Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia kwenye bajeti hii muhimu. Kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa uhai na nguvu kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wa Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri wanayoifanya. Kwa kweli nawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kipekee kumpongeza Mheshimiwa Rais, Jemedari wetu kwa kazi nzuri ambayo kwa kweli anaifanya katika Taifa hili. Kwa kweli tunamwombea kwa Mwenyezi Mungu amlinde, ampe afya njema, ampe nguvu, aendelee kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anazozifanya ambazo zinaonekana. Kuna watu wengine walikuwa wanasema aah, ndiyo tunaanza, siyo kusema ndiyo tunaanza, Mheshimiwa Rais ameshaonesha mfano mkubwa kwa kazi ambazo amezifanya, sina haja ya kuzieleza, wenye masikio wanasikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli Mheshimiwa Rais, kazi ambayo anaifanya mtu yeyote mwenye akili timamu ambaye ni mzalendo na Mtanzania, lazima apongeze kazi hii. Inasikitisha ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, anaposimama mtu ambaye anaona kazi kubwa iliyofanyika halafu anasema kilichofanyika ni upuuzi. Ni kitu ambacho kwa kweli mimi nimejiuliza sana Waheshimiwa Wabunge sijui kama na nyie mmejiuliza. Hawa watu wanadai wao ndio waliokuwa na hoja ya kusema hii mikataba mibovu haifai. Leo ni nini kilichowabadilisha? Wakati mwingine tunaweza tukaamini maneno ambayo yanayosemwa huko nje kuwa wengine kuna sehemu mmepelekwa ndiyo maana leo mmegeuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea leo mseme kwa kweli tunampongeza Mheshimiwa Rais kwa hoja ambayo tulikujanayo, sasa leo ameishikilia na sisi tunaenda naye. Leo mmegeuka, nini kilichowageuza wenzangu? Ni nani aliyewaloga? Huo upofu umetoka wapi leo? Watanzania wenye akili wanajua Rais anachokifanya na wanamuunga mkono na wanamwombea. Naamini Waheshimiwa Wabunge katika vita hii Mheshimiwa Rais atalindwa atatunzwa na hakuna kitakachomdhuru kwa sababu ni wakati wa Mungu kuitengeneza Tanzania. Ni wakati wa Mungu kurudisha vile ambavyo viliibiwa, ndiyo maana mmeona Mwenyekiti mwenyewe wa hiyo kampuni amekuja kwa ndege binafsi. Huu ni wakati wa Mungu, kwa hiyo, nyamazeni, Mungu yuko kazini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee bajeti yetu. Bajeti yetu kwa kweli ni nzuri, naipongeza sana, lakini niiombe Wizara, Mheshimiwa Waziri Mpango kuna vitu ambavyo tukiwekeza nguvu Taifa hili litainuka kwa muda mfupi. Sehemu kubwa ya Watanzania, wakulima ndio walio wengi, lakini nguvu ambayo tumeiwekeza kwenye kilimo ni ndogo sana. Naiomba sana Wizara, tunasema tunaingia kwenye Tanzania ya viwanda, hivi viwanda vitapata malighafi wapi tusipowekeza kwenye kilimo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tuwekeze kwenye kilimo ili tuweze kumwinua mkulima. Kuna mazao ambayo ni muhimu, kwa mfano, kuna mazao kama kahawa. Mazao haya tumeyaacha kwa muda mrefu, lakini mazao haya kama kahawa, korosho, tumbaku na mazao mengine yanaweza kuliingizia Taifa hili pesa nyingi na tukamwinua mkulima na kipato cha Serikali kikaongezeka. Kwa hiyo, naomba sana hilo tuliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la viwanda. Nchi hii tumejipanga kwenda kwenye viwanda. Naomba sana Wizara yangu, ili tuwe na viwanda lazima tuwe na umeme wa uhakika ambao utaweza kuendesha viwanda vyetu; lakini ukiangalia bado uzalishaji wa umeme ni mdogo kulinganisha na jinsi ambavyo tumejipanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Wizara iweze kuongeza nguvu tuweze kuzalisha umeme, tuwe na umeme wa uhakika ndipo tutafanikisha Tanzania ya viwanda na tunapowakaribisha wawekezaji ili kuwekeza kwenye viwanda, pawepo na umeme wa uhakika. Kitu kingine kwenye viwanda, tuweke mazingira ambayo ni rafiki, mazingira ambayo hata wawekezaji wakija waweze kuvutiwa na mazingira ambayo ni rafiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali kwa hizi tozo ambazo wameondoa kwenye mazao mbalimbali kama korosho na kahawa. Hili ni jambo ambalo ni zuri na litaweza kumwinua mkulima. Bado zipo tozo kwa upande wa kahawa na mazao mengine. Huyu mkulima amesahaulika sana na tunasema kilimo ni uti wa mgogo, lakini uti huu wa mgongo umesahaulika.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja.