Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi jioni hii ya leo ili nami niweze kuchangia Kamati hizi mbili. Awali ya yote nizipongeze Kamati zote mbili kwa uwasilishaji wa umakini kabisa na kazi nzuri iliyofanywa na Kamati hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, naomba nielekeze ushauri kwa Serikali. Serikali ya Awamu ya Tano au Serikali ya Chama cha Mapinduzi hebu tupunguze umakini unaotupelekea kutokuwa makini. Kwa mfano, mradi huu wa reli ya standard gauge tumesaini mwaka mmoja na Kenya, Kenya wamemaliza lakini sisi kwa sababu ya umakini tumechelewa mpaka leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bandari ya Dar es Salaam yuko mwekezaji pale alileta ombi lake la kujenga grain terminal miaka kumi na moja (11) imekwisha mpaka leo haijajengwa amekwenda Msumbiji amepewa miaka miwili grain terminal inafanya kazi. Tanzania tuko makini mno, huu umakini ndiyo unaotupozea muda na kuonekana tuko nyuma. Naomba hilo mlichukue kama ni changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende kwenye hotuba za Kamati mbalimbali. Kamati zote ambazo zimeshawasilisha hapa taarifa zake, tatizo hili la upatikanaji wa fedha kila Kamati lazima iguse. Tunalo tatizo kwenye Serikali ya Chama cha Mapinduzi ya utoaji wa pesa, pamoja na kwamba tulipopitisha bajeti Wizara nyingi zilikuwa zinalalamikiwa kwamba pesa hazitoshi lakini hata zile kidogo zilizotengwa bado haziendi kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili limekuwa likigharimu sana miradi yetu ya maendeleo kukwama. Miradi mingi hapa ambayo leo hii haijatekelezwa tatizo kubwa ni upatikanaji wa pesa. Sasa hatuelewi tatizo hili ni nini na dawa yake ni nini, ni tatizo sugu kwa mimi ninavyoliona.

Mheshimiwa Naibu Spika, ufanisi wa bandari hasa nikianzia na bandari yetu ya Dar es Salaam. Kabla sijaingia kwenye Bunge hili Gati namba saba, moja na mengine tangu mwaka 2008 linatajwa mpaka leo lipo kwenye vitabu tu. Mnaendelea kutuchafulia makaratasi tu Gati namba tatu , namba nne hatuelewi nini kinachoendelea. Tunawaombeni sana sana wote sisi tuna uchungu na nchi hii hebu tufanye kazi tuache kufanya kazi kwa mazoea.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa viwanja vya ndege. Nashukuru Serikali imetuletea takwimu hapa, viwanja vingi vinaonekana vinataka kufanyiwa ukarabati, lakini hivi kweli tunajenga hivi viwanja hivi kwa mikakati ya kiuchumi au kukidhi matakwa ya kisiasa? Kwa sababu mimi kama ungeniuliza mikakati ya kiuchumi ningekutajia viwanja kama cha Mtwara, Kigoma, Songwe - Mbeya na hicho cha Mwanza ambacho mmekikazania.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo kubwa zaidi hatuna vipaumbele, tuna viwanja hapa tumeviandika lukuki lakini mwisho wa mwaka vyote hivi hakuna kilichokwenda. Hivi kwa nini hatuwezi kuamua tu mwaka huu tunashughulika na kiwanja namba A, mwaka mwingine namba B ili twende kuliko kurundika viwanja vya ndege lukuki ambavyo vyote hivi mwisho wa siku hatuwezi kuvifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bodi ya Wakandarasi kwa mujibu wa sheria ndiyo mlezi wa wakandarasi lakini hivi kweli bodi hii inalea wakandarasi hasa hawa wazawa, tunawajengea uwezo kiasi gani? Mikakati ya kuwajengea uwezo wakandarasi hawa wadogo tunayo, mbona haieleweki? Mimi naiomba Serikali ya Chama cha Mapinduzi sisi wote nchi hii ni ya kwetu, wote ni wazalendo na haya tunayashauri kwa uzalendo mkubwa sana, naomba myachukue. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Kamati pametajwa sera ya kuunganisha mikoa yetu kwa barabara, mikoa kadhaa imetajwa, lakini nisikitike tu Mwenyekiti wangu alisahau tu, Mkoa wa Lindi na Morogoro hajautaja. Lindi na Morogoro unaunganishwa kwenye Wilaya ya Liwale na Wilaya ya Mahenge na hili tumelipigia kelele sana lakini kwenye vitabu hivi bado halijaweza kuonekana. Nawaombeni sana jambo hili ni la muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, upande wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (USCAF). Huu Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote kwa mujibu wa taratibu unachangiwa na makampuni mbalimbali ya simu, hatujapata malalamiko kwamba makampuni haya hayajawahi kuchangia lakini tunapata malalamiko (USCAF) wana uhaba wa pesa. Sasa uhaba huu wa pesa unatoka wapi, iwapo haya makampuni yanachangia? Maana ukienda kuwauliza wanasema miradi mingi haitekelezwi kwa sababu ya pesa lakini source zile za pesa zinapatikana kwamba hawa wanachangiwa na kampuni za simu na zinachangia. Kwa nini pesa hizi Serikali hamtaki kuwapa hawa watu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile mimi niende upande wa madini, kule kwetu Mtwara kuna Kanda ya Mtwara ambayo ofisi yake moja iko Nachingwea, lakini Halmashauri ya Wilaya ya Liwale ina madini na soko lake liko Nachingwea. Sisi watu wa Halmashauri wa Wilaya ya Liwale tunapataje faida zaidi ya kuachiwa yale mashimo iwapo soko la madini liko Nachingwea na mratibu wa Kanda yuko Nachingwea. Naomba Mheshimiwa Waziri atufafanulie hili limekaaje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii.