Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuboresha bajeti hii ambayo imewasilishwa leo asubuhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niipongeze Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Wagogo tuna msemo unaosema, chigwie misi chiliwaone wenji maana yake tukio la mchana linaonekana na watu wengi. Kwa sasa Serikali inaonekana inavyofanya kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi pamoja na Naibu wake ndugu yangu Ole-Nasha na timu nzima ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi, kwa kazi kubwa ambayo mnaifanya na inaonekana tunawapongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye kuboresha maana naiunga mkono hoja hii ya bajeti kwa asilimia 120. Haya nitakayoyazungumza ni kuboresha tu na hasa jimboni kwangu. Katika mawasilisho ya Mheshimiwa Waziri asubuhi ametaja kitu kizuri sana, amesema anawasiliana na Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kuweza kuazima magreda ili yakachimbe mabwawa kwenye maeneo yetu hasa vijijini ila wananchi tu watoe mchango wa mafuta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hivyo ndivyo, namuomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo aiorodheshe Manyoni Mashariki namba moja, haya magreda tutaanza kuyatumia sisi. Tuko tayari kuchanga mafuta na Mbunge wao nasema niko tayari, natanguliza milioni tano kama mchango. Tunawajibika kuisaidia Serikali tusisubiri tu Serikali ihudumie kila kitu, sisi Manyoni tunataka tuanze. Tutaunda Kamati, mchango huu utaanza, mtuunge mkono mlete kweli magreda, tutasimamia fedha vizuri, mafuta yatajazwa kwenye magreda, tukachimbe mabwawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Manyoni hatuna mvua za kutosha, tuna msimu mmoja tu wa mvua hatuna vuli. Mito yetu inakauka na ukichimba maji chini ukiyakuta yana chumvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niliposikia kuna magreda yanakuja kutusaidia kuchimba mabwawa nimefurahi sana. Hakika hili jambo naliunga mkono moja kwa moja; wa Manyoni mjipange magreda haya yaje kutuchimbia mabwawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la mifugo kujaa Wilaya ya Manyoni. Wilaya hii imekuwa kimbilio la wenzetu kutoka Mikoa ya Magharibi, Kaskazini, kwa kweli mifugo imejaa kiasi cha kutosha. Naona kabisa mwelekeo sasa migogoro inakwenda kuzuka Manyoni. Mbaya zaidi wahamiaji hawa wa ndani, Mtanzania unaruhusiwa kuhamia au kuishi mahali popote lakini kwa utaratibu. Kuna wahamiaji wengine ni hatari sana wanakata miti sijapata kuona. Wanapoingia wanafyeka miti sijapata kuona. Silitaji hilo kabila lakini wanakata miti sana, wamehamia pale Manyoni. Wanakata miti, wanachimba visiki, wanalima miaka miwili, wanahama, wanafyeka pori, wanachoma, wanachimba visiki yaani miaka mitatu wakihamia unaangalia unakuta miti hamna.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara isimamie jambo hili, jana bahati mbaya sikupata nafasi katika bajeti ya Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira) lakini tuna tatizo kubwa sana la wahamiaji ambao wanafyeka misitu na kuharibu mazingira Wilayani Manyoni. Naomba mtusaidie sana, elimu itolewe na watu wa Mazingira na Kilimo ili muweze kuokoa misitu hii kwenye eneo la Manyoni Mashariki, Magharibi pamoja na sehemu ya Tabora, wanafyeka sana tena kwenye vyanzo vya maji, ni hatari sana. Naomba Wizara mtusaidie jambo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kukabiliana na majanga na naomba nizungumzie majanga mawili tu. Kuna suala la upungufu wa chakula, hili ni janga, Wizara naomba ijipange vizuri. Nawashukuru sana Wilaya ya Manyoni kwa maana ya Mkoa mzima wa Singida pamoja na Wilaya nyingine zote mwaka jana hatukupata mavuno ya kutosha. Tulilima vya kutosha lakini jua likawaka, mazao yakakauka, njaa ikatukabili lakini Wizara imesaidia ikishirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, tunashukuru sana. Tulipata karibu tani 1,600 watu wetu wakapata ahueni lakini tulifanya kazi kubwa sana kwa sababu Wizara ilivyojipanga si sawasawa. Tulitumia msuli mkubwa sana mpaka watu wakaanza kuathirika. Naomba mjipange kwenye eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia mjizatiti sana kwenye suala la kukabiliana na ndege waharibifu wanaoitwa quelea-quelea wanashambulia sana eneo la kati kwenye Bonde la Ufa. Tumeshambuliwa sana mwaka huu, tumetoka kwenye njaa, sasa ndege tena wakaanza kuharibu mazao, Tunapojaribu kufuatilia Wizarani inakuwa ngumu sana, tunaomba watendaji wa Wizarani mtusaidie sana. Mpaka sasa hivi navyozungumza ndege wanakula mtama na mpunga na hata mwaka huu nadhani mavuno hayatakuwa mazuri pale kwenye Bonde la Ufa, mtusaidie sana na mjipange. Kuweni na ndege ile ya ku-spray dawa za kuua ndege wale maana tunakodisha nchi nzima hatuna ndege kwa ajili shughuli hiyo, si jambo jema. Upatikanaji wa sumu pia siyo mzuri, naomba mtusaidie sana katika kushughulikia jambo hili. Naomba mjipange ili linapotokea janga kama hili muweze kulikabili mtunusuru tuweze kuvuna.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru sana Wizara imetamka mpango wa kuondoa mageti ya ushuru kule vijijini, jambo hili tunalipokea kwa dhati. Suala hili la mageti ya ushuru imekuwa ni usumbufu mkubwa sana kwa wananchi wetu ni bora tukakutane kule kwenye soko kuliko kuweka mageti huku kusumbua wakulima. Manyoni kwa kweli tuna shida kubwa sana, gunia moja kupitisha kwenye geti pale ni shilingi 2,000 yaani unaweza ukalipia shilingi 2,000 zile karibu mara tatu. Nimefurahi haya mageti kuondolewa, ushuru utozwe sokoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi watu wa Manyoni tunaomba mbegu bora zilizofanyiwa utafiti za mazao ya biashara ya mpunga, ufuta na alizeti. Kuna mbegu moja ya ufuta inasemwa sana, nilienda siku moja Naliendele inaitwa Lindi 2002, naomba kwenye ruzuku mtukumbuke mbegu hizi zifike mapema lakini ziwe zimefanyiwa utafiti ili tukilima basi tuwe na kilimo cha tija kuwasaidia watu wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa niishukuru Wizara hii naona sasa ina vijana ambao wamejipanga vizuri, wako kila mahali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache, naunga mkono hoja kwa mara nyingine na nakushukuru sana