Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa ambayo ameendelea kuifanya ndani ya Taifa letu hasa katika sekta ya madini, ameanza kuonyesha mfano. Kwa kipindi kirefu sana kumekuwepo na malalamiko mengi kwa wananchi na watu mbalimbali na NGOs kuhusiana na suala la madini. Kwa kweli Mheshimiwa Rais amefanya kitu kikubwa cha ujasiri kuweza kuchukua hatua thabiti na kuweza kuona namna ya kukwamua mambo ya rasilimali katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi ambao tunatoka maeneo ya madini tunaona jinsi ambavyo tunaachiwa mashimo. Ukienda kwa mfano GGM watu wanachimba madini kwa kiwango kikubwa lakini wananchi waliopo jirani na maeneo hayo hatuoni faida zaidi katika madini hayo. Kwa hiyo, kwa hatua ambazo Mheshimiwa Rais amechukua mimi binafsi pamoja na wananchi tunampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mwimbaji mmoja alisema kwamba niseme nini Bwana. Kwa kweli hata mimi nasimama hapa leo kuimba kusema niseme nini Bwana kwa kazi kubwa ambayo Mheshimiwa Rais ameifanya katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niendelee sasa kuomba kwamba mikataba iendelee kuletwa hapa Bungeni ili tuweze kuipitia kuona namna ya kuwezesha zaidi rasilimali za Taifa hili ili tuweze kufaidika sisi wananchi wa Taifa la Tanzania. Sambamba na mikataba lakini pia ziangaliwe sheria ambazo zipo pamoja na sera, kama hazitupeleki mahali ambapo tunastahili, tuweze kuzifanyia kazi na kuzirekebisha ili wananchi tuendelee kufaidika zaidi na rasilimali ambazo Mungu ametupatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kutoa msisitizo pia kwenye usimamizi wa maliasili zetu. Mheshimiwa Rais ametuonesha mfano na viongozi wengine tuendelee kuonyesha mfano, tuwe wazalendo kwa Taifa letu. Kwa hiyo, niombe tu kwa ujumla sisi sote kwa pamoja wananchi na Wabunge tusimame imara tukiendelea kumuunga mkono Mheshimiwa Rais lakini pia hata sisi wenyewe tuweze kusimamia kwa dhati rasilimali za Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa uwasilishaji mzuri wa bajeti ya mwaka huu 2017/2018. Kama ambavyo wenzangu wametangulia kusema ni bajeti ya mfano. Ni bajeti ambayo kwa kweli ukiisoma inafurahisha na wananchi wengi tumeifurahia bajeti hii. Mimi nasimama kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Busanda kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa bajeti nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu gani? Wananchi walio wengi hasa vijijini walikuwa wanateseka sana na vikodi vidogo vidogo lakini bajeti hii imeweza kuondoa hizi kero. Mwananchi alikuwa anaenda kuuza gunia lake la mahindi analipa kodi, lakini kwa jinsi ambavyo bajeti hii imeweza kuondoa kodi ndogo ndogo, kwa kweli nichukue nafasi hii kwa niaba ya wananchi kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Wizara kwa ujumla kwa mambo makubwa ambayo ameyafanya kwa wananchi wetu na kwa Taifa zima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika bajeti tunaona jinsi ambavyo imejikita katika kuangalia miundombinu muhimu kwa ajili ya kujenga uchumi kuelekea kwenye viwanda. Tanzania ya viwanda inahitajika tuwe na reli na tayari kwenye bajeti imo, tunaenda kujenga reli ya standard gauge. Kwa hiyo, nipongeze kwa kweli kwa jinsi ambavyo ameangalia mifumo ya kiuchumi ikiwepo reli, maji na umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe tu msisitizo zaidi katika suala la maji. Katika bajeti mmeonyesha jinsi ambavyo mtaangalia vyanzo vya maji kwa mfano kwenye maziwa makubwa kama Ziwa Viktoria, Tanganyika na maziwa mengine. Kwa hiyo, niombe sasa katika utekelezaji wa bajeti tuhakikishe wananchi walio kandokando ya maziwa, kwa mfano, mimi Jimbo langu la Busanda lipo kandokando ya Ziwa Viktoria lakini hatuna maji. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kuomba sasa utekelezaji, wananchi waweze kupewa maji ya kutosha na ya uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iweke utaratibu mzuri wa kuweza kutenga hizi fedha ikiwezekana tuwe na Mfuko Maalum wa Maji, kama jinsi ambavyo REA iko katika suala la umeme, inapeleka umeme vijijini, hata katika suala la maji tuangalie kuwa na Mfuko Maalum kwa ajili ya kusaidia upelekaji wa maji vijijini. Vijijini ndiyo kuna changamoto kubwa sana ya suala la maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia kumtua ndoo mwanamke ni hasa wanawake waliopo vijijini. Kwa hiyo, niiombe Serikali sasa ituwezeshe kuwa na Mfuko Maalum kwa ajili ya maji ili utuwezeshe kutekeleza miradi ya maji katika vijiji vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa umeme, mimi napenda kuishukuru Serikali kwa mipango thabiti na ndiyo maana nasema nitaiunga mkono bajeti hii ya Serikali. Hii ni kwa sababu katika upande wa umeme Serikali imejipanga vizuri kupeleka umeme vijijini na tayari tumeshapata wale wakandarasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoomba sasa umeme huu tunapofikisha kwenye vijiji vyetu, tuhakikishe unafika kwenye taasisi muhimu za umma zikiwepo shule za sekondari, shule za msingi, vituo vya afya na zahanati ili kuwezesha wananchi kupata huduma vizuri kwa sababu kuna huduma muhimu ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika suala la umeme, naomba Serikali iangalie uwezekano miradi hii ianze mara moja, kwa sababu wananchi wamesubiri umeme kwa muda mrefu na wanahitaji umeme ili waweze kuwa na viwanda vidogo vidogo. Vilevile wachimbaji wa madini na wafanyabiashara wanahitaji umeme. Kwa hiyo, naomba sana utekelezaji mara tutakapopitisha hii bajeti uanze mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika bajeti tumezungumzia suala la elimu kwamba tutatoa mikopo kwa watoto wetu kwa masomo ya elimu ya juu. Napenda kuipongeza sana Serikali, tunaomba utekelezaji huo ufanyike ili watoto waweze kupata mikopo na waweze kuendelea na masomo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, ni vizuri kuwa na Vyuo vya VETA. Kwa mfano, kwenye Mkoa wa Geita hatuna Chuo hata kimoja cha VETA. Nitumie fursa hii kuiomba Serikali kupitia Wizara ya Elimu, hebu hakikisheni basi tunakuwa na Chuo cha VETA katika Mkoa wa Geita. Wilaya zote tano hatuna VETA hata sehemu moja na pia katika mkoa hatuna hata VETA moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sasa Serikali iangalie kutoa kipaumbele kwa mikoa na sehemu ambazo hawana kabisa huduma ya VETA. Hapo tutawazesha vijana wetu ambao ni wengi wanamaliza sekondari kupata ujuzi na hatimaye kuweza kuanzisha biashara zao na kujimudu katika maisha yao ya kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la zahanati pamoja na vituo vya afya, ni Sera ya Taifa inasema kwamba kila kijiji kiwe na zahanati na kila kata iwe na kituo cha afya. Ninachoomba sasa Serikali iangalie uwezekano wa kuendelea kutimiza, kweli imetenga fedha, lakini tuhakikishe zinafika kwa wananchi kwa wakati hasa katika Halmashauri zetu ili kazi iweze kufanyika, wananchi tuweze kujenga zahanati kwenye kila kijiji kama ambavyo Sera ya Taifa inasema, lakini vilevile kuwa na kituo cha afya kwenye kila kata na hospitali kwenye kila wilaya. Vilevile kuboresha huduma zote ambazo ni za muhimu ili wananchi wetu waweze kuwa na huduma bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kodi kwa wachimbaji wadogo wa madini. Napenda tu kuomba Wizara ya Fedha hebu tuiangalie hii kodi, haiwezekani hawa wachimbaji wetu wadogo tuanze kuwatoza kodiā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana.