Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nichangie katika hoja iliyoko mbele yetu. Kwanza nianze kwa kuipongeza Kamati kwa taarifa nzuri ambayo wameiwasilisha, lakini pia nimpongeze sana Mwenyekiti wa Kamati, Mheshimiwa Peter Serukamba, kwa uwasilishaji mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia fursa hii kuishukuru sana Kamati kwa namna ambavyo tumekuwa tunafanya kazi na kwa ushauri na maelekezo yao. Katika misingi hiyo, nianze tu kwa kusema kwamba Serikali imepokea ushauri ambao umetolewa na Kamati na itaufanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajielekeza katika mambo machache ambayo yamezungumzwa na Kamati na mengine ambayo yamechangiwa na Waheshimiwa Wabunge ambao wamepata nafasi ya kuchangia hoja hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ningependa kuzungumzia suala la Hospitali ya Taaluma ya Kufundishia Mloganzila. Niseme kwamba Serikali imejenga Hospitali ya kufundishia ya Mloganzila kwa lengo la kuimarisha mafunzo ya fani za afya na tiba katika nchi yetu. Hii ilitokana na dira na malengo ya chuo hicho pamoja na malengo ya Serikali ya kuhakikisha kwamba inakuwa na wataalam wa kutosha, na utaratibu wa kuwa na hospitali ya kufundishia ni utaratibu ambao upo hata katika Mataifa na nchi nyingine za Afrika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilihakikishie Bunge lako kwamba dhamira ya Serikali ya kuwa na Hospitali ya Taaluma ya Kufundishia ya Mloganzila bado iko palepale na Serikali kwa sasa haina mpango wowote kwa sababu ndiyo kwanza hospitali hiyo imekamilika, ni hospitali nzuri ya kisasa na ina uwezo wa kutoa mafunzo na tiba katika fani zote. Kwa hiyo, Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili kitaendelea na kusimamia hospitali hiyo kama ambavyo kimesimamia katika mchakato wote wa ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuzungumzia suala la vitabu ambalo limezungumziwa. Ni kweli kama ambavyo nilisema tarehe 15, Mei wakati nahitimisha hotuba, kulikuwa na changamoto ya vitabu na nikaahidi katika Bunge hili kwamba Serikali itaenda kuvifanyia kazi, kuvifanyia mapitio na kuchukua hatua kwa wale waliosababisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba kazi ya kufanya mapitio ya vitabu imekamilika na baadhi ya vitabu vilivyorekebishwa viko hapa na viko katika hatua ya uchapaji ili viweze kusambazwa. Pia niwahakikishie Wabunge kwamba Serikali itaendelea kuimarisha Taasisi yetu ya Elimu Tanzania ili iweze kutekeleza vizuri majukumu yake ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba vitabu vyote shuleni vinapatikana vikiwa na ubora unaotakiwa na kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na suala ambalo limezungumziwa la kuhusiana na Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima, kwamba hii taasisi ifutwe kwa sababu inaonekana kwamba haina tija. Ningependa kusema kwamba Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima ilianzishwa kwa Sheria Na. 139 ya Mwaka 1989 na lengo lake kubwa ilikuwa ni kutoa elimu kwa watu ambao hawakuweza kupata mafunzo katika mfumo ambao uko rasmi, lakini pia ina lengo la kutoa mafunzo endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme tu kwamba bado madhumuni ya kuanzisha taasisi hiyo yapo na Serikali itaangalia namna ya kuimarisha na tupo tayari kupokea ushauri na mapendekezo kwa namna ambavyo taasisi hii inaweza ikaimarishwa zaidi ili iendane na mahitaji ya sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo ambalo mdogo wangu, Mheshimiwa Rehema alilizungumzia, kuhusiana na suala la Waraka wa Elimu Bila Malipo na kwamba Mheshimiwa Rais ametoa maelekezo ambayo yanapingana na Waraka wa Elimu bila malipo. Ningependa tu kumwambia ndugu yangu, Mheshimiwa Rehema, Mwalimu mwenzangu Migila kwamba Serikali hii, kwanza niseme kwamba Waraka Namba Tatu wa Elimu Bila Malipo ni waraka wa Serikali na Kiongozi wa Serikali hii ya Awamu ya Tano ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Joseph Pombe Magufuli na ni Rais ambaye ni mfuatiliaji, anajua kila kitu kinachoendelea katika Serikali yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maelekezo yote ambayo Mheshimiwa Rais aliyatoa kuhusiana na elimu bila malipo, tarehe 17, Januari, 2018, hakuna hata jambo moja ambalo Mheshimiwa Rais amelisema ambalo linakinzana na Waraka wa Elimu Bila Malipo ambao ni waraka wa Serikali ambayo Kiongozi wake mkubwa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, ningependa kumshauri tu dada yangu atafute ile clip aisikilize kwa umakini kwa sababu hakuna jambo ambalo Mheshimiwa Rais alilosema ambalo ni kinyume na huo waraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuzungumzia suala la Chuo Kikuu Huria. Chuo hiki kilianzishwa kwa Sura 344, Sheria Na. 346 na kupata hati idhini mwaka 2007 na madhumuni ya kuanzisha Chuo Kikuu Huria ilikuwa ni kutoa fursa kwa watu ambao hawawezi kwenda kukaa darasani kutokana na majukumu mbalimbali kwenda kusoma kwa kutumia huo mfumo wa masafa au open and distance learning bado kuna mahitaji hata sasa ya watu kupata mafunzo kwa kupitia mfumo huo huria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Sheria ya Chuo Kikuu Huria iko hapa na majukumu ya Chuo Kikuu Huria yameainishwa vizuri na Serikali haina mpango wowote wa kufuta hicho Chuo Kikuu Huria kwa sababu inaona kwamba yale majukumu bado yanahitajika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba Serikali imekuwa ikifanya kazi kubwa ya kuimarisha miundombinu katika Sekta ya Elimu. Tumeendelea kuboresha shule zetu kongwe, nafikiri Waheshimiwa Wabunge mnaona katika maeneo yenu shule mbalimbali tumezifanyia ukarabati. Ukienda Ifakara, ukienda Musoma Technical, ukienda Ifunda, ukienda Kondoa, Masasi, Tabora Girls, Ihungo huko watani wangu hawa akina Mheshimiwa Mwijage wananiambia Mheshimiwa hii sio sekondari, wananiambia hii ni University of Ihungo kwa sababu imejengwa kwa uimara ambao uko vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea pia kuimarisha miundombinu katika vyuo vya ualimu, tunafanya ukarabati katika Chuo cha Ualimu Tandala, Chuo cha Ualimu Nachingwea, Tarime, Kinampanda, Mandaka, Patandi na Ilonga.

Hata Tarime kwako tumefika tu, sisi hatuna ubaguzi, Serikali hii inawatumikia wananchi wote hata kama ni jimbo la Upinzani tunatumikia. Kwa hiyo tupo Tarime tunafanya hiyo kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niseme kwamba tunaendelea na ujenzi katika vyuo vyetu vya ualimu ambavyo ni pamoja na Chuo cha Ualimu cha Ndala, Chuo cha Ualimu cha Mpuguso pamoja na Chuo cha Ualimu cha Shinyanga ambapo majengo ya kisasa; madarasa, mabweni, maabara, kumbi za mihadhara, inaendelea kufanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia katika vyuo vikuu tunafahamu kwamba bweni namba mbili na namba tano na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam lilikuwa limekuwa na uchakavu mkubwa mpaka lilikuwa haliwezi kutumika, Serikali hii ya Awamu ya Tano tayari imekwishaanza kulifanyia ukarabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika Chuo cha Elimu cha Mkwawa tunaendelea na ujenzi, tunakamilisha ujenzi wa ukumbi wa mihadhara ambao utaweza kuweka wanafunzi 1,200 kwa wakati mmoja, lakini pia tumewapatia shilingi bilioni mbili kwa ajili ya kujenga maabara ya chemistry. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunaendelea na ujenzi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Maktaba ambayo ina uwezo wa kuweka wanafunzi 2,500 kwa wakati mmoja. Kwa hiyo, nataka kusema tu kwamba Serikali inaendelea na jitihada katika kuboresha miundombinu katika Sekta ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la shule binafsi, wachangiaji mbalimbali wamezungumza na kuna wengine wamesema kwamba Serikali inaziingilia hizi shule. Naomba niseme tu kwamba hizi shule zipo kwa mujibu wa sheria na Wizara ya Elimu ndiyo msimamizi wa sheria za elimu, kwa hiyo, niombe tu kwamba wamiliki wa shule binafsi wanafahamu sheria na walipewa nyaraka, walipewa miongozo wakati wanasajili shule zao wahakikishe kwamba wanaendesha shule kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitakuwa ni kitu cha ajabu kwamba Serikali iache tu, kwamba kwa sababu ni shule binafsi wakati Serikali ndiyo imepewa dhamana ya kusimamia elimu ikiwa ni pamoja na shule binafsi. Kwa hiyo niseme kwenye suala la kukaririsha na suala la kufukuza wanafunzi kimsingi hivi vitu vinaongozwa na nyaraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waraka wa Elimu Na. 7 wa Mwaka 2004 ulikataza suala la kukaririsha wanafunzi au kuwafukuza wanafunzi kwa sababu hawajafikisha alama ambazo zimewekwa na shule na mitihani inayotungwa hakuna mtu ambaye anaikagua kuona kwamba ina kiwango gani lakini pia hata usahihishaji hakuna mtu ambaye anauangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Waraka Na. 12 wa Mwaka 2011 ukawa umeweka utaratibu kama kuna haja ya wanafunzi kukariri basi kuna utaratibu ambao unatakiwa kufuatwa. Kilichojitokeza, wakati shule zimeanza mwaka huu, 2018, kulikuwepo na wimbi kubwa la wanafunzi ambao walikuwa wanafukuzwa shuleni kwa sababu shule zinadai kwamba hawajafikisha zile alama na hawa wanafunzi waliokuwa wanafukuzwa ni wanafunzi ambao wako katika miaka ya mitihani; wanafunzi wa primary wa dasara la saba na wanafunzi wa sekondari wa kidato cha nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo shule ambazo shule moja ilikuwa imediriki kufukuza wanafunzi 114, shule moja inafukuza wanafunzi 35, shule moja inafukuza wanafunzi 25, hawa wanafunzi wanapokuwa wanafukuzwa kwa wingi namna hiyo wanajua kwamba wana Serikali yao na wazazi wamekuwa wanakuja kulalamika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukianza kuangalia, hivi shule moja inafukuza wanafunzi 114 kwa mkupuo kwa kigezo kwamba hawajafikisha alama. Je, tatizo ni wanafunzi au Walimu? Kwa hiyo Serikali inaliangalia hilo jambo na tunashirikiana na shule binafsi, na wenyewe wameelewa na tutaendelea kuangalia kama kuna haja ya kupitia huu waraka wa kukariri basi tutafanya katika njia shirikishi, lakini suala la kuwafukuza wanafunzi nadhani ni suala ambalo halikubaliki. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.