Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kuhusiana na taarifa iliyowasilishwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Mendeleo ya Jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nizungumze mambo machache tu. Moja ni kuhusiana na ule Mfuko wa Maendeleo hasa kwa Wanawake ile asilimia kumi.

Nakumbuka mwaka jana katika bajeti tulipendekeza kwamba katika ile asilimia tano kwa wanawake na vijana pamoja na watu wenye ulemavu wakasema kwamba iende mbili. Naiomba Serikali iweze kuleta sheria kwa sababu wengine wanafanya kwa mapenzi tu, naomba kwamba iwe sheria. Vile vile lakini vilevile Watu wa Maendeleo ya Jamii wasaidie kutoa elimu ili hata wanapopewa hiyo mikopo waweze kuitumia katika malengo yaliyokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie katika ukurasa wa hamsini ambao wamelizungumzia Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) na nakubaliana kabisa na maoni ya Kamati kwamba TBC ni shirika pekee la Serikali ambalo linategemewa kwa kazi nyingi na hata katika habari na matukio mbalimbali ya Serikali, TBC wamekuwa mstari wa mbele kuhakikisha kwamba jamii inapata taarifa hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikubaliani na maoni yao kwamba TBC ikajifunze kwa Azam TV na kwa nini sikubaliani nao. Miongoni mwa mshirika ambayo yana waandishi na wataalam wenye weledi ni TBC. Changamoto kubwa ya TBC wanayokutana nayo ni kwamba tangu mitambo imefungwa mwaka 1999 hatimaye TBC mwaka 2000 mpaka leo mitambo bado ni hiyo hiyo. TBC inakabiliwa na changamoto kubwa ya mitambo iliyochakaa na imechoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, endapo Serikali itaamua kweli kuwekeza kwa shirika hili la TBC kufunga mitambo ya kisasa na vilevile hasa kwa kuzingatia wakati tulionao hivi sasa, naamini kabisa TBC itafanya kazi vizuri na ipasavyo. Naomba niseme tu nimekuwepo kwa miaka nane katika shirika hili na nimeshuhudia, inasikitisha baadhi ya mitambo ukienda TBC wafanyakazi wa TBC wanafanya kazi katika mazingira magumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka mwaka 2008 ndipo ambapo mbali na ile studio ya awali kabisa ya mwaka 1999, baadaye wakaja wakafunga studio nyingine ndogo ambayo ndio wanayotumia kusomea habari na vipindi vya asubuhi vya jambo. Hakuna studio na mfano mzuri tu, kwa bahati nzuri tunaona wakienda kuhojiwa na hasa kipindi cha tunatekeleza, wenyewe wanashuhudia ubovu na uchakavu wa mitambo iliyopo ya TBC. Hiyo studio iliyopo ni ya tangu mwaka 1999. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali iweze kuhakikisha kwamba inazingatia umuhimu wa kuwekeza mitambo ya kisasa ili TBC iweze kutimiza majukumu yake ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka kabisa vituo vingine kwa mfano hata Azam ilivyokuwa inaanzishwa ni wataalam hao hao wa TBC ambao waliweza kwenda kusaidia katika uwekezaji wa mitambo ya kisasa. Hatuwezi kulinganisha na TBC kwa sasa kwa sababu wao wana mitambo iliyo bora zaidi na vilevile TBC mitambo yao imechoka sana. Kwa hiyo, Serikali izingatie hili, tusipende tu kumkamua ng’ombe maziwa pasipo kumlisha ipasavyo. Ikiamua kuwekeza TBC ina wafanyakazi na watumishi wenye weledi na uzoefu mkubwa na itaweza kufanya kazi zake kwa ukamilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kuhusiana na Wizara ya Habari, mchangiaji mmoja alisema kwamba Wizara ya Habari hivi sasa na hasa Idara ya Habari (Maelezo) wamekuwa wakitumika sana kuhariri au kufungia vyombo vya habari. Utaratibu uliopo na kama inavyofahamika, endapo wanataaluma wakizingatia weledi na umakini zaidi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa mzungumzaji)

Hayatoweza kutokea hayo.