Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza napongeza Kamati zote mbili kwa kazi nzuri na taarifa nzuri waliyotuletea. Nawaunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba kurudia kwamba Bunge lingeangalia mfumo wa namna ya kuboresha ili hizi Kamati tuweze kufanya kazi kwa pamoja, Kamati mbalimbali na Waheshimiwa Wabunge hawako kwenye Kamati hiyo wakitaka kuchangia pawe na namna ya kuweza kuchangia kwa sababu kwa hii siku moja Waheshimiwa Wabunge wachache, haya mawazo yetu bado hayatoshi kuboresha hizo taarifa za hizo Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la afya, naipongeza Serikali kwa kazi kubwa na nzuri ambayo inaendelea kufanywa hasa hii ya kujenga vituo vya Afya. Ombi langu ni kwamba kama kuna maeneo kwenye Kata, Wilaya au Vijiji wana ramani tofauti ambazo zinakidhi vigezo vyote na ubora wa majengo, basi hizo ramani waruhusiwe kama gharama za ujenzi zitapungua, tusiwe na mfumo ambao lazima zote zifanane nchi nzima. Watu wanaweza kuwa na design nzuri na wakaweza kujenga vituo vyao ambavyo vinapendeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwenye sekta ya afya suala la non-communicable disease (magonjwa yasiyoambukizwa) tulichukulie kwa uzito mkubwa sana. Juzi tulipofanya high camp kule Magugu kwenye watu 600 tumekuta watu zaidi 160 wana kisukari hawajijui, kuna watu zaidi ya 200 na kitu wana pressure hawajijui. Kumi kati yao ilibidi walazwe siku hiyo hiyo kwa sababu hawajui. Sasa ni jambo ambalo ni vizuri tulifanyie kazi kwa haraka na watu wapewe taarifa na wapewe elimu namna ya kujikinga na haya magonjwa na nini wafanye kama tayari wameshapata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la lishe bora. Mimi naomba Serikali iangalie upya suala la lishe bora, tutilie mkazo elimu itolewe, lakini pia tukifika kwenye Finance Bill, mwaka 2017 tuliweka kodi kwenye virutubisho vya kuongeza kwenye unga, mafuta, vitamini A. Vile virutubisho baada ya kuweka kodi, wale wote ambao walipewa misaada na USAID na wengine ambao wana viwanda vya kuongeza hivyo virutubisho, wamepunguza au wameacha kabisa kuweka. Kwa sababu huwezi kuuza unga au hayo mafuta kwa bei ya juu zaidi kuliko bei ya unga ya soko. Ina maana wenye hasara ni sisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali haina kiwanda hata kimoja, kwa hiyo, tunaposema isipokuwa kwa Serikali; Serikali haina viwanda. Kwa hiyo, wangerudisha tu ile na waangalie namna ya kuratibu kwamba hivyo virutubisho watu waendelee kupewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kuomba kwamba tuangalie namna ya kuboresha na kuongeza bajeti ya COSTECH ili suala la tafiti mbalimbali liendelee kupewa kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara safari hii ikija ituwekee bajeti kwenye Kitengo cha Ngozi pale KCMC ambacho ndiyo kitengo pekee Tanzania kinachotengeneza madawa, sunscreen yaani lotion kwa ajili ya albino (watu wenye ulemavu wa ngozi).

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka yote kuna taasisi ambayo inafadhili, inatoa huduma pale, inatengeneza, wameweza kufikia maalbino 4,000 lakini ingependeza kama Serikali ingeweka bajeti kidogo ili badala ya 4,000 wafikie hata zaidi kwani wako zaidi ya 64,000. Kwa hiyo, bado tuna hatua ndefu na Serikali ingeunga mkono pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kwenye suala la elimu, Serikali iangalie namna ya kurudisha ile 2% kati ya nne ambazo zinazotakiwa kwenda VETA kwa ajili ya Skills Development Levy (SDL). Leo hii 2% inaenda kwenye Bodi ya Mikopo. Tuangalie chanzo kingine cha kupata fedha kwa ajili ya Bodi ya Mikopo ili zile 4% zote ziende kwenye skills development kwa sababu nchi ambayo tunatarajia kuwa na viwanda, VETA ina kazi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tunatakiwa kubadilisha mitaala kwa sababu leo hii mitaala mingi bado ni ile ya tindo na nyundo na sasa hivi tunatakiwa kubadilika kwenda kwenye IT.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii hata mashine ya kushona lazima ujue namna ya ku-program. Sasa ni vizuri hata hao mafundi umeme, mafundi gari wote hao wanafundishwa VETA kwa ule mfumo wa zamani, watakuja kukosa ajira na wazazi wao wamechangia fedha nyingi. Ni vizuri tubadilishe mfumo, vitu vyote sasa vinaenda na mfumo wa IT yaani wa computer. Kwa hiyo, tuhakikishe kwamba kuanzia Juni safari hii suala la hiyo VETA na namna ya kubadilisha hiyo mitaala tuwe tumeshakamilisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ni muhimu ni suala la vyuo vyetu. Mimi ningependekeza, Chuo kwa mfano cha Sokoine ambacho ni cha Kilimo na Mifugo kingerudishwa Wizara ya Kilimo badala ya kubaki Wizara ya Elimu. Kwa sababu kwa Wizara ya Elimu inafanya kazi nzuri lakini inaona watoto wote wale ni sawa tu, bajeti inapelekewa sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri Wizara inayohusika ikisimamia chuo chake, kama Chuo cha Madini, kiko chini ya Wizara ya Madini, kile chuo kingekuwa kinapata msukumo mkubwa na Wizara ingeweza kukiangalia kwa ukaribu zaidi. Kwa hiyo, naomba suala hilo tuliangalie kwa umuhimu wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye suala la michezo, ningeomba pia Mheshimiwa Waziri angetoa tamko kwamba huko tunapokuwa na michezo katika ngazi ya Kata na ngazi ya Wilaya, hivi vyama vya mipira au vyama vya michezo vinadai sasa walipwe asilimia fulani ya fedha ambazo watu wamechangishana ili gharama za uendeshaji wakati hawajawahi kuchangia hata shilingi moja, wala kutoa elimu wala jambo lolote. Ukianzisha tu ligi, wao wanataka waingilie kati na wanataka walipwe hizo fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninashauri Mheshimiwa Waziri kwa hilo angetoa tamko ili kama wamewekeza, wana haki ya kudai, kama hawajawekeza, waachane kabisa na kudai watu wakichangishana kwa ajili ya kujiletea maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine pia ningependa tuliangalie ni kwenye suala la elimu. Ni vizuri sasa tuangalie huko tunakoelekea tunahitaji kuwa na mafundi wengi kwa ajili ya viwanda vidogo vidogo.

Pia tuondoe dhana nzima kwamba tukiwa na viwanda tutaajiri watu 4,000 au 5,000. Viwanda vya kisasa vyote vinaajiri watu wachache, skilled labour na ni vizuri sasa katika hizi taasisi zetu za kufundisha tubadilike na sisi tuwe tunaenda na mitaala hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine naomba TFDA kwa suala hilo hilo la afya sasa, wawe na mashine za kupima. Leo hii mboga mboga nyingi ambazo zinaletwa sokoni, unakuta zimepigwa dawa leo, jana, ndani ya siku mbili, tatu zinapelekwa sokoni. Ndiyo maana magonjwa mengi haya ya cancer na nini yanatokea. Hizo mashine zingekuwa zimewekwa katika maeneo mbalimbali hasa katika masoko makubwa ya mboga mboga inaweza kusaidia...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.