Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

Hon. Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuishukuru Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji. Katika muda wote ambao wamekuwa na Wizara yangu wamesaidia sana kubaini changamoto, kuishauri Wizara katika utendaji, lakini pia wametoa ushauri mzuri sana kwa upande wa Serikali katika hatua ya kuhakikisha kwamba tunatekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi, ili tutakapofika mwaka 2020 tufikishe maji asilimia 85 vijijini na asilimia 90 hadi asilimia 95 mijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imebainisha kuhusu mtiririko wa fedha. Nikiri kwamba, mtiririko wa fedha, hasa upande wa mfuko wa maji ni mzuri sana kwa sababu hadi kufikia Desemba tulikuwa tumeshavuka asilimia 50 na leo hii tena Hazina imetoa bilioni 14 kwa ajili ya kulipia hati za madai za wakandarasi wanaotekeleza miradi ya maji vijijini na mijini. Lakini Kamati ilibainisha pia kuhusu asilimia ya maji iliyopo upande wa vijijini kwamba ni asilimia 56.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Awamu ya Kwanza ya utekelezaji wa Mpango wa Sekta ya Maji nchini tulibainisha kutekeleza miradi 1,810 hadi desemba tulishatekeleza miradi 1,466. Katika miradi hiyo 1,466 vituo vya kuchotea maji tumefikisha 122,635 na iwapo kama vituo vyote hivyo vingetoa maji sasa hivi tungezungumzia asilimia 81.5 kwa hiyo, tulikuwa tunakaribia kwenda asilimia 85.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepata changamoto mbalimbali ikiwemo baadhi ya maeneo kukauka maji pamoja na mambo mengine, matokeo yake ni kwamba vituo vinavyotoa maji ni vituo 83,575 ndiyo sawa na asilimia 56. Vituo ambavyo havitoi maji ni vituo 39,060 sawa na asilimia 44. Lakini kwa kutambua hilo katika bajeti ya mwaka huu wa fedha tulionao Serikali imetenga shilingi bilioni 53.6 na fedha hii imepelekwa kwenye Halmashauri zote kwa ajili ya kuhakikisha kwamba vituo ambavyo havitoi maji basi fedha hiyo inatumika ili kuhakikisha kwamba vituo vinatoa maji. Kwa hiyo, kama Halmashauri zote zitafanyakazi vizuri tuna hakika mpaka tunafika mwezi wa sita tutakuwa tumeshapandisha hadi kwenda zaidi ya asilimia 76, 77 na tutaendelea kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge niwashukuru sana kwa kuendelea kusimamia Wizara hii ya Maji na Umwagiliaji na ndiyo maana sasa hadi tunafika Ijumaa waheshimiwa wabunge inabidi sasa tutoe table ambayo tunasambaza kwa wabunge wote katika mikoa ili waweze kujua katika Halmashauri yako ni vituo vingapi ambavyo havitoi maji. IIi tuweze kusaidiana kuzisukuma Halmashauri kwa sababu fedha zipo watumie fedha ile waweze kurudisha huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati pamoja na Waheshimiwa Wabunge wamechangia kuhusu kilimo cha umwagiliaji. Kweli ni kilimo muhimu ili tuweze kuwa na uhakika wa chakula. Mwaka 1970 Serikali ya Japan ilitusaidia kufanya study na ikabainisha kwamba nchi yetu ina zaidi ya hekta milioni 29.4 ambazo zinafaa kwa kilimo cha umwagiliaji na katika hizo tulitengeneza scheme za umwagiliaji hekta 461,326 sawa na asilimia 1.6.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ambayo tumekutana nayo kwamba scheme hizi zilitengenezwa bila kufikiria sasa vyanzo vya maji ambavyo vinaweza vikafanya kwamba kilimo ili kilimwe mara mbili, mara tatu kwa mwaka. Kutokana na changamoto hiyo sasa hivi kuna master plan ambayo pia tumepata msaada kutoka Serikali ya Japan ambayo ilianza mwaka 2016 na tunatarajia tarehe 1 Julai watakuwa wamekamilisha kufanya study ya hiyo Master Plan. Ili sasa kuweza kuainisha scheme za umwagiliaji pamoja na vyanzo vya maji ili tutakapokuwa tumezitengeneza wananchi waweze kulima muda wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia Wakala Maji Vijijini, Bunge lilituagiza tukaunda sekretarieti na tayari Sekretarieti imefanya kazi na kuwasilishwa kwa wadau wa Wizara ya Maji na TAMISEMI na sasa hivi mwezi huu wa pili mwishoni hiyo taarifa itafikishwa kwa Mawaziri wa TAMISEMI na Waziri wa Maji na Umwagiliaji tuweze kuipitia na baadaye tupeleke sasa kwenye hatua nyingine lengo itakapofika tarehe Julai, basi Wakala huu utakuwa umeanza kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo miradi ya kimkakati, miradi ya kimkakati tuna Bwawa la Farkwa, tuna Bwawa la Ndembela Lugoda lakini pia tumeweka Bwawa la Dongo. Bwawa hili litajengwa katika halmashauri ya Kiteto ambayo litasaidia sasa kuvuna maji ya mvua zinazonyesha maeneo ya Manyara kuleta mafuriko Mkoa wa Morogoro, tunaanza kujenga mabwawa ili sasa hayo maji tuweze kuyahifadhi maeneo na yaweze kutumika kwa matumizi ya majumbani ambayo tuna uhakika baada ya bwawa hili maji yatakwenda Gairo, yatakwenda Kibaigwa na vijiji vya Wilaya ya Kiteto pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua iliyofikiwa tayari tumeshatangaza tender na sasa hivi tuko kwenye uchambuzi ili tuweze kumpata muhandisi mshauri atakayefanyakazi kwa haraka sana na malengo yetu ni kwamba bajeti inayokuja tuweke fedha kwa ajili ya kuanza utekelezaji.