Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Makubaliano ya Paris chini ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi

Hon. Yussuf Salim Hussein

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Chambani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Makubaliano ya Paris chini ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nichangie katika azimio hili lililopo mbele yetu.

Kwanza nisikitike tu kwamba Azimio lenyewe ni kubwa sana na kwa lilivyopangwa na litakavyojadiliwa sioni kama tumelipa thamani hiyo au uzito huo ambao inalo. Ni kitu kikubwa sana na ndiyo kinagusa maisha yetu sasa kujadiliwa hapa kwa siku moja sidhani kama tunalipa uzito huo, naomba tulipe uzito sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Azimio hili nasema linagusa maisha yetu kwa sababu gani? Wamezungumza hapa katika paragraph ya nne kwamba kuna kupotea, sasa nitazungumza hii habari ya kupotea kwa visiwa na maeneo ya namna hiyo, sea erosion.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuna upoteaji mkubwa sana, lakini siyo kwamba vile visiwa vinaisha tu au ardhi inamegwa na bahari kwa sababu ya nguvu ya maji, hatuishii hapo tu lakini kuna na viumbe vinapotea ambavyo vimo katika vile visiwa au katika bahari na vikiendelea kupotea viumbe na mimea ndiyo na sisi maisha yetu yanapotea vilevile.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitatoa mifano michache tu, kuna miti ambayo inapotea kwa kasi kubwa sana, xylocarpus moluccensis na xylocarpus granatum hii ni mitonga, mtonga mweusi na mtonga mwekundu inapotea sasa ikipotea hiyo ina maana kizazi chetu watakuja kuona au watakuja kusikia ni historia.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna heritiera littoralis (msikundasi) nayo inapotea. Kizazi chetu kinachokuja hii miti hawataikuta, watakapokuja hawakuti hii miti ni hisotoria itakuwa nini? Itakuwa tumewajengea faida gani? Lakini siyo hivyo tu ni mazalia ya viumbe vingine hii kama kaa, chanje kama hii miti haipo katika bahari ina maana na hivyo viumbe vingine navyo vinapotea.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika visiwa vilevile kuna ndege ambao ni endemic, ni ndege muhimu hapa duniani wanapotea vilevile. Kwa mfano white eyes (chigi manjano) sisi kule Zanzibar tunaita tayari wamepotea hawapo, sawa. Kuna ndege hawa Javaspirous tayari wanapotea hawapo na yote ni kwa sababu ya kwamba mabadiliko haya ya tabianchi yanapotea. Kwahiyo kupotea na kuondoka kwa visiwa siyo kwasababu tu kwmaba tuna ardhi inaondoka, lakini tunapoteza na hizo mnaita wenyewe sasa bioanuai sijui na nini, vitu vyote vinapotea tutakuwa hatuna na kizazi chetu kitakujakurithi nchi ambayo mimea na ndege hawapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee mbele kuna tatizo linasema kwamba mvua hizi tunapata tunaita mabadiliko ya tabianchi, lakini hatuwezi kuwa na mabadiliko ya tabianchi mazuri tunayoyategemea kama sisi wenyewe hatujabadilika. Mwenyezi Mungu ametuleta duniani kuitawala dunia na vilivyomo ndani yake, je, sisi wenyewe tunalijua hili? Tumebadilika? Kama hatujabadilika na tunachokitawala katika dunia hii kitaendelea kuharibika, hakitakuwa katika namna tunayoitaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania tulikuwa tunapata mvua nne kwa mwaka, leo tunapata mvua mbili kwa taabu na zikija hizo mvua basi ni laana maana yake ni mafuriko, uharibifu. Likitoka jua ni hivyo hivyo, kwanini? kwamba sisi wenyewe hatujabadilika kwa hiyo na sisi wenyewe lazima tubadilike. Oman ilikuwa jangwa, walikuwa miaka miwili hawaoni mvua, mvua ikinyesha ni ajabu leo wanapata mvua nne, kwanini? Wao wenyewe wamebadilika. Kwa hiyo na sisi lazima tubadilike na tuelewe kwamba tumeletwa ulimwenguni kwamba tuvitawalie hivi, Je tumebadilika nafsi zetu? Tunalijua hilo? Kwa hiyo na sisi wenyewe lazima tubadilike na ndiyo maana sasa mvua hizi zinaleta mafuriko, zinaleta athari kubwa, kilimo kinaharibika, matokeo yake sasa ni hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini siyo hapo tu wadudu hawa kuna wadudu sasa hivi matunda haya yote kuna vidudu dudu hivi mapapai yanaharibika, maembe, ndizi, wale wadudu weupe sijui mnawaitaje sijui sigatoka, sijui wenyewe wataalam mnawaitaje. Wataalam wa kilimo kwa miaka nenda miaka rudi hakuna mabadiliko yoyote. Yote haya yanasababishwa na kubadilika kwa haya mabadiliko ya tabianchi ambayo tunayasababisha sisi wenyewe.

