Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imekuwepo hoja ndani ya Bunge na tokea jana na leo Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wanazungumza mambo mengi juu yetu sisi upande wa pili ambao tunaambiwa hatuungi mkono juhudi za Serikali au za Rais za kutetea rasilimali za Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya msingi ni kwamba sisi hatuhusiki kwa namna yoyote ile na mikataba yote ya madini iliyofungwa na Serikali hii. Hatujawahi kuwa kwenye Serikali hiyo na hatujawahi kuingia katika hiyo Serikali na kwa hiyo, hatujawahi kusaini mkataba wowote ule. Kwa hiyo, hiyo mikataba yote iliyofungwa ni ya Chama cha Mapinduzi na Serikali yao. Wasichukue kesi isiyotuhusu wakatutupia sisi. Hiyo ni kesi yao, hilo ni dudu lao, wameliamsha, wamalizane nalo wenyewe. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imekuwepo hoja ya msingi sana kwamba eti tumeibiwa katika rasilimali zetu, kwamba tumeibiwa na watu waliokuja kuwekeza. Mikataba iliyofungwa imefungwa kwa mujibu wa sheria zilizopo. Waliofunga mikataba na ambao bahati njema mmoja wao amezungumza hakamatiki, anasema, mikataba hiyo imefungwa baada ya kikao cha Baraza la Mawaziri kukutana na kuwepo minutes za vikao hivyo. Hatuwezi kusema tumeibiwa wakati tumeruhusu mali yetu wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningewaelewa sana kama tungesema mikataba iliyofungwa ni ya kinyonyaji, mimi hiyo ningewaelewa. Siyo wizi, hapa hakuna wizi! Wizi ni mtu anayeondoka ndani ya nchi yako, anagonga stempu, analipa ushuru, anakulipa hela yako, anaondoka unasema anakuibia! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana kuthibitisha kwamba hakuna wizi, Rais amekaa na aliyemwita mwizi jana Ikulu. Mlango wa Ikulu jana ulifunguliwa ukawa wazi, mwizi akaingia Ikulu, Rais mwenye vyombo vya dola…

TAARIFA . . .

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini huyo ndio mwizi aliyeitwa na Mheshimiwa Rais kwamba kampuni hii haikusajiliwa nchini, inatudhulumu, wamekaa naye Ikulu wakazungumza naye. Nilitegemea Mheshimiwa Rais angeenda kumweka ndani huyu mtu na akamzuia asizungumze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima yako, naomba niliache hilo jambo, lakini message imefika. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mchango wangu kwenye Wizara ya Nishati na Madini nilizungumza juu ya kuwepo mgongano wa maslahi kwa baadhi ya viongozi wetu waandamizi kwenye Serikali. Bahati njema au bahati mbaya nilimtaja kaka yangu, rafiki yangu Mheshimiwa Victor Mwambalaswa, Mbunge wa Lupa. Naye juzi akajibu hapa, akanieleza mimi binafsi nilivyo na akasema amenichangia matibabu, akasema ameninunulia kompyuta yeye na rafiki zake. Kwa kweli kama nisingelelewa katika misingi ya Uislamu ningerejesha fedha ya Mheshimiwa Mwambalaswa aliyonichangia matibabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sikumwomba Mheshimiwa Mwambalaswa anichangie, nilikuwa kitandani ninaumwa, watu wakaomba mchango wakanichangia, lakini nimesikitika kwamba mchango alioutoa sirini amekuja kuusema hadharani ndani ya Bunge hili. Ni masikitiko makubwa sana, kwamba ukiwa na kiongozi wa namna hii siku akikuchangia maziko atakuja kukudai sanda au kuja kukudai jeneza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe onyo kwa Waheshimiwa Wabunge mnaochangisha michango ya harusi humu ndani ya Bunge, mkimchangisha Mheshimiwa Mwambalaswa, kuna siku atakuja kuwadai wake mnaooa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mgongano wa maslahi upo katika viongozi wetu wakubwa katika nchi hii. Mheshimiwa Ame Mpungwe alikuwa Balozi wetu wa Afrika Kusini, akawa dalali katika makampuni ya Makaburu yaliyonunua NBC, yaliyochimba Tanzanite na magazeti yaliandika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, gazeti la Rai lilihoji Balozi Mpungwe ni Balozi mzalendo au muuza nchi? Mara baada ya Balozi Mpungwe kustaafu akawa mmoja wa wamiliki wa makampuni makubwa ya uwekezaji wa madini katika nchi hii, AFGEM ya Tanzanite.