Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. MUSSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia katika hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza kabisa nianze kwa pongezi kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anayoifanya. Amefika Jimboni kwangu Igalula, ametatua kero za tumbaku katika Jimbo langu la Igalula sasa wakulima wa tumbaku wanaanza kupata kile ambacho wanategemea kutokana na zao lao la tumbaku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri, MheshimiwaJenista na Naibu Waziri mdogo wangu Mheshimiwa Anthony Mavunde na Dada yangu Stella Alex Ikupa kwa kazi kubwa wanayomsaidia Mheshimiwa Waziri Mkuu, mambo yanakwenda vema na sisi tunaona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu wakati alivyokuja Jimboni kwangu hakuondoka hivi hivi, aliniachia mchango katika kituo changu cha afya na sasa tunakwenda vizuri. Namshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe shukrani zangu kwa Serikali hasa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Alivyokuja Jimboni kwangu Igalula nilimweleza matatizo ya miundombinu katika Jimbo letu la Igalula, barabara yangu ya Chaya – Nyahua na aliniahidi baada ya mwezi mmoja Mkandarasi atakuwa site na hivi ninavyozungumza Mkandarasi yupo site na barabara imeanza kutengenezwa. Nashukuru sana kwa kazi nzuri anayofanya Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Igalula unapozungumzia reli ya kati, ujenzi unaofanyika sasa wa standard gauge unatugusa sisi kwa asilimia 100. Wananchi wetu kusafiri wanategemea sana reli katika Mkoa wa Tabora na kusafirisha mazao yetu kutoka Tabora kwenda sokoni kunategemea sana usafiri wa reli. Kwa hiyo, ujenzi wa standard gauge kwa sisi wananchi wa Tabora tunapongeza kwa kazi kubwa inayofanywa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tunamwomba aendelee kuwa na afya njema ili ujenzi huu uweze kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kidogo suala la Watendaji wa Vijiji na Kata. Nashukuru baadhi ya Wabunge wamelizungumzia, kuna waraka umetoka Watendaji wetu wa Vijiji na Kata ambao wana elimu ya darasa la saba ambao wengi wao wameajiriwa takribani miaka 20 iliyopita leo wanatakiwa waondoke kwenye ajira, wanapoteza mafao yao na kazi zao. Baadhi yao wana takribani miaka miwili wanaelekea kwenye kustaafu, mtu aliyefanya kazi kwa miaka 20, leo anaambiwa anaondoka kwenye kazi hana mafao na hajui ataenda kuishi vipi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watendaji hawa ndio tuliwatumia kujenga shule zetu za msingi, tuliwatumia kujenga shule za sekondari, kujenga nyumba za Walimu, tumewatumia kusimamia ulinzi na usalama katika maeneo yao, wamefanya mambo mengi kwa miaka 20, leo malipo yake ni haya! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali yangu na namuomba Mheshimiwa Waziri Mkuu waliangalie hili kwa macho mawili ili tuwasaidie watendaji hawa ambao wengi wao baada ya miaka miwili mitatu wanaondoka kwenye utumishi, tusubiri waweze kumaliza muda wao tuanze upya utaratibu wa kuajiri watu wengine baada ya hawa kuondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la afya. Ilani yetu inazungumzia kila Kijiji kiwe na zahanati lakini kila Kata iwe na kituo cha afya. Haya yote tunataka kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanapata huduma bora na salama za afya. Tunataka kuhakikisha kwamba mama na mtoto wanajifungua salama, wanapata huduma zilizo bora zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Igalula hatuna kituo hata kimoja cha afya katika Jimbo zima. Tunazo zahanati lakini referral ya kutoka kwenye zahanati ni hospitali yetu ya Kitete iliyopo Tabora Mjini takribani kilomta 100 toka Jimboni Igalula. Mama mjamzito anapopata tatizo la kujifungua kutoka Igalula kwenda kwenye Hospitali ya Serikali ya Kitete takribani kilomita 100, asiyekuwa na uwezo wa kusafiri wanapata matatizo, wengine wanapoteza maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuingia madarakani sisi tuliliona tatizo hili, tumeanza kujenga vituo vya afya katika kila Kata, lakini Kata zetu tano za Jimbo la Igalula tumeshafika katika eneo la lenta tunasubiri sasa Serikali iweze kutusaidia. Tunaomba waliopata milioni 500 na sisi tuangaliwe tuweze kusaidiwa kupata fedha hizo kujenga vituo vya afya katika Jimbo la Igalula ili kuondokana na tatizo la vifo vya mama na mtoto kama Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi inavyosema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la maji na umwagiliaji ambalo katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ipo katika ukurasa wa 27 ikiambatana na upatikanaji wa chakula kwa wananchi wetu. Nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Maji na Naibu Waziri kwa kazi kubwa wanayoifanya kuondoa kero ya maji katika maeneo yetu. Wamefanya haya kwa bajeti tuliyowapitishia mwaka jana ya Sh.50 tuliyoiongeza katika lita moja ya mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nnaomba kama waliweza kufanya mambo makubwa haya kwa Sh.50 tulizoziweka kwenye bajeti iliyopita, kama kuna uwezekano tuwaongezee Sh.50 tena katika lita ya mafuta iwe Sh. 100 iingie katika Mfuko wa Maji, nina hakika kero kubwa ya maji katika maeneo yetu itakwisha. Niombe Waheshimiwa Wabunge tusimamie hili sisi tunaotoka vijijini tunaiona kero kubwa ya maji. Tulisema tutamtua mama ndoo kichwani, tutekeleze kwa vitendo kwa kumwongezea bajeti ili aweze kutekeleza. Tusipoweka bajeti ya kutosha haya yote hayawezi kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la upatikanaji wa chakula linaendana na kuboresha miradi ya umwagiliaji katika maeneo yetu. Tukitengeneza miradi mizuri ya umwagiliaji suala la upatikanaji wa chakula katika maeneo mengi halitakuwa tatizo. Tunapowaambia wananchi wasiseme kama kuna njaa wakati hatutengenezi mazingira bora ya umwagiliaji tunakuwa hatutendi haki, lakini yapo maeneo mengi ambayo miradi hii ipo inaweza ikafanyika na ikasaidia upatikanaji wa chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu kuna miradi miwili mikubwa, Goweko kuna mradi wa umwagiliaji umeshatengenezewa feasibility study, umeshafanyiwa usanifu na imeshapatikana hati ya mazingira. Katika Kata ya Loya tumeshapata hati ya mazingira na usanifu umefanyika. Katika bajeti ya mwaka 2016/2017, iliwekwa miradi hii iweze kutekelezeka, lakini mpaka leo haijaweza kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri Mkuu ili wananchi wetu wasiwe na shida ya chakula, miradi hii iweze kuangaliwa kwa makini iweze kutengewa fedha, ikiweza kutekelezeka hatutakuwa na shida ya chakula. Wananchi wetu watapata fedha za kuchangia miradi ya maendeleo, Halmashauri zetu zitapata kodi na mwisho wa siku hata uchumi wa viwanda tutakwenda nao vizuri huko tunapokwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la barabara. Nilipoanza kushukuru barabara yangu ya Chaya – Nyahua nilizungumzia umuhimu wa barabara hii. Barabara hii inaunganisha Mikoa ya Katavi, Mkoa wa Kigoma lakini pia ni njia rahisi kufika Bukoba, Kahama na Mwanza. Inapotengenezwa barabara hii maana yake tunawasaidia hata ndugu zetu wa mikoa ya jirani kuunganisha safari zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika barabara hii kuna kipande ambacho naomba kifanyiwe kazi, kifanyiwe upembuzi kuanzia pale Chaya kuja Lutende kutokea Ndala kwenda kutokea Puge na Nzega. Barabara hii kama itatengenezwa itapunguza tena siyo chini ya kilometa 120 kutoka Dodoma – Tabora – Mwanza na maeneo mengine badala ya kupitia Singida na Nzega. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niliomba barabara yangu ya Miswaki – Loya – Iyumbu kilometa 75 iweze kutengenezwa. Kwa nini niliomba barabara hii iweze kutengenezwa? Kuna kilimo kikubwa cha mpunga tunalima mpunga mwingi sana kule, barabara hazipitiki wakati wa mvua. Kupitia TARURA tuliomba fedha ili iweze kufunguliwa barabara hii. Kuna uchumi mkubwa wa Wilaya yetu ya Uyui, Halmashauri inakusanya zaidi ya milioni 200 kutokana na kodi kwa sababu ya mpunga unaolimwa kule. Barabara hii ikitengenezwa itasaidia wananchi wetu kuweza kujikwamua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la elimu. Nipongeze elimu bila ada. Wananchi wetu wanapata fursa kubwa ya kupata elimu, wale ambao walikuwa hawapati elimu lakini changamoto zilizojitokeza, kwanza vyumba vya madarasa vimepungua, nyumba za Walimu zimepungua, Walimu wamekuwa wachache na matundu ya vyoo pia yamekuwa machache. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachosahuri ni kwamba Serikali sasa ije na mkakati maalum kama ilivyofanya kwenye madawati, tuwe na mkakati wa kuhakikisha kwamba tunajenga sasa nyumba za Walimu za kutosha, tuongeze Walimu, tujenge matundu ya vyoo lakini pia tuweze kupata nyumba za Walimu na madarasa pia yaongezeke ili kutatua changamoto hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani yake hapo wananchi wetu wamejenga majengo haya mengi ambayo maboma hayajakwisha kwa ahadi kwamba wakifikisha kwenye lenta Serikali itakuja kuwasaidia. Katika maeneo mengi majengo haya yapo, siyo katika Jimbo la Igalula tu, ni nchi nzima. Serikali sasa lazima ije na utaratibu wa kuhakikisha kwamba na haya maboma yote yanaisha ili nguvu za wananchi zisipotee bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie ofisi za Wabunge. Suala hili naomba lichukuliwe katika uzito mkubwa sana. Waheshimiwa Wabunge kuendelea kupewa ofisi kwenye ofisi za ma-DC siyo sawasawa. Waheshimiwa Wabunge kwenda kukodisha ofisi mitaani siyo sawasawa. Ninachoomba Bunge lije na mkakati maalum kusaidia upatikanaji wa ofisi za Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na ahsate sana.