Waheshimiwa Wabunge, tunasema kwamba theluji inayeyuka katika Mlima Kilimanjaro, wenyewe Wachaga wa Kilimanjaro wanaita Kibo. Sasa kwa maana ile Kibo ikipotea maana yake na Mlima Kilimanjaro unapoteza thamani yake tutakuwa tunajivunia nini kama Watanzania? Kwa hiyo, vyote hivi ni vitu ambavyo tunatakiwa tuviangalie sana. Lakini jangwa linaongezeka kwasababu sisi wenyewe ambao tumeambiwa tuitawale dunia ndiyo wakataji wakubwa wa miti, ndiyo wachomaji mkaa, ndiyo wachomaji wa moto kwenye misitu, kwa hiyo, ni sisi wenyewe na ndiyo maana nikasema tunalichukulia uzito kiasi gani? Sisi kama wananchi, kama binadamu ambao tmeletwa tuvitawale hivi tunalichukulia hili suala la mabadiliko ya tabianchi kwa thamani kiasi gani, kwa nguvu kiasi gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni nini athari yake? Wanaoathirika sana ni wakulima na wavuvi. Tabianchi ikibadilika, wakulima hawa watalima hawavuni kwa sababu hizo nilizozitaja ama kwa mafuriko ama za jua ama za wadudu waharibifu hawatavuna na matokeo yake sasa tutakuwa tunawasema watalaam wa kilimo, sijui madawa, sijui hatuna watu ugani lakini ni tabianchi tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tabia hizi zikibadilika, mazingira yakibadilika, hali ya hewa ikibadilika na maradhi yatakuja. Zanzibar nime-check mara hii pale mwezi Januari na Februari ongezeko la wagonjwa wa pressure hospitali pale ni kubwa sana, kwa sababu gani? Ya joto tu limeongezeka. Kwa hiyo, hizo ni athari za moja kwa moja tunaziona lakini wavuvi pia samaki watakosekana, wakikosekana samaki inamaana hao nao wanaathirika. Kwa hiyo, ikifa hii ecosystem yote ina maana na kizaizi chetu kinachokuja hakitaona mimea na ndege na wanyama ambao walikuwepo wa asili hapa kwa hiyo, lazima tuwe serious na hili ili tuone kwamba kizazi chetu kinakuja kufaidika kwa kiasi gani, nini tufanye?

Mheshimiwa Naibu Spika, waathirika wa masuala haya duniani asilimia 20 ni wale watu maskini kabisa na ndiyo hao wanaoathirika kwa sababu wao ndiyo wanaoishi huko kwenye miti, kwenye misitu na huko vijijini kwa hiyo, hao ndiyo watakaoathirika. Sasa hili suala linalozungumzwa la global warming basi ionekane sasa kwamba inafanyakazi vizuri na iwafikie wale walengwa. Nitatoa mfano, kwa mfano, kuna hizi kaya maskini ambazo zinasaidiwa sijui shilingi 20,000 kwa mwezi hivyo inamsaidia nini mtu wa kaya maskini? Yeye ni masikini unampa shilingi 20,000 kwa mwezi inamsaidia nini? Pesa ambayo hata mtoto wangu na mtoto wako Mheshimiwa Naibu Spika haimtoshi kwa mwezi kwenda shule tu.

Sasa unamsaidia mtu wa Kaya maskini sasa nadhani hizi pesa Mheshimiwa Waziri hebu zipangiwe sasa utaratibu ili kama tuna tatizo sehemu fulani twende tuka-solve hilo tatizo na hizi pesa tusiwe tunazigawanya kisiasa siasa tu, kupendezeshana pendezeshana tu hali ni mbaya ni lazima tuwe commited katika kuyatafutia suluhisho masuala haya vinginevyo itakuwa tunapoteza muda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nadhani natoa mfano tu hapa wa TASAF kwamba hizi shilingi 20,000 hizi hazisaidii kuondoa yale matatizo na badala yake zinaleta mizozo tu zaidi, mnawapa mnaowajua, mnawapa watu mnachangua na nini kwa hiyo, hebu hii pesa ndogo ambayo
tutaipata katika kufanya haya basi tuipeleke katika eneo ambalo lina tatizo tuondoe tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna masuala haya ya social protection (kinga za kijamii) je, tuna alternative gani? Maana yake tusiwe tunasema tu wkamba kuna hili, Je, alternative yetu ni ipi? Juzi nilikuwa namuangalia Dkt. Kilahama amepunguza yaani wamefanya utafiti, wamepata miti kutoka miaka 14 kuvuna mkaratusi sasa ni miaka nane unavuna katika ubora. Kwa hiyo, solution ziwe hizi na tuzieleze sasa kwa jamii moja kwa moja kwamba solution ni hii. Kwa hiyo, tufanye vitu vya namna hii na tuwatumie wasomi na watalaam wetu katika tafiti zao tufanye katika kukabiliana na hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, lazima tujitathmini kama Watanzania. Kama haya tunayaona leo na haya dunia inayasema leo tunachukua hatua gani? Tuna gesi lakini bado asilimia 80 ya Watanzania wanatumia mkaa na kuni kama nishati. Kwa hiyo, tuendeleze elimu na tuwasaidie, tuboreshe kurahisisha matumizi ya gesi ili tupunguze sasa hizi athari zinazotkana vinginevyo itakuja kuwa kama hadithi ya biashara ya utumwa. Wazungu ndiyo walioanzisha biashara ya utumwa, wakafaidika, walipopata teknolojia wakawatupia watu wengine wao wakasema ni biashara haramu. Kwa hiyo, na sisi tusipoliangalia hili tutakujakuishia katika historia za namna hiyo.

Kwa hiyo, naomba katika matumizi sasa gesi tunayo tuhamasishe sana ili tuepuke ukataji wa miti na utumiaji wa mkaa na kuni kama nishati na badala yake tuweze kuyatunza mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii.