Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Leonidas Tutubert Gama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. LEONIDAS T. GAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba niungane na wenzangu kuipongeza sana bajeti ya Serikali ya mwaka huu, ni bajeti ambayo tumeona wote, ni bajeti ya karne, bajeti ambayo haijawahi kutokea, ni bajeti ambayo imegusa kila mahali, bajeti ambayo imegusa wakulima, bajeti ambayo imegusa wafanyabiashara, bajeti ambayo imegusa wafanyabiashara wadogowadogo na akinamama lishe, bajeti ambayo imegusa viwanda, bajeti ambayo imegusa wafanyakazi, bajeti ambayo ina vipaumbele vinavyoonesha mwelekeo wa Taifa letu. Vipaumbele kama ujenzi wa reli, vipaumbele kama uanzishaji wa makaa ya mawe, vipaumbele vya ndege, vipaumbele vingi ambavyo vinaonesha mwelekeo mzuri kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumza uzuri wa bajeti hii hatuna jinsi lazima tumsifu Rais wetu. Nataka niwakumbushe tu ndugu zangu, mwaka 2015 wakati tunajiandaa na uchaguzi Mkuu, watu wote tulikwenda kwenye Makanisa yetu, tulikwenda Misikitini, tukaomba tupate Rais mzuri ambaye atasaidia nchi hii. Hakuna aliyemtazamia Mheshimiwa Magufuli. Mheshimiwa Magufuli aliibuka alikoibuka na tumefika mahali tumeona. Tunaweza tukasema Mheshimiwa Magufuli ni chaguo la Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama anavyosema mwenyewe na kama tulivyosema hapa, tumuombee. Tufike mahali tumpe moyo. Anavyovifanya havijawahi kufanyika nchi hii, tulitaka Rais wa namna gani? Kwa hiyo, nachukua nafasi hii nimpongeze sana Mheshimiwa Rais na mipango yote ya maendeleo ambayo ameipanga kwa ajili ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme kitu kimoja, Mkoa wa Ruvuma ni moja kati ya mikoa inayozalisha kwa wingi sana mazao ya chakula. Wakati fulani ulikuwa kwenye the big four, ile the big four imepungua sana sasa hivi. Nafikiri niiombe Serikali tuone namna gani tunaweza kuifanya the big four iwe kweli the big four ili tuweze kuzalisha chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza kwa Serikali, kama kuna uwezekano hebu tukusanye nguvu zetu zote badala ya kusambaza kwenye mikoa tofauti ili kujiletea uhakika wa chakula, twende tuwekeze kwenye mikoa ile yenye hali nzuri ya hewa ikiwa ni pamoja na Mkoa wa Ruvuma. Tuangalie namna ya kupeleka mbolea ya uhakika ili watu walime bila wasiwasi, tuangalie namna ya kupeleka ununuzi wa mazao ili watu wauze kwa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo hatuna sababu ya kuhangaika na njaa katika nchi hii. Tukitumia mikoa miwili, mitatu au mikoa hiyo minne, tukaamua nguvu zetu zote za uzalishaji tuzipeleke kwenye mikoa ile, nina uhakika kabisa nchi hii itaondokana kabisa na tatizo la njaa, badala ya kuhangaika, mbolea tunapunguza, tunatafuta njia tunapeleka kwenye mikoa ambayo mvua haina uhakika, tusifanye hivyo. Kwenye mikoa ambayo mvua haina uhakika tupeleke mazao ambayo yanavumilia ukame, mbolea, matunzo na shughuli zote za kilimo cha mazao ya chakula tukipele kule kwenye maeneo ambayo yanaweza kutuzalishia mazao kwa wingi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo pendekezo langu hilo la kwanza tuangalie mikoa ile ambayo ina uzalishaji mzuri, tuipeleke uzalishaji ili kuhakikisha ghala ya chakula linapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, tumezungumza kwenye bajeti hii juu ya suala zima la kupunguza asilimia tano za mazao ya mkulima mpaka asilimia tatu au mbili, lakini tumeweka vilevile kwamba usafirishaji wa mazao kutoka Wilaya moja kwenda Halmashauri nyingine yanayozidi tani moja tuweze kuya-charge. Nashauri kwamba kwa vile tumeshatoa punguzo na tayari wakulima wanakwenda kulipa asilimia tatu au mbili kwenye eneo ambalo wamezalishia basi hii tozo ya tani zaidi ya moja tuifute, tuifute ili mazao yasafiri bure, asilimia watakazolipa za CESS kwenye eneo ambalo wamezalisha iwe imetosheleza kulipa gharama zote za uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kwangu Songea ni wakulima. Tuko Songea Mjini lakini hatuwezi kulima mjini kwa mujibu wa Sheria za Mjini, kwa hiyo wakulima wa Songea Mjini wanakwenda kulima maeneo ya Halmashauri za karibu. Wanakwenda kulima Madaba, Namtumbo na Peramiho. Akishalima anatakiwa kutoa mazao yake kuyasafirisha kurudisha mjini. Sasa ukimtaka huyu alipe mara mbili atalipa CESS asilimia tatu, wakati huo huo atalipa na tani zaidi ya moja anayoisafirisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nafikiri ili tuweze kumfanya mkulima huyu apate faida kutokana na kilimo chake, basi tum-charge mara moja na kwamba aweze kusafirisha mazao kwenda Halmashauri yoyote. Napendekeza pendekezo hili lifanywe kwa mazao yote ndani ya nchi. Mtu akiwa na mahindi anataka kuyaondoa Songea kwenda kuyauza Shinyanga, aruhusiwe kupita na mahindi hayo mpaka Shinyanga, anatoka Tabora anakwenda Kigoma aruhusiwe kwenda mpaka Kigoma bila kulipa gharama yoyote zaidi ya ile asilimia ya CESS ambayo tumeiweka. Itawasaidia sana wakulima wetu kuwapa moyo katika shughuli za uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho nataka nizungumze katika bajeti hii, Mkoa wa Ruvuma ni Mkoa ambao bahati mbaya sana sio mkoa wenye viwanda. Ukienda pale Songea Mjini hakuna kiwanda chochote ukiacha kiwanda kilichoko Mbinga cha Kahawa na Kiwanda
kilichoko Tunduru cha Korosho, lakini Songea Mjini hakuna kiwanda chochote. Kwa hiyo maana yake mzunguko wa fedha ni mdogo sana kwa wananchi wa kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu alifanya ziara mwezi Januari mwaka jana kule Songea na alipofanya ziara alitembelea kiwanda cha Ngomati, kiwanda cha tumbaku. Kile kiwanda kimekufa katika mazingira ya ajabu sana, hebu tuangalie; Waziri Mkuu alisema angalieni mazingira haya ili muone namna gani tunaweza kukifufua kile kiwanda. Kwa sababu kuna tatizo kubwa la tumbaku kwa sasa kama kiwanda kile hakiwezekani kuzalishwa kwa ajili ya kuzalisha tumbaku, basi tufanye utaratibu wowote wa kupata kiwanda ambacho kitakuwa mbadala wake, maana mashine zipo, mitambo ipo, kiwanda kipo lakini kimekufa katika mazingira ya ajabu kidogo na hivyo mzunguko wa pesa ni mdogo sana kwa sababu hakuna ajira Songea Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna utaratibu ambao tumekubaliana na Serikali wa kutafuta eneo la EPZA ambalo bado halijakamilika. Naomba katika bajeti hii tukamilishe eneo la EPZA kwa ajili ya kutafuta wawekezaji ili waje kuwekeza viwanda Songea Mjini. Hii itasaidia sana kuweza kuinua uchumi na kusaidia ajira kwa wananchi wa Songea na Mkoa mzima wa Ruvuma kwa ujumla. Kwa hiyo, naomba sana Serikali iweke kipaumbele kwanza suala hili la kufufua kiwanda cha Ngomati lakini la pili ni hili la kufungua EPZA, ukanda wa viwanda ambao bahati nzuri Serikali imeshaamua, imetafuta eneo lipo pale, watu hawajalipa tumalize tatizo la kulipwa ili watu waje kuwekeza pale Songea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina uhakika kabisa viwanda vitasaidia sana hali ya uchumi ya wananchi wa Songea. Sisi tuko pembezoni sana, hatuna viwanda, hatuna shughuli zote zaidi ya kilimo, hakuna shughuli zozote za kiuzalishaji. Kwa hiyo, tukifanya hivi tutasaidia wananchi wa Songea ili wapate ajira waweze kupata uzalishaji huo utakaosaidia maeneo yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuna tatizo kubwa sana la suala la makaa ya mawe Ngaka kule Mbinga. Tuna makaa ya mawe lakini usafirishaji wa makaa yale ya mawe ni mgumu sana, unafikia mahali unaharibu barabara zetu unaharibu mazingira. Tunaomba tuone uwezekano wa kupata reli, reli ile ambayo ingejengwa kati ya Mbamba bay na Mtwara naomba iharakishwe kwenye mpango ili iingie kwenye mpango wa maendeleo ili iweze kutengenezwa reli. Reli ile itasaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niunge mkono mkono hoja.