Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuongea. Nianze kwanza kwa kuunga mkono hoja asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sana kumpongeza Waziri wa Fedha, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Naibu Makatibu Wakuu wote kwa bajeti nzuri ambayo inaelekea sana katika mfumo mzima wa kuboresha viwanda katika nchi yetu. Napenda vilevile kumpongeza Rais wetu wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, kwa hatua na ujasiri aliouchukua kusimamia rasilimali za nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha kuwa watu walewale ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakipigia kelele suala hili mara wamegeuka sasa wanaona kuwa ni vibaya lakini tuyaache hayo, wale wenye macho wameona, wenye masikio wanasikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitishiwa hapa kama ambavyo Viongozi wa Afrika huwa wanatishiwa wanapojitokeza kupigania rasilimali za nchi zao kuwa, watashitakiwa, hii ni mikataba mikubwa sana, haya ni Mataifa makubwa sana, hamuwezi kuwachezea hawa, wanaweza wakawafanya hivi, wakawafanya vile!

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake tumeona, huyo Rais wa Barrick Gold badala ya kutushtaki kaja mwenyewe, nginja-nginja na ndege yake mwenyewe kaja hapa anasema tuongee na hatujaambiwa, tumemsikia kwenye youtube anaongea! Tuongee tuangalie tunachotakiwa kuwalipa tuwalipe, sasa kiko wapi cha kushtakiana? Hatuwezi kuwa tunaishi kwa uwoga wakati rasilimali ni zetu wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais Magufuli endelea baba, sisi wananchi wako tuko nyuma yako, tunakuamini na tunajua unalolifanya ni kwa ajili yetu sio kwa ajili ya binafsi yako na familia yako. Endelea kutetea maslahi hayo kwa sababu huu ndio wakati muafaka, hukuwekwa pale kwa bahati mbaya, Mungu kakuweka hapo akijua makusudi gani anayo juu yako wewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale wanaosema tunaendela kuibiwa, sijui kama wametambua kuwa katika yale mapendekezo ya Kamati ya Profesa Osoro kuna suala la kuzuia sasa madini yasisafirishwe nje moja kwa moja. Zinaenda kutengenezwa clearing houses na kila yanapoondolewa madini yatafanyiwa ukaguzi na asilimia moja itatozwa palepale kwa ajili ya ukaguzi huo kwa thamani ya madini yanayotoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachotaka kuiomba Serikali ni kuwa mfanye haraka hizo clearing houses ziwekwe na tayari hili zoezi lianze kusudi madini yasiendelee kutoka. Siamini hawa jamaa wana ujasiri wa kuendelea kutuibia harakaharaka baada ya kuona eti kuwa sisi tunawadhibiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nirudi sasa kwenye masuala mazima ya hotuba yetu. Miradi ya kimkakati ni miradi ambayo imekuwa ikizungumzwa kwa miaka mingi sana. Hebu sasa Serikali amueni jambo moja, malizeni zile taratibu zote zilizobakia ambazo ni chache sana za mikataba ya uwekezaji, za maeneo ya uwekezaji, taratibu za ulipaji wa fidia, ili sasa hii miradi ya kimkakati ianze kufanya kazi kwa sababu moja kubwa, miradi hii ikianza kufanya kazi suala zima la uchumi wa viwanda litakuwa dhahiri zaidi, maana hivi ndio viwanda mama vitakavyozalisha input za kuingia katika viwanda vyetu tunavyovitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umeme tayari tunao wa kutosha, miundombinu ya barabara imeshatengenezwa ya kutosha, reli imeshaanza, tunachongojea sasa ni hii miradi mingine ya kimkakati ambayo sasa itashirikiana katika kuhakikisha kuwa viwanda vyetu vinawezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la maeneo maalum ya kiuchumi. Serikali ilituanishia maeneo maalum ya kiuchumi karibu nchi nzima, ilikuwa ni jambo jema sana, yenyewe pia yamesimama kwa muda mrefu. Hebu Serikali waje sasa na bajeti hata kama watakwenda kukopa, wamalize masuala ya fidia na miundombinu muhimu katika maeneo haya, halafu wayatangaze kwa sekta binafsi ya ndani na ya nje waje wawekeze ili wananchi kwanza wapate ajira lakini vilevile wapate mapato na nchi yetu iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna suala la PPP, najua kuwa PPP labda ni dhana ambayo haijatambulika vizuri au haieleweki vizuri kwetu. Hebu tutafute jinsi ya kuboresha uelewa wetu wa PPP tupate mafunzo Serikalini na sisi Wabunge vilevile tupate mafunzo ya kutosha, tujue jinsi gani ya kushauriana na hawa wawekezaji wanaokuja kuingia mikataba hiyo na sisi ili tupate mikataba ambayo itatunufaisha sisi wote. Kwa hiyo naomba PPP isitupwe pembeni tu kwa sababu hatuifahamu vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna suala zima la ukusanyaji wa mapato hasa kwenye Halmashauri. Tunashukuru sana Serikali kwa hatua ambazo wameziainisha ambazo wanaenda kupunguza tozo mbalimbali. Vilevile tunaomba sana kwa yale maeneo ambayo wamepunguzia Halmashauri uwezo wa kukusanya wenyewe, hebu watuhakikishie watakuwa wanaturudishia hizo fedha kwa muda mfupi kiasi gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama wanavyofahamu hata sasa hivi Halmashauri zetu nyingi zinajiendesha kwa shida sana kwa sababu vyanzo vingi vilikuwa vimechukuliwa na Serikali Kuu. Wafanye hima watakapokusanya tu waturudishie, kama vile ambavyo kila mwezi wanatangaza wamekusanya kiasi gani basi mwezi huo huo watuambie na Halmashauri wanapeleka kiasi gani. Mambo yote sasa hivi ni kielektroniki, sioni kama kutakuwa kuna ugumu katika kurudisha hizo fedha kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni juu ya kupunguza kwa tozo, crop cess. Nafikiri katika Kamati ya Bajeti tulipendekeza kuwa kusema kuwa wanapunguza tozo peke yake na kuainisha kuwa mazao yawe ni chakula na mazao yawe ni biashara inaweza ikaleta mkanganyiko na vilevile ikatumika vibaya. Waweke tozo moja na kwa vyote ili ijulikane kuwa whether inatumika kwa chakula whether inatumika kwa biashara tozo ni hiyo moja. Wasitoe mwanya kwa watu kuanza kucheza na hiyo dhana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la ufuatiliaji wa mapato na tathmini zake. Tumekuwa mara nyingi tukikadiria mapato tutapata kiasi gani kwa vyanzo mbalimbali, lakini je tunafanya tathmini labda ya miaka miwili, mitatu kuona kuwa pamoja na kuwa tulikuwa tumeweka maoteo fulani tumekuwa tumefikia kiwango hiki tu, ili itusaidie tunapopanga tupange kwa uhakika zaidi kwa uhalisia zaidi tusipange kwa vitu ambavyo pengine hatutaweza kufikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuzungumzia masuala ya elimu ya walipakodi na hasa kwenye masuala ya sekta isiyokuwa rasmi. Sekta isiyokuwa rasmi ni kubwa na itaendelea kukua na itaendelea kuwepo. Ni muhimu sasa kuhakikisha kuwa pamoja na hili suala la kuanza kuwaorodhesha au kuwa-register basi tuanze kutoa na elimu ya kulipa kodi, tuanze kuwaelekeza kodi zitakuwa za namna gani, watazilipa kwa mfumo upi, watazilipia sehemu zipi. Maana kodi zilizopo ni nyingi na zina sehemu nyingi mbalimbali za kwenda kulipia. Huu kwanza ni usumbufu lakini vilevile inaleta hali ya mkanganyiko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana watakapokuwa wakitoa elimu ya kulipa kodi wahakikishe kuwa wajasiriamali hasa wadogowadogo wanatambua kwanza wajibu wao wa kulipa kodi lakini kuwa watalipa kodi za aina gani wapi na kwa mtindo upi. Hii inatuhakikishia kuwa watu wengi watalipa kodi wakijua kuwa ni wajibu wao na siyo za usumbufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hata kwa walipa kodi wa kawaida kwa wengine bado elimu hii haijaenea ndio maana bado kuna resistance, lakini nafikiri kwa kuongeza juhudi za TRA za kutoa elimu badala ya kujikita kwenye redio na kwenye TV peke yake itasaidia zaidi. Ningependa vilevile, kupendekeza hata mashuleni sasa suala la elimu ya kulipa kodi lianze kuwekwa ili watoto wakue wakiamini kuwa kulipa kodi ni sehemu ya kuchangia maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia sana kuzungumzia suala la Ileje. Ileje ni Wilaya au hata Mkoa nzima wa Songwe ni mkoa ambao unazalisha sana mazao mbalimbali ya biashara na ya chakula. Mungu ametujalia kuwa na hali ya hewa nzuri sana, lakini hatuna masoko ya uhakika kwa mfano kahawa. Kahawa yetu lazima ipelekwe ikaweke kwenye mnada wa Kilimanjaro. Hiyo inatuletea…….

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)