Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii kukushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye bajeti hii ya Serikali. Nianze kwa kumpongeza sana Waziri, Mheshimiwa Mpango na Dada yangu Mheshimiwa Dkt. Kijaji kwa kazi nzuri wanazozifanya na kutuletea bajeti ambayo imejenga matumaini makubwa sana kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nami niungane na Waheshimiwa Wabunge kwa kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano kwa jinsi anavyofanya kazi. Nami nataka niseme tu, hii ni zawadi kwa Watanzania. Kama ambavyo nchi nyingine wanatamani Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli awe Rais katika nchi nyingine, sisi wote kwa pamoja tunatakiwa tuienzi hii tunu ambayo tumepata kutoka kwa Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyoeleza Mjumbe aliyetangulia kusema hapa Mheshimiwa Bura, kwamba ziko taarifa kwamba yako matumaini makubwa ya kupata zile fedha ambazo Mheshimiwa Rais alikuwa anazisema, nashauri hizi fedha zikipatikana, basi baadhi ya sehemu kubwa ya fedha hizi zielekezwe kwenye mradi wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kuzungumzia suala la uchumi bila kuhusisha suala la upatikanaji wa maji kwa wananchi wetu. Tulipendekeza kuanzia kwenye Kamati ya Bajeti lakini pia kwa Waheshimiwa Wabunge wengine kwamba tungeweza kupata Sh.50/= kwa kila lita ya mafuta ili iende kwenye maji, lakini bahati nzuri imetengwa Sh.40/= kwa kila lita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tungependa hizi fedha sasa zielekezwe kwenye maji ili ziweze kwenda kutusaidia kuwafanya Watanzania waweze kufanya kazi nyingine na kuhakikisha kwamba maji yanapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye uti wa mgongo wa Taifa letu ambao ni kilimo. Naishukuru Serikali kwamba imefanya juhudi sana za kuondoa tozo na kwenye korosho Serikali imeamua kwa mara ya kwanza kabisa kutoa sulphur bure kama ruzuku kwa wakulima wa korosho. Sasa isiishie tu kwenye kuondoa tozo, ni lazima tuelekee pia kwenye kuwatafutia masoko bora wakulima wetu ili waweze kupata masoko mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitembelewa na viongozi wengi hapa nchini akiwemo Waziri Mkuu wa India; na alipokuja alizungumza na Serikali na alizungumza na Mheshimiwa Rais, akatoa matumaini kwamba Serikali ya India iko tayari kushirikiana na Serikali ya Tanzania kununua aina zote za Kunde kwa maana ya choroko, kunde na mbaazi. Naomba Serikali iharakishe suala la mazungumzo na Serikali ya India. Hivi sasa Wakulima wa Wilaya ya Masasi na Mkoa mzima wa Mtwara kwa ujumla, waliitikia wito wa kulima mazao haya na choroko sasa ndiyo zinavunwa lakini bei imeshuka kutoka Sh.1,200/= hadi Sh. 400/= kwa kilo. Kwa hiyo, naiomba Serikali, pamoja na juhudi ya kuondoa tozo kwenye mazao, lakini ihakikishe tunapata soko zuri la mazao yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri mwingine ninaotaka kuutoa kwa Serikali; hivi karibuni Kamati ya Bajeti ilipata nafasi ya kuzungumza na wenzetu ambao wanatusaidia misaada kutoka nje. Jambo ambalo limeonekana kuchelewa kupata misaada ya nje ni kwamba tunawatoza VAT, fedha zinazoletwa hapa nchini kwa misaada ya maendeleo, jambo ambalo Mataifa yanayotoa misaada yanakataa, kwamba sisi tunatoa misaada kuwaleteeni ninyi kwa maendeleo, kwa nini mtukate VAT? Kwa hiyo, naiomba Serikali hili suala liondolewe ili kuwafanya wafadhili wetu walete zile fedha zao bila vikwazo. Sasa tunalalamika kwamba fedha haziji kumbe tatizo ni kwamba Serikali zile wamesita kuleta kwa sababu sisi tunawatoza VAT. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka nichangie ni juu ya Serikali kuona umuhimu wa kupeleka milioni 50 kwa kila kijiji. Fedha hizi zinahitajika sana kule, lakini iko haja ya kutazama pia upya jinsi ya kuzipeleka fedha zile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri badala ya kwenda kuwagawia mmoja mmoja kwa ajili ya miradi midogo midogo, ni vizuri kuchagua mradi mmoja katika Kijiji na zile fedha zikatumika shilingi milioni 50 kwa ajili ya kusaidia kwenye maendeleo ya kile kijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nilitaka nichangie kwenye bajeti hii, lakini kabla sijamaliza kuchangia nirudi kwenye kilimo kuwapongeza sana Waziri wa Kilimo na Naibu Waziri wake Mheshimiwa Ole Nasha, wanafanya kazi kubwa sana na Watanzania wana imani nao sana kwenye Sekta ya Kilimo. Naamini kabisa wataongeza bidii ili kuhakikisha wakulima wanaweza kufanya kazi yao vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwenye Sekta ya Viwanda. Ni lazima Serikali sasa tujielekeze kwenye suala la viwanda kwa moyo wa dhati kabisa na dhamira ya kweli. Tunavyo viwanda ambavyo kama tungevifufua tungeweza kuongeza uchumi wetu kwa kiasi kikubwa sana likiwemo zao la korosho. Tunavyo viwanda ambavyo vilijengwa, viwanda vile vikachukuliwa na baadhi ya watu wakisema watavifufua, lakini hadi sasa hawajafufua. Ni vizuri tukavifufua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naipongeza Serikali kwa kuwasaidia wakulima wa zao la tumbaku ambao kwa muda mrefu walikuwa wanalia, lakini naamini sasa wale wa Urambo, wale wa maeneo yote yanayolima tumbaku sasa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)