Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii pia kukushukuru kwa kunichagua lakini na mimi nichangie hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Kilimo kwa namna ifuatavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na dhamira njema ya Serikali ya kupunguza makato kwa wakulima lakini bado napata shida sana. Wakati Serikali inakusanya asilimia 15 mfano kwenye zao la korosho kama ushuru wa Serikali ile export levy, kwa bei ya mwaka jana ambapo tumeuza korosho kwa shilingi 2,990 tozo tu ya Serikali inakuwa ni shilingi 448.5. Leo tunasema tunataka kumsaidia mkulima huyu kwa kupunguza tozo lakini kuna tozo kubwa hii ya Serikali ambayo matumizi yake yamekuwa ni holela sana wakati mwingine hayana maelezo ambayo yanajitosheleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kuangalia mgawo wa export levy ambayo tunaipata kutoka Serikalini unakutana na asilimia tano inakwenda mkoani pamoja na wilayani ambayo wanatumia tu Wakuu wa Mikoa bila kujali maslahi ya wakulima wenyewe, kuna asilimia 20 ya ubanguaji inakwenda huko. Ukiangalia asilimia 20 ya ubanguaji Serikali hii ya CCM miaka ya 1970 na 1980 mlikopa fedha nyingi sana kutoka Japan na Italy, mkajenga viwanda vya ubanguaji wa korosho Mtwara, Lindi, Newala, Tandahimba lakini leo vile viwanda mmeviuza kwa bei chee, bei isiyoelezeka na bado tunaendelea kulipa deni kwa Wajapan hawa. Sasa kama mna nia njema, leo mnakata asilimia 20 kwa ajili ya ubanguaji wakati viwanda mmegawana wenyewe, mimi sioni u-serious wa Serikali hii ya CCM na msipoangalia tuna take off mwaka 2020. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na suala wenzangu wamelizungumza sana, la vyama vya ushirika. Kwangu Tandahimba ambayo ndio wazalishaji wakubwa wa zao la korosho hii imekuwa ni changamoto kubwa sana. Kumekuwa na mfumo mbovu wa Wizara ya Kilimo, katikati yake kuna Bodi ya Leseni pale ambao ndiyo wanawapa leseni waendesha maghala, leo ukija Wilaya ya Tandahimba wakulima wanadai zaidi ya shilingi bilioni saba kutokana na upotevu wa korosho zao kwenye maghala, lakini Serikali hii ndiyo inatoa dhamana kwa waendesha maghala. Mwendesha ghala anapewa ghala lenye thamani ya shilingi bilioni 15 za korosho za wakulima lakini security yake ni shilingi milioni arobaini. Kwa hiyo, korosho ya mkulima inapopotea hakuna anayeweza kumfidia kwa sababu hata dhamana ambayo ameweka yule warehouse operator ni ndogo kuliko korosho zinazopotea na Serikali hakuna hatua inayochukua kwa watu hawa. Mimi niombe wakati mnafanya windup ya mambo yenu, tuone namna gani wakulima wa korosho ambao wanaendelea kudai wanaweza wakafidiwa na Serikali kwa niaba ya warehouse operator walioko kule. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mmekuwa na mipango mizuri ya Serikali yenu, lakini utekelezaji wa mambo ni mbovu. Mmeendelea kuwasomesha watoto wa Kitanzania kwa ngazi ya cheti kwenye vyuo vyetu vya kilimo vya Naliendele na Ilonga pale Morogoro, kuanzia mwaka 2010 mpaka 2013 lakini vijana wale wako mtaani wakati vijijini na kwenye kata hatuna Maafisa Kilimo, mnakaa mnasema mnataka kukiinua kilimo. Tuna vijana zaidi ya 4,000 wako mtaani wametumia fedha za Serikali, vyuo vile mmewasomesha bure wale vijana kwa ngazi ya vyeti, diploma lakini mwisho hawana ajira halafu tunakaa tunalalamika hatuna wataalam wa kilimo, mko serious kweli Serikali ya CCM?
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Waziri mwenye dhamana muone namna gani wale vijana ambao wamekaa muda mrefu mtaani mnawasaidia kuwapa ajira kwa ajili ya kwenda kusimamia sekta ya kilimo kama kweli tuna dhamira njema ya kulitoa Taifa hapa lilipo kwenda mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumezungumza suala la vyama vya ushirika, hata sheria mnazozitunga, kama mlivyofanya mambo ya uteuzi wa Mawaziri wakawa hawana instrument hata kwenye ushirika mambo yako hivyo hivyo. Mmetunga sheria mkataka makatibu wa vyama vya msingi angalau wawe kidato cha nne, lakini Tanzania nzima makatibu hawa wa vyama msingi ni wa darasa la saba hata hesabu hawawezi. Tuna vijana ambao wamemaliza kidato cha nne kwenye shule za kata mlizoanzisha wanaweza kunyambua hesabu hizi, mmewaacha mtaani kwa ajili ya kuwa na watu ambao wanakibeba Chama cha Mapinduzi. Maana wakati mwingine pesa hizi zinapotea kwa ajili ya watu mnaowaweka kwa ajili ya kusaidia CCM. Sasa watumieni wasomi hawa ambao wamemaliza kwenye shule hizi za kata ambazo mmezianzisha wawasaidie kwenye sekta hii ya ushirika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu Tandahimba leo ukija kwenye ushirika hata watu mnaoweka kwenye ushirika hawa Warajisi ni miongoni mwa wala rushwa wakubwa, kabisa. Chama cha ushirika ambacho hakina uwezo wa kukusanya hata tani 50 lakini kinasajiliwa kutokana na mianya mikubwa ya rushwa. Mfanye tathmini na mje Mtwara, tutawaambieni na tutawatajia na majina. Kwa sababu unapokisajili chama kwa rushwa kwa kutumia shilingi milioni 10, 15 ambapo fedha zenyewe wanachukua kwa riba, mtu anachukua milioni 10 kwa milioni 20 kwa ajili ya kusajili chama cha ushirika lakini anakusanya tani 50 ushuru wake haumtoshi kulipa deni mwisho wa siku mkulima anakatwa pesa yake kwa sababu pesa inaingia kwenye chama cha msingi.
Niiombe Serikali na niishauri Wizara kama mna dhamira ya dhati muangalie sana jambo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niombe Wizara ya Kilimo, kuna suala la asilimia tano ya ushuru wa halmashauri. Ukisoma sheria wanasema ile asilimia tano tutaipata kutokana na market price lakini la ajabu leo sisi hatupati asilimia tano kutokana na market price. Wilaya kama ya kwangu ya Tandahimba mngekuwa mnatupa asilimia tano kutokana na market price kuna uwezekano mkubwa hata matatizo ya barabara tungeweza kutatua wenyewe. Hizi pesa mnazowapa Wakuu wa Mikoa na wa Wilaya hebu turejesheeni halmashauri ili tuendeleze Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, sitaunga mkono hoja mpaka nione majibu haya ya msingi na mambo haya mmeyaweka sawa.