Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

MHE. DKT. MARY M. NAGU - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA KILIMO, MIFUGO NA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kutoa majumuisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri naanza ili dakika zangu zisipotee.

Naomba nichukue nafasi hii ya awali kabisa kukushukuru wewe kwa kuendesha majadiliano hapa Bungeni kwa umahiri mkubwa. Nawashukuru sana Wabunge kwa kujadili na kushauri na kuonesha maeneo ambayo yalikuwa na sababu ya kuyaonesha ili Serikali iweze kuyachukulia hatua na kutekeleza ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawashukuru sana Wabunge wa Kamati yetu kwa ajili ya kufanya kazi nzuri na ninyi wote mmeshuhudia kwamba hakuna jambo jipya ila mlisisitiza zaidi yale yote yaliyokuwa kwenye taarifa ya Kamati yetu, ninawashukuru na kuwapongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wabunge waunge mkono mambo mengi ambayo tumeyaongelea kwa sababu kwa kweli ni muhimu sana, na Wabunge wengi wamejadili kwa kuongea na maandishi, jumla yao imefika 51 katika muda mfupi huu, ninawapongeza sana na kuwashukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru vilevile Mawaziri wanaoongoza sekta hii kwa kujitahidi sana kutoa na wao majibu au kuelezea mambo ambayo wameyatekeleza ninaomba wazingatie yale yote ambayo yametiliwa mkazo na Waheshimiwa Wabunge wote. Ninawashukuru kwa kuchangia hoja na kusisitiza zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawashukuru sana kuona matatizo yaliyoonekana Lake Victoria au Ziwa Victoria katika kuona kwamba Waziri kuhangaika na wenzake kuona kwamba wanajaribu kudhibiti uvuvi haramu, lakini ninaomba wachukue jitihada ambazo zitaondoa uvuvi haramu bila kukandamiza wavuvi. Vilevile jitihada zinazochukuliwa ziondoe uvuvi haramu ili tusiendelee na hayo mambo ambayo yanaumiza watu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo sikuweza kuliongelea pale kwenye taarifa lakini ipo ni kwamba Ziwa Victoria siyo la Tanzania tu ingawa sehemu kubwa ipo kwetu ni ziwa ambalo kuna nchi tatu ambazo zinazunguka, tusichukue hatua ya kunufaisha nchi zingine na kuinyima manufaa Tanzania. Vilevile nafikiri kwa sababu kuna malalamiko mengi kama walivyoomba Waheshimiwa Wabunge tuunde tume ili tuondoe malalamiko hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni migogoro ya watumiaji wa ardhi. Mheshimiwa Lukuvi alisema kwamba tume iliundwa ya Mheshimwa Sendeka, ilikuwa zaidi kati ya wafugaji na wakulima. Lakini malalamiko ya safari hii ni zaidi ya wafugaji na Hfadhi za Taifa, ninaomba kama tulivyoomba awali kwamba tuunde Tume ili migogoro hii vilevile iweze kuondoka na malalamiko yaondoke. Ninaomba Bunge liweze kuunga mkono hayo ili migogoro hii isiendelee na malalamiko ya wananchi yawe yametumika kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni la pembejeo, Waheshimiwa Wabunge bila pembejeo hakuna kilimo na hakuna tija, kwa hivyo Mheshimwa Waziri na Serikali tunaomba sana hatua mliochukua Wajumbe wa Kamati waliwaungeni mkono na Wabunge waliwaunga mkono, lakini mmeona changamoto zilizojitokeza, naomba mzitathmini, msimamie na mratibu ili kudhibiti usambazaji na upatikaji wa wakati wa pembejeo. Serikali isipofanya hivyo kilimo kitazidi kudidimia.

