamani lilikuwa la Uluguru Tailors. Ni shamba ambalo wakulima pale wamekaa zaidi ya miaka 40. Leo hii kapewa mwekezaji na kesi iko mahakamani. Sitaki kulizungumza sana kwa sababu lipo, lakini nakuomba Mheshimiwa Waziri uje ili uone hali halisi ilivyo pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano wa pili, kuna shamba la Pangawe, ambapo pale kuna mradi wa mfano, walikuwa wa KOICA (Corea) ndiyo wamewekeza. Leo hii tuna tatizo kubwa sana na mwekezaji. Nakuomba Mheshimiwa Waziri uje katika jimbo langu la Morogoro Kusini Mashariki ili tuweze kukaa na mwekezaji huyu tuone ni namna gani tunaweza kumaliza tatizo hili; kwa sababu nia nzuri mliyokuwanayo, bila kumaliza migogoro ya wakulima na wafugaji tatizo hili litakuwa kubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwingine uko kule mpaka Kata za Maturi, Kidugaro, kwenye vijiji vya Ng‟ese huko matatizo ni hayo hayo. Kwa hiyo, ndiyo maana dhamira yako kuu ya kusema vijana twende huko, tunakwenda huko lakini ardhi hakuna. Nina ushahidi ndiyo maana unaona kuna migogoro ya ardhi kila siku nchini kote. Kwanza uje na mkakati, nafikiri baada ya kuja kutoa majumuisho yako, uje utuambie, Serikali na Wizara yako imejipanga vipi katika kutatua tatizo la migogoro ya wakulima na wafugaji ili tuwe salama tuweze kuongeza uzalishaji katika nchi hii? Leo hii wakulima wa nchi hii hususan wa Morogoro Kusini Mashariki, zamani tulikuwa tunalinda nguruwe na kima, sasa hivi tunalinda ng‟ombe ili wasile mavuno. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili. Sisi Morogoro Vijijini ni wakulima wazuri wa matunda, lakini sijaona katika kitabu chako mpango mkakati kwa ajili ya viwanda vya kusindika matunda, kwa ajili ya kutengeneza soko la uhakika kwa matunda yanayooza katika sehemu kubwa ya nchi yetu hususan Morogoro Vijijini. Sisi ni wakulima wazuri wa ndizi, machungwa, machenza na maembe katika vijiji vya Tegetero, Kinole, Kiloka na sehemu nyingine zote, lakini leo hii matunda yanaoza mtini wakati mwingine kwa kukosa soko la uhakika, hasa viwanda vya kusindika mazao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, niende kwenye Jimbo langu tena kuhusu Shamba la LMU lililoko Ngerengere. Lile shamba ni la kuzalisha mifugo ya kisasa. Shamba lile lina ukubwa zaidi ya heka 11,000 lakini utaishangaa Serikali kuna ng‟ombe 900 tu, mbuzi 200, nguruwe 50 na eneo lote limebaki ni pori. Hapa ninashauri mambo mawili, kwanza, naiomba Serikali kuwekeza nguvu kubwa katika uendelezaji wa shamba hili ili lengo lililokusudiwa litimie liweze kutufaidisha watu wa Morogoro Kusini Mashariki hususan Tarafa ya Ngerengere.
La pili, ushauri wangu na ombi kwa Serikali, Ngerengere sasa hivi imekuwa Mji Mdogo, imekua na bahati mbaya hatuna eneo lolote la upanuzi kwa sababu tumezungukwa na vikosi vinne vya Jeshi. Tunamba ombi maalum Serikalini, angalau tupatiwe heka 1,500 katika shamba hili ili tuweze kuliendeleza na shamba hili pia vigawiwe vitalu kwa ajili ya wafugaji na wakulima ili kuendeleza maendeleo ya watu wa Morogoro Kusini Mashariki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nichangie katika Bodi ya Korosho na bodi nyingine za mazao nchini. Miongoni mwa majipu yaliyopo katika nchi hii, hizo bodi za mazao ndiyo matatizo makubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe mfano mmoja tu katika Bodi ya Korosho, hapa wadau wa korosho wamezungumza mengi kuhusu makato yanayotokea huko. Miongoni mwa kazi nyingi za Bodi ya Korosho ni pamoja na kuhamasisha uzalishaji, lakini pia usindikaji (processing), lakini pia kutafuta masoko. Haya yote matatu Bodi ya Korosho inakwenda kwa kusuasua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano mmoja, mwaka 1973 uzalishaji wa Korosho tulifikia tani 145,000 wakati wa Mwalimu Nyerere, leo hii baada ya miaka zaidi ya 30 tunazungumza uzalishaji tani 154,000. Kwa ushahidi hata nchi zilizokuja kuomba mbegu hapa, kama Vietnam leo zimeshatupita, lakini bodi hii kila mwaka wanakupa projection, wanakwambia tunazalisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia kuhusu kodi nyingi zilizokuwepo kwenye Bodi hii ya Korosho. Mkulima analipa zaidi ya shilingi 640 kwakilo moja ya korosho, ambapo tukichukua tu hesabu hii iliyokuwa ni projection ya mwaka wa 2015 ambayo ni tani 154,000, zaidi ya shilingi bilioni 99 wakulima wa korosho wanaiacha. Hiyo fedha bei ya korosho ingeachwa kwa mkulima ingekuwa kubwa zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mkulima wa Korosho anakatwa shilingi 207 huko kijijini, kwa maana ya five percent tunazungumza shilingi 60 kwenye ushuru wa Hamashauri, shilingi 50 ni Chama cha Ushirika, shilingi 10 ni kwa ajili ya mtunza ghala, shilingi 20 Cooperative Union, shilingi moja kwa ajili ya kikosi kazi. Makato hayo jumla yake inafika 207. Achana na hayo, anaambiwa kuna export levy.
Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi wa kuwa na export levy ni kwa ajili ya ku-encourage investment katika nchi yetu. Kwa miaka yote ambayo tumekuwepo hapa, Bodi ya Korosho inasema inafanya investment ya ubanguaji wa Korosho nchini. Inachukua 15 percent ya FOB price ambapo kwa mwaka wa 2015 kwa sababu FOB price ilikuwa ndogo, wakachukua bei elekezi ya shilingi 2,900 ni sawasawa na kukata shilingi 435 sawasawa na shilingi bilioni 69. Hakuna kiwanda chochote kilichowekezwa, kitu ambacho… (Makofi)
MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga hoja.