Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

NAIBU WAZIRI , OFISI YA WAZIRI MKUU (VIJANA, KAZI NA AJIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nitajielekeza katika kupambana na kudhibiti dawa za kulevya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo napenda kulizungumza ni suala la bajeti kama ilivyoshauriwa na Kamati. Ni kweli ukiangalia bajeti ya mwaka 2017 na mwaka 2018, bajeti hii ililenga hasa katika muundo wa iliyokuwa Tume ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya. Baada ya mabadiliko ya sheria na hivi sasa kuwa na mamlaka na kufahamu majukumu ya mamlaka, Serikali katika kipindi cha fedha cha mwaka 2018/2019, tutaangalia namna ya kuweza kuongeza bajeti ili iendane na kazi ambazo zinafanywa na mamlaka hasa kwa kuwa tumeshapata uzoefu wa kazi ya mwaka mmoja ambayo mamlaka imefanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa na hoja ya kuhusu Sera ya Taifa ya Dawa za Kulevya. Serikali inatambua umuhimu wa sera ya Taifa ya Dawa za Kulevya na utungwaji wa sera unapitia hasa katika kupata maoni ya wadau na mpaka ninapozungumza hivi sasa, tumeanza na Mikoa ya Kanda ya Ziwa ambapo tayari Mikoa ya Mwanza, Mara, Shinyanga, Kigoma na Geita wamekwishatoa maoni yao. Tunategemea kwamba katika bajeti ya mwaka 2018/2019 fedha zitaongezwa zaidi kuharakisha ukamilishaji utungwaji wa sera hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia imekuwepo hoja ya kuwepo chombo cha kisheria kushughulikia udhibiti wa biashara na matumizi ya dawa za kulevya katika ngazi ya Halmashauri kama ilivyo kwa zile Kamati za UKIMWI katika ngazi ya Halmashauri. Kwa mujibu wa kifungu cha 66 cha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Sheria Na. 5 ya mwaka 2015 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2017, sheria hii imeipa mamlaka Tume kufanya kazi na chombo chochote katika kushughulikia matatizo ya dawa za kulevya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, tayari tumeanza mazungumzo chini ya uratibu wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI, sisi pamoja na TACAIDS kuona namna bora ya kufanya suala hili la uratibu ili Kamati zile zile za UKIMWI katika ngazi ya Halmashauri pia zifanye kazi ya Kamati ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ilikuwepo hoja hapa ya changamoto za upatikanaji wa tiba kwa waathirika wa dawa za kulevya, kwa hivi sasa tunavyo vituo vitano ambavyo vinatoa tiba kwa waraibu wa madawa ya kulevya lakini mpango wetu ni kuongeza vituo vingine vitano mwaka huu wa fedha pale fedha itakapopatikana ili kuwafikia waraibu wengi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hivi sasa tunakamilisha kituo cha Itega hapa Dodoma na Mwanza ambapo kwa Dodoma tayari tumeshapokea dola milioni 2.5 kutoka Global Fund ambayo lengo lake ni ukamilishaji wa kituo hiki ili tuweze kuwafikia vijana wengi zaidi ambao ni waathirika wa dawa za kulevya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile Serikali imeongeza ukomo wa uagizaji wa dawa ya methadone kutoka kilo 120 mpaka kilo 300 na hii inatokana na mikakati tuliyonayo kama Serikali, hasa katika eneo la supply reduction, hali inayosababisha kunakuwa na upungufu mkubwa sana wa dawa za kulevya mtaani na hivyo kuwalazimu waraibu hawa kukimbia katika vituo vya tiba. Hivyo, tumeongeza ukomo wa uagizaji wa dawa ya methadone na hivi sasa ninavyozungumza muda wowote dawa hii itaingia kwa ajili ya kuweza kuwashughulikia watu walioathirika na dawa za kulevya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sita, katika sehemu ya hoja ambazo zilisemwa hapa ni kuwepo kwa unyanyapaa kwa waraibu wa dawa za kulevya. Kwa kulitambua hili, ni kweli wako vijana na watu wazima ambao wameathirika na madawa ya kulevya ambao wakirudi mtaani wanapata
unyanyapaa mkubwa sana na vilevile hali hii inawasababisha pia kurudia kufanya matumizi ya dawa za kulevya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Serikali tumeona hatua ya kwanza ni kuanzisha kituo ambacho tunakiita occupational therapy ambacho kitajengwa katika eneo la Itega Dodoma, lengo lake ni kuwapa elimu ya stadi za kazi ya fundi uashi, ufundi seremala, ili akiacha matumizi ya dawa za kulevya akirudi mtaani awe ana shughuli ya kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia limezungumzwa hapa jambo la nyumba za upataji nafuu (sober houses), Serikali inaendelea na ujenzi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii.