Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, lakini namshukuru pia Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na kunipa muda wa kusimama katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Mpango, Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji kwa kazi nzuri pamoja na Watendaji wengine ambao wapo chini ya Wizara hii kwa kazi nzuri ambazo wanazifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba kila jambo chini ya jua lina makusudi; na sisi tumeletwa humu ndani kwa makusudi ya Mungu.

Hata kama ulitumia njia zako za giza, lakini Mungu amekubali uingie humu kwa makusudi maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Mungu kamweka kuwa Rais wa nchi hii kwa makusudi maalum.

Kwa anayoyafanya ni makusudi ya Mungu anayoyatekeleza. Kwa hiyo, nawaomba Watanzania tudumishe amani, tudumishe umoja tunapozungumza mambo ya Kitaifa.

Nawaomba Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote wa Tanzania kwa kazi nzuri anayoifanya Mheshimiwa Dkt. Magufuli, tumwombee kwa Mwenyezi Mungu ampe afya njema, amwezeshe kuwa na hekima na maarifa ya kufanya kazi hii kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu tu. Kazi anayofanya ni kubwa, hawezi kuwa na marafiki. Marafiki wasioitakia mema Tanzania hawawezi kumpenda. Kwa hiyo, lazima tumweke kwa Mwenyezi Mungu kila siku.

Nampongeza sana kwa kazi nzuri anayofanya ya kusimamia rasilimali za Taifa hili. Nimesoma kwenye Mtandao kwamba Mwenyekiti Mtendaji wa Barrick kaingia Tanzania. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kaingia kwa ndege yake binafsi, kaja kuongea na Rais wetu kuhakikisha kwamba rasilimali, fedha ambazo hawakulipa wanalipa. Jamani, ningekuwa na uwezo ningesema Watanzania wote tumwombee huyu baba, Mungu ampe maisha marefu, lakini pia aendelee kumpa maarifa ya kutawala katika nchi yetu. Asiyemtakia mema na sisi tunamlaani kwa sababu Mungu alishatupa uwezo; ukimlaani mtu ambaye hakutakii mema na amani, analaanika. Kwa hiyo, yule ambaye hamtakii mema Rais wetu, atalaanika tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefarijika baada ya kuona makaa ya mawe ya Mchuchuma na Liganga sasa wataanza kuchimba na kiwanda kitajengwa pale na wananchi wanalipwa fidia. Tumelizungumza muda mrefu sana suala la Mchuchuma na Liganga na sasa imefika mwisho. Sasa tunaona matokeo ya Mchuchuma na Liganga. Nimeona kwenye bajeti kwamba na wananchi watalipwa fidia. Kwa hiyo, Tanzania chuma cha reli ambacho tunakitaka tutatoa Liganga kule ambako tutachimba chuma; lakini na vyuma, nondo kwa ajili ya ujenzi tutapata Liganga kwa sababu tutakuwa ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watani zangu wale wa kutoka Bukoba, reli inajengwa, watakuwa wanafika baada ya siku moja tu badala ya siku mbili. Ndugu zangu wa Mwanza na Mara watakuwa wanasafiri kwa muda wa siku moja tu kwa sababu tunajenga reli ya standard gauge. Tumpongeze Mheshimiwa Rais kwa juhudi kubwa na kazi kubwa anayoifanya ya kuwatetea Watanzania. Tulikuwa mvua ikinyesha tunalala Kilosa siku mbili, ukitoka Dar es Salaam unalala Kilosa siku mbili ndiyo ufike Dodoma. Kwa hiyo, hayo tena hatuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeze pia kwa ajili ya kuleta Makao Makuu Dodoma. Sitaacha kumpongeza Mheshimiwa Rais wangu kwa suala la Serikali kuhamia Dodoma. Nawashauri Wawekezaji, Waheshimiwa Wabunge, Dodoma viwanja vipo, fursa za uwekezaji ni nyingi, karibuni mwekeze Dodoma. Dodoma patakuwa pazuri kuliko Dar es Salaam kwa sababu tunajenga kufuata plan ya Mji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme habari ya kilimo. Nilipozungumza katika bajeti ya Mheshimiwa Waziri Mkuu niliomba kwamba suala la kilimo litiliwe mkazo kwa sababu tunataka viwanda, nchi yetu iwe ya viwanda; lakini je, tuna malighafi? Malighafi ya viwanda vya kilimo iko wapi? Nikapendekeza kwamba tuwatumie JKT katika suala la kilimo cha umwagiliaji, tutapata mazao ya kulisha viwanda vyetu. Pia tunaweza tukatumia Magereza wakalima kilimo cha umwagiliaji na tukajitosheleza kwa mazao kwa ajili ya viwanda vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ranch zetu sioni kama zinaweza ku-feed viwanda vyetu vya nyama. Hata hivyo, wafugaji bado hawajafuga ufugaji wa kisasa kiasi kwamba tunaweza tukalisha viwanda vyetu ndani ya nchi. Kwa hiyo, lazima tuwe na mikakati katika masuala ya kilimo, kilimo cha umwagiliaji, ufugaji wa kisasa lakini hata vijana wetu tunaweza tukaanzisha Makambi ya vijana kwa ajili ya ufugaji, kilimo cha horticulture, kilimo cha kisasa na tukawa na malighafi ya kutosha katika nchi yetu; na tukawawezesha hasa hawa wanaoandaa mbegu. Wazalishaji wa mbegu ni asilimia 35 tu wanazalisha, tunaweza tukawawezesha lakini kama hawawezi pia watu binafsi wanaweza kupata mikopo kutoka mabenki yetu na wakazalisha mbegu za kisasa kwa ajili ya kilimo chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusu vivutio vya utalii. Bado vivutio vyetu havijatangazwa. Tulipotangaza kidogo, Waisrael walikuja 600 kwenye utalii wa nchi yetu. Je, tukitangaza zaidi ya hapo tutapata pesa nyingi kutoka kwa watalii? Tuwafundishe watoto wetu utalii. Utalii ufundishwe mashuleni; vivutio vifundishwe mashuleni ili mtoto anapokua ajue kwamba kuna vivutio vizuri ndani ya nchi yetu. Hapa ukiwauliza Waheshimiwa Wabunge wangapi wametembela Serengeti, Selous na Mikumi, inawezekana wasifike hata 50. Kwa hiyo, hatujatangaza utalii vya kutosha. Tutangaze utalii vya kutosha tutaopata fedha za kutosha kuendesha nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Sekta ya Uvuvi tuitangaze kwa kadri inavyowezekana ili hata doria zifanyike tuone kwamba Sekta ya Uvuvi inachangiaje pato la Taifa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dodoma tuna uranium hapa Bahi, hatujaanza kuchimba. Tuna madini ya kutosha ndani ya nchi yetu; tuna nickel pale Itiso, Chamwino. Tukiweka sheria nzuri ambazo zitawabana wawekezaji kama Mheshimiwa Rais alivyoamua, tunaweza kuwa matajiri kiasi kwamba watoto wetu wakaishi maisha ambayo hawakuyatarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusiseme kwamba Tanzania ni nchi maskini, sisi sio maskini na wala tusikae tunalaumiana. Juzi juzi nilimsikia Mheshimiwa Mbunge mmoja anasema kwamba wawekezaji sio wezi, hawa wachimbaji wa madini sio wezi. Amesahau kwamba mwezi uliopita tu alisema kwamba wawekezaji ni wezi, kutokana na mikataba yetu. Tunataka kuijenga nchi yetu, tumetumwa na wananchi kuishauri Serikali. Tuishauri Serikali pamoja ili tusonge mbele katika mambo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Dabalo tunajenga Kiwanda cha Miwa na tumeshampata Mwekezaji, lakini huyu Mwekezaji hajapa hati ya kumiliki ardhi. Naiomba Serikali, mpeni yule Mwekezaji hati miliki aweze kujenga kile kiwanda na wananchi wa Dabalo ambao amewapa mikopo kwa ajili ya kulima miwa waendelee na kile kilimo na viwanda viendelee kuwa vingi vya kutosha katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)