Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nami napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutujaalia kufanya shughuli zetu tukiwa na afya njema.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuishukuru sana Kamati yangu ya Miundombinu kwa taarifa nzuri na kwa mwongozo mzuri. Nachukua fursa hii kuunga mkono taarifa ya Kamati ya Miundombinu. Naomba niwahakikishie tu Kamati yetu kwamba maelekezo yote waliyotoa tutayatekeleza kwa maslahi ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano katika mwaka wa fedha 2017/2018, tulitengewa shilingi trilioni 4.5. Fedha hizi tumezitumia kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Sekta ya Uchukuzi kwa upande wa Bandari; Bandari yetu ya Dar es Salaam imeanza kuimarika vizuri kwa sababu sasa hivi tumeongeza uadilifu mkubwa na tumejipanga katika kuboresha miundombinu. Kwa taarifa tu, katika mwaka wa fedha 2016/2017, tani milioni 14.7 zilipita kwenye Bandari ya Dar es Salaam. Katika kipindi cha miezi minne kutoka Julai mpaka Septemba, miezi mitatu, quarter ya mwanzo, mizigo ya nchi za jirani imeongezeka kutoka tani milioni 1.16 mpaka tani milioni 1.479. Hii imetokana na kujipanga vizuri na wafanyakazi wetu kufanya kazi kwa uadilifu mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa mapato, mwaka 2016/2017, Bandari ya Dar es Salaam au Bandari zote zilitengeneza karibu shilingi bilioni 734.9 wakati matumizi yalikuwa shilingi bilioni 446. Salio lilikuwa ni shilingi bilioni 288. Kwa quarter ya kwanza kuanzia mwezi Julai mpaka Septemba mwaka 2017/2018, Bandari ya Dar es Salaam imekusanya mapato ya shilingi bilioni 207.5 wakati matumizi ni shilingi bilioni 67. Inaonesha sasa Bandari ya Dar es Salaam imejipanga kuhakikisha kwamba hata matumizi yenyewe wanapunguza kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, matokeo yake ni kwamba pato halisi ni shilingi bilioni 139.6. Hii ina maana, kama tutaendelea namna hii, itakapofika mwisho wa mwaka wa fedha huu, bandari itaweza kuwa na mapato halisi takriban shilingi bilioni 450. Haijawahi kutokea katika historia ya bandari zetu za Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo haya yote hayakuja bure, yamekuja kutokana na miundombinu ambayo sasa hivi inaendelea hapo Bandari ya Dar es Salaam. Tukianzia Bandari ya Dar es Salaam sasa hivi, tuna mradi mkubwa wa uboreshaji wa gati ya kwanza mpaka gati namba saba ambayo tutatumia takriban shilingi bilioni 336. Kazi kubwa inayofanyika ni kuongeza kina cha maji kwenye bandari hiyo, pia na kuboresha bandari yenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya ukarabati huo, tutahakikisha sasa meli kubwa zenye uwezo wa kuchukua kontena 19,000 za tani 20 zinaingia Bandari ya Dar es Salaam bila matatizo yoyote. Tunaamini tukifanya hivyo, tutaweza kushindana na bandari zote zilizopo katika maeneo ya jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatukusimama hapo tu, lakini hata Bandari ya Mtwara tuna mradi ambao sasa tunajenga gati jipya lenye urefu wa mita 350 ambalo lenyewe litagharimu shilingi za Kitanzania bilioni 149 na Mkandarasi yuko kwenye site na kazi inaendelea. Hatukusimamia hapo, lakini tumeendelea na ujenzi wa matishari ambayo tuyatumia kwa ajili ya kupeleka mizigo katika bandari zetu za kule Kyela na maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna mradi wa ununuzi wa scanner ambapo tayari sasa scanner nane zimefika Dar es Salaam. Kwa mara ya kwanza katika Bandari ya Dar es Salaam mwaka huu tumeingiza scanner maalum kwa ajili ya reli. Pia tumeingiza scanner nyingine nne (mobile scanners) pamoja na scanner nyingine tatu ambazo gharama yake ni shilingi bilioni 52.2. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu flow meter, kazi tunaendelea nayo ya utaratibu wa ununuzi wa flow meter na hivi karibuni manunuzi hayo yatakamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, huwezi kuwa na Bandari imara kama huna usafiri wa barabara imara. Kwa kulijua hilo, Serikali ya Awamu ya Tano tumeanza ujenzi wa reli ya kiwango cha standard gauge. Awamu ya kwanza imeanza Dar es Salaam mpaka Morogoro yenye urefu wa kilometa 300. Treni hii ni ya kipekee katika nchi za Afrika ya Mashariki na Kati. Treni hii itatumia umeme na itakuwa inakwenda mwendokasi wa kilometa 160 kwa saa. Itakuwa na uwezo wa kubeba tani milioni 17 kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu utagharimu takribani shilingi za Kitanzania trilioni 2.7. Jumatano hii Mungu akipenda, Wajumbe wa Kamati ya Bajeti na Kamati ya Miundombinu watatembelea eneo la ujenzi; na nawataka Wajumbe hawa watembelee usiku, ndiyo unaona raha ya ujenzi, siyo mchana. Pale watu wanafanya kazi saa 24 kwa wiki, siku saba.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitafurahi kama ninavyosema; na nimemwalika hapa Mheshimiwa atembelee lakini atembelee usiku, siyo mchana, kwa sababu usiku ndiyo utaona ile raha ya ujenzi wenyewe. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeanza awamu ya pili. Awamu ya pili inaanzia Morogoro mpaka Makutupora yenye urefu wa kilometa 442. Wiki iliyopita Serikali ililipa advance payment, yaani malipo ya awali dola za Kimarekani milioni 215 sawa na shilingi bilioni 483. Wakati wowote mwezi huu tutaweka jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa kutoka Morogoro mpaka Makutupora ili kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2020 ifikapo mwezi Juni, Watanzania wataanza kufurahia treni ya kisasa kutoka Dar es Salaam mpaka Dodoma ambapo sasa watatumia masaa mawili na nusu mpaka masaa matatu kutoka Dar es Salaam mpaka Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi haikuishia hapo tu, tunaendelea na mpango wa kuanzia Makutupora mpaka Tabora, Tabora - Isaka, Isaka – Mwanza. Tunatoka Tabora – Kigoma – Uvinza - Msongati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wiki mbili zilizopita, wenzetu wa Rwanda walikuja hapa na tuliweka makubaliano sasa ya kujenga reli ya kisasa kutoka Isaka mpaka Kigali yenye urefu wa kilometa 521 na tunategemea jiwe la msingi litawekwa mwezi Oktoba mwaka huu, kwa vile tumejipanga vizuri kuhakikisha kwamba Bandari ya Dar es Salaam tunaiboresha kwa miundombinu ya aina yoyote ili kuhakikisha kwamba mambo yanakwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa usafiri wa anga; ili anga zetu ziwe salama tunajipanga tunanunua radar nne za kisasa ambapo radar moja itafungwa Dar es Salaam, moja itafungwa Mwanza, moja itafungwa Mbeya na nyingine itafungwa Kilimanjaro. Hiyo imegharimu takriban shilingi za Kitanzania bilioni 63. Tunafanya hivyo kwa sababu tunapoteza mapato mengi kwenye sehemu ya madini, watu wanaingia na ndege ndogo hatuwezi kuona.

Tunaamini sasa, tukiweka radar hizo za kisasa ndege yoyote itakayoingia Tanzania hasa ndege hizi za kiraia, tutaweza kuiona na tutakusanya mapato yanayostahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa viwanja vya ndege; tunaendelea na ujenzi wa jengo la abiria pale Dar es Salaam ambalo litakuwa na uwezo wa kuchukua abiria milioni sita ikilinganishwa na jengo la abiria terminal II lenye uwezo wa kuchukua abiria milioni mbili na nusu. Jengo hili litagharimu shilingi takriban bilioni 560 litakapomalizika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wakati mmoja kwenye jengo lile zitaweza kukaa ndege 22 kwa wakati mmoja. Kwa kweli ni jengo la kisasa ambapo kazi inaendelea na ujenzi umefika asilimia 70. Kwa upande wa Mwanza, tumetenga takriban shilingi bilioni 110 ambapo tunajenga runway na maegesho mengine kuhakikisha kwamba uwanja wa Mwanza sasa unakuwa uwanja wa Kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa uwanja wa Shinyanga tumetenga shilingi bilioni 49.18 na Mkandarasi tumeshampata kwa ajili ya ujenzi. Kwa upande wa uwanja wa Sumbawanga tumetenga shilingi bilioni 55 na Mkandarasi tumempata. Kwa upande wa uwanja wa Songwe vile vile tumetenga bilioni 17 na kazi inaendelea. Uwanja wa Musoma, Songea na Iringa tayari tunahangaika kuwatafuta Wakandarasi kuhakikisha kwamba nako mambo yanakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali hii imejipanga kuunganisha mikoa yote ya Tanzania kwa kiwango cha lami. Sasa hivi kuna mradi unaendelea kutoka Katavi mpaka Tabora ambapo Serikali itatumia shilingi bilioni 770. Huu ni mradi mkubwa na tutajenga barabara ya kisasa. Pia kuna mradi unaendelea baina ya Katavi na Kigoma, Kigoma - Kagera, Kigoma - Tabora na mengineyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja ya Kamati yangu ya Miundombinu.