Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii muhimu ya kuchangia hoja muhimu iliyo mbele yetu. Naomba nianze kwa kusema kwamba naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kutoa pongezi kwa Serikali yetu na kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi nzuri ambayo inaendelea kufanyika na inafanyika kwa speed ambayo ni kubwa na walio wengi hawakutarajia kama tunaweza kufanya mambo haya kwa speed tunayoenda nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka tulipoweka mtaalam mshauri ili ashauri nchi za Afrika Mashariki ni kwa namna gani tuendeleze mfumo wetu wa reli, yule mtaalam alitushauri nchi za Afrika Mashariki akasema hizi reli zenu mlizonazo ni vizuri muendelee nazo kwa sababu nyie ni nchi maskini, nyie hamhitaji zinazoenda kwa kasi na hamna fedha za kufanya hayo mambo makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka tuliokuwepo wakati ule pale Arusha tulikataa na tukamwambia huyo mtaalam mshauri kwamba ni kweli uchumi wetu haujakaa vizuri nchi za Afrika Mashariki, labda hatuhitaji treni zinazokimbia sana kama unavyosema labda bado sisi ni nchi maskini, lakini hatuwezi kukaa hivyo milele, tunabadilika kila siku. Kwa hiyo, tukakubaliana kwamba tutajenga sasa standard gauge kwa nchi zote za Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kuipongeza Serikali yetu kwamba tumeonesha njia, nchi zote za Afrika Mashariki tulikubaliana kwamba sasa tujenge standard gauge lakini Tanzania tumeanza sio tu tunajenga standard gauge lakini pia tunajenga standard gauge ambayo tutatumia nishati ya umeme. Hilo ni jambo kubwa nawapongeza sana wanaohusika na tuendelee kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongelea mambo machache, la kwanza, kuna malalamiko ya wananchi Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, jukumu mojawapo ni kushughulikia malalamiko ya wananchi na kuyapatia ufumbuzi. Malalamiko yao mengi lakini kwa leo nitazungumzia malalamiko ya wananchi wa Kata ya Kakunyu ambayo yamechukua zaidi ya miaka 18 bila kupatiwa ufumbuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mgogoro mkubwa na umechukua muda mrefu, mgogoro wa Ranchi ya Misenyi pamoja na vijiji vinavyozunguka Ranchi ya Misenyi. Mgogoro huo umechukua muda mrefu, nimwombe Mheshimiwa Waziri Mkuu sasa wakati umefika tuweze kupata ufumbuzi na ukiangalia kwa umakini. Mgogoro huo umechangiwa na mambo matatu ambayo tukiamua tunaweza tukayapatia ufumbuzi kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza lililochangia sana mgogoro huo ni kwamba, tulipoamua mwaka 2002 kwamba Ranch ya Misenyi na Ranch nyingine ambazo kuna maeneo makubwa yasiyotumiwa vizuri yawekwe kwenye blocks ndogo ndogo na wagawiwe wafugaji wadogo wadogo, lakini utekelezaji ulivyoanza haikufanyika hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukiangalia uamuzi uliofanyika ni mzuri, lakini utekelezaji ulipoanza haikufanyika hivyo, hawakugawiwa wafugaji wadogo wadogo badala yake waligawiwa watu wala hawajawahi kuona ng’ombe na wengine wala sio wafugaji na wengine wala hawapo ni marehemu lakini waligawiwa Ranch. Sasa mgogoro ukaanzia hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili kukatokea uamuzi, ulikuwa mzuri tu kwamba ile Ranchi ya Misenyi kwa maeneo ambayo ranchi ilikuwa haiyatumii, basi lazima NARCO iyagawe katika blocks ndogo kama nilivyosema haikufanyika hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu ilikuwa ni kwamba ukiangalia ile ramani ambayo NARCO walikuwa wanaitumia na ambayo bado wanaitumia ingawa hawataki kuionesha, ramani ile wanayoitumia wao unapofika Mto Kagera unapovuka tu ramani wanayoitumia NARCO inaonesha kuanzia Mto Kagera mpaka kwenye mpaka wa Uganda hakuna mtu anayeishi na hakuna kijiji wala kata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wanapokaa kwenye meza yao wanagawa wanavyotaka, jambo ambalo sio sahihi. Maana unapovuka Mto Kagera