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Daniel Yona aliyekuwa Waziri wetu wa Nishati na Madini alichukua dokezo akapeleka kwenye Baraza la Mawaziri la kuuza Kiwira. Kiwira ikauzwa akaanzisha Kampuni inaitwa TanPower, nayo ikaingia ubia na Kampuni nyingine inaitwa ANBEN Limited wakauziana Kiwira. Ilivyoenda Kiwira, mnaijua. Leo tunakaa hapa tunazungumza kana kwamba hayo mambo hayapo! Eti tusijadili watu waliohusika kuiingiza nchi hii katika migogoro ya kifisadi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mwambalaswa amesema kwenye Bunge hili kwamba yeye hakuwa na maslahi binafsi na mradi wa umeme wa upepo wa Singida, akiwa Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya TANESCO, mimi natoa ushahidi hapa, alikuwa na mgongano wa maslahi. Mwaka 2011 kuna invitation letter, hii hapa, inatoka China inamwalika Mheshimiwa Victor Mwambalaswa mwenye Passport number AD002021 iliyotolewa Januari, aliyezaliwa tarehe 08, issued Januari, 2006. Hii hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaliko huu anakwenda China akifuatana na William Mhando ambaye alikuwa Mkurugenzi wa TANESCO; na wengine ni Timothy Njunjua Kalinjuna na Machwa Kangoswe, hii hapa. Wanasema wanakwenda kufunga mkataba kati ya TANESCO na Kampuni ya China na Kampuni ya Power East Africa Limited ambayo ni yake. Anasafiri kwa fedha za Tanzania, anasafiri kwa passport ya Tanzania, analipwa posho ya TANESCO, anakwenda kufunga mkataba wa kampuni yake, halafu anakuja hapa anasema lile lilikuwa wazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii hapa taarifa ya NDC inasema Mradi wa Umeme wa Upepo wa Singida PT 33162, mradi umeanza mwaka 2010. Maelekezo ya mradi; mradi unatekelezwa kwa Kampuni ya Seawind Power Limited na NDC; na hiyo Power Pool East Africa Limited, ya kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2010 Mrindoko Bashiru anakuja kutoa barua hii ya kuipa kazi kampuni ya akina Mheshimiwa Mwambalaswa. Mwaka 2010, Mheshimiwa Sitta anafunga mjadala wa Richmond Bungeni kwa ubabe tu. Mwaka 2011 Mheshimiwa Mwambalaswa anakuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, mwaka 2010 Mheshimiwa Mwambalaswa anakuwa Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya TANESCO.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mambo, tunapozungumza mgongano wa maslahi ndiyo huu. Mnazungumza vitu gani humu ndani? Halafu watu wanasema hapa mnafukua makaburi, fukueni haya. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mgongano mkubwa wa maslahi. Nina orodha ndefu ya viongozi wa Serikali hii ambao mikataba iliyofungwa nyuma yao wana mgongano wa maslahi. Hatuwezi kukaa hapa tunadanganyana kwamba Taifa hili ni letu wote wakati wengine wananufaika, wengine wanaliibia Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mtu mmoja hapa amesimama asubuhi anasema nampongeza Mheshimiwa Rais. Namwomba Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli akaangalie fedha iliyotumika kulipa Kampuni ya IPTL; na Waziri wa Fedha na Mipango akaangalie. Mwaka 2010 kuelekea kipindi cha Uchaguzi Mkuu, shilingi bilioni 46 kulipia mafuta IPTL; kwa mwezi shilingi bilioni 15, Mheshimiwa Ngeleja akiwa Waziri wa Nishati na Madini na ndiye aliyesaini hiyo hoja; yule, Mheshimiwa William Ngeleja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyaraka zipo, ushahidi upo! Aende, Mheshimiwa Rais ana faili huko Ikulu afungue faili la IPTL aangalie mwaka 2010 kipindi ambacho tunaelekea kwenye Uchaguzi Mkuu. IPTL imelipwa shilingi bilioni 15 kwa mwezi kuwasha mitambo ya IPTL. Halafu mnakaa hapa tunadanganyana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa heshima kabisa, naviomba vyombo vya ulinzi na usalama viwachunguze hawa watu, hatuna maslahi binafsi, tunatetea maslahi ya Taifa letu.