Lakini vilevile kuna issue ya wadudu waharibifu, tusipochukua hatua haraka mazao yatakuwa hayapo na umaskini utazidi kuingia Tanzania. Kwa hiyo, naomba sana hatua ya haraka kwa upande wa Serikali na wale wote wanaohusika kuona kwamba dawa zinapatikana au viatilifu vinapatikana ili kunusuru kuingia kwenye janga la Taifa la mazao ya kilimo. (Makofi)

Kuhusu masoko ya mazao, soko la uhakika na bei ya mazao lenye faida ni kichocheo cha uzalishaji wa mazao ya kilimo. Serikali iwe na utashi wa kusimamia kwa makini, kuratibu na kufanya utafiti wa soko la mazao. Ukosefu wa soko la mazao ya kilimo ni moja ya sababu inayofifisha kilimo nchini. Hivyo, Serikali iangalie bei ya mazao hasa katika kilimo cha mkataba, lakini vilevile Wabunge walilalamikia sana bei ya mahindi na masoko ya mahindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli lazima tuchukue hatua wakati unaotakiwa kuchukua. Kama ukiangalia Tanzania inazalisha mahindi kabla ya Zambia na Malawi, na kwa hivyo tusipotumia masoko ambayo yapo wakati tumevuna, tutakutwa na nchi za jirani na hivyo itakuwa ni sababu ya kukosa masoko kwa ajili ya mahindi yetu. Kwa hiyo. Mheshimiwa Waziri tunaomba sana pamoja na Wizara yako muwe makini sana katika kutoa uamuzi ambao unaleta hasara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ya mwisho kuhusu kilimo, ninaomba Serikali ione umuhimu wa kutoa kodi, tozo, ushuru na ada mbalimbali kwenye pembejeo na mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi pamoja na zana za sekta hiyo. Tukifanya hivyo tutahamasisha kilimo na kodi zitalipwa kwenye kununua bati, kwenye kununua cement na maeneo mengine yote na uchumi wa nchi utachanganya kwa urahisi zaidi kwa sababu kilimo ndiyo chimbuko la uchumi wa Watanzania. (Makofi)

Kwa upande wa maji; maji ni uhai, maji ni uchumi, maji ni usafi na afya. Umuhimu wa maji hauna mjadala, tunaomba wakala uanzishwe mara moja na tunaomba sana ile shilingi 50 Waheshimiwa Wabunge tuazimie tena, tulishaazimia tumuombe Waziri wa Fedha aone umuhimu wa maji ndani ya nchi hii kwa sababu utaondoa gharama za sekta zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mifugo, tunaomba Tume ya kuangalia malalamiko kama nilivyosema, lakini mifugo ni rasilimali ya Taifa na ni mali ya wafugaji mmoja mmoja, naomba tuone kwamba wafugaji wanapaswa kuhamasiswa, wafugaji wanapaswa kusaidiwa, wafugaji wanapaswa kuangaliwa ili mifugo iwe sehemu ya rasilimali ya Taifa, tusigombane na wafugaji, haitusaidii lolote na ninaomba sana mgogoro huu wa wafugaji na hifadhi uangaliwe kwa kuunda Tume. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuhusu uvuvi, naomba tuunde bandari ya uvuvi na tununue meli za uvuvi na ili tuwe na samaki wengi ambao ni rasilimali kubwa kuliko hata hayo madini tunayoyapigania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, tunaomba tuongeze thamani, kwa hiyo suala la viwanda vya kuongeza thamani na kuongeza muda wa maisha ya mazao ni jambo muhimu ambalo litawahakikishia wakulima wanaozalisha mazao ya kilimo na yanayoongeza maisha ili mazao ya kilimo yasiharibike sana kwa sababu mazao ambayo hayajaongezewa thamani, hayajachakatwa yanaharibika upesi na viwanda vinapaswa kuwa masoko.

Namshukuru sana Mheshimiwa Rais, namshukuru sana kwa yeye mwenyewe kusema kwamba viwanda ndivyo vitakavyookoa uchumi wa nchi hii na kutufikisha kwenye uchumi wa kati na mapato ya kati na tukifanya hivyo tutatuwa tumeiokoa nchi hii na mambo yataenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili nami niokoe muda niishie hapa niwaombe Waheshimiwa Wabunge waunge mkono Maazimio ambayo yako kwenye taarifa ya Wabunge ili tuweze kuimarisha sekta hizi ambazo ni muhimu na wala haina mjadala kwamba kilimo, ufugaji, uvuvi na maji ni eneo muhimu ambalo tukiliangalia vizuri nchi hii itaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sasa kutoa hoja ili Bunge liweze kupokea na kuweza kuunga mkono masuala ya Kamati hii, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja na naomba muunge mkono.