Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 na Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017.

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ili nami niweze kuchangia kwenye hotuba mbili hizi za Kamati; Kamati ya Miundombinu lakini vilevile Kamati ya Nishati na Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa ya Kamati ya Miundombinu imesisitiza umuhimu wa kuimarisha barabara zetu. Katika ule ukurasa wa 37, anazungumzia umuhimu wa kuunganisha makao makuu ya mikoa kwa mikoa. Vilevile katika ukurasa wa 38, naomba kunukuu kipengele (d), anasema, kuendelea na ujenzi wa barabara za lami hasa maeneo yanayochochea uchumi wa Taifa letu kama vile maeneo yenye vivutio vya utalii, kilimo, viwanda na madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo hili, napenda niikumbushe Serikali, imekuwa ikitoa ahadi nyingi kwa barabara za namna hii hasa katika Mkoa wa Tanga na upande kwa Kilimanjaro. Ipo barabara inayounganisha Mkoa wa Tanga na Kilimanjaro lakini ni barabara ya kimkakati maana inapita kwenye maeneo muhimu ya ukuzaji wa uchumi, utalii na viwanda. Ni barabara kutoka Tanga – Mabokweni – Maramba - Mtoni Bombo - Mlalo - Same.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili kwanza linagusa usalama wa nchi yetu, maana ni eneo la mpakani lakini vilevile kiutalii ni eneo ambalo ukitokea ukanda wa Tanga mpaka kule Same unazungumzia kuunganisha utalii kutoka Mombasa, Saadani na Mbunga ya Mkomazi ambayo inaanzia upande wa Mkinga inakuja mpaka Mlalo, inakuja mpaka Same tunaelekea Kilimanjaro na maeneo ya namna hiyo.

Kwa hiyo, rai yangu, barabara hii imekuwa ikipewa ahadi kwa muda mrefu, ni wakati sasa upembuzi yakinifu ufanyike barabara hii iwekewe utaratibu wa kuwekewa lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikitoka kwenye taarifa ya Kamati hiyo, sasa nizungumzie taarifa ya Kamati ya Nishati. Nataka niipongeze Serikali kwa kazi kubwa inayofanya kwa kupeleka umeme vijijini kupitia mradi wa REA. Tulipoanza na REA I tulifanya makosa lakini ilikuwa ni sawasawa tufanye makosa kwa sababu tulikuwa tunajifunza. Tumekwenda REA II hali kadhalika tumefanya makosa, yapo tuliyorekebisha lakini bado kuna makosa tumefanya katika usimamizi