unakutana na Makao Makuu ya Wilaya, unakutana na Kata nyingi tu na vijiji vingi tu lakini ramani wanayoitumia kugawa blocks zinazotuletea matatizo, yenyewe inaonesha unapokatiza tu Mto Kagera hakuna vijiji, kata wala mtu. Sasa kwa utaratibu huo lazima migogoro ya namna hii iendelee kuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ufumbuzi, leo hii nimeona nishauri ufumbuzi. Nitashauri mambo manne; jambo la kwanza, ni kwamba mipaka ya Ranchi ya Misenyi na Vijiji vinavyozunguka ranchi hiyo ni Mto Kiboroga na Mto Kyaka Kuru, hii ndio mipaka inayoeleweka kwa mtu yeyote yule. Kwa hiyo, ufumbuzi wowote ule ambao hautabainisha kwamba mipaka ya ranchi ni Mto Kiboroga na Mto Kyaka Kuru unakuwa hujatoa ufumbuzi wowote. Kwa hiyo, huo ni ufumbuzi wa kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ufumbuzi wa pili, iwekwe barabara ya ulinzi na kukagua mipaka kuanzia Mutukula hadi Kakunyu maana ukiwa na mpaka ambao huwezi kuukagua ni kazi bure. Ukiangalia upande wa Uganda wao wana barabara nzuri tu ya kukagua mpaka wao, unapokwenda upande wa Tanzania hakuna barabara. Kwa hiyo, barabara hii ni barabara ambayo lazima tuipe kipaumbele, tuitengeneze kwa haraka na itatusaidia kufanya mambo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kengele ya kwanza imelia, sababu nyingine sitaendelea nazo nimalizie na mambo mengine matatu ambayo nataka kuyaongelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ni muhimu, tulikaa Wabunge wa Kagera na Mkuu wa Mkoa wa Kagera, tumekubaliana katika kikao mambo ya msingi ambayo yakitekelezwa yatamaliza migogoro ya ardhi Karagwe, Muleba na Misenyi. Nimwombe Mheshimiwa Waziri Mkuu amuelekeze huyo Mkuu wa Mkoa amletee makubaliano tuliyokubaliana ili aweze kutusaidia kumaliza mgogoro huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile iliundwa Kamati nzuri na Mheshimiwa Waziri Mkuu na akatoa hadidu za rejea nzuri tu. Mheshimiwa Waziri Mkuu aliahidi kwamba atatuletea taarifa ya Kamati hyo, lakini hiyo taarifa siioni na wala haiji Nimwombe Mheshimiwa Waziri Mkuu taarifa hiyo ije ili tuweze kumaliza mgogoro huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Profesa alichangia kuhusu zao la kahawa, nami nizungumze kidogo tu. Zao la kahawa, kuna maamuzi ambayo yamefanyika, ni utaratibu mpya, mzuri tu. Niseme mambo mawili kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, uuzaji wa kahawa ni biashara na mtaalam wa uchumi Adam Smith alishasema, uchumi huendeshwa na mkono usioonekana (invisible hand). Uchumi hauendeshwi na mtutu wa bunduki, wala mizinga. Kwa sababu hiyo, ufunguzi wowote tunaouweka kuendesha uchumi, uuzaji wa kahawa, lazima tulijue hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ambalo napenda kulitoa hapa kwa haraka ni kwamba kama huna muda wa kusoma vitabu, maana duniani vitabu viko vingi. Chagua vichache vya kusoma. Kuna kitabu kimoja kinasema, Why Nations Fail? Moja ya sababu kitabu hicho kinasema Nations fail, yaani Mataifa mengi hushindwa kuendelea kwa sababu ya kutojenga mifumo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unaposema unabadilisha mfumo wa kununua kahawa, hujajenga mifumo ya kununua kahawa, ujue utapata matatizo. Kwa sababu unaposema Vyama vya Ushirika kuanzia sasa vinunue na vinunue vyenyewe tu, aah, shughuli ipo. Kwanza ni lazima ujenge hivyo Vyama vya Ushirika viwe tayari kununua hiyo kahawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata taarifa kwamba wametangaza bei, wakasema watanunua kwa Sh.1,000/= na Profesa amesema hapa, lakini sio wakulima wa kahawa ninaowajua. Hao ninaowajua, hamtakaa mwone kahawa yao. Najua tutajidanganya kwamba tuna wanajeshi, tuna nini, watashughulika, watapambana, hiyo ni kupoteza muda bure, kwa sababu wakulima na wao wanajua soko liko wapi. Mkulima siku zote atapeleka kahawa yake kule ambako anajua atapata soko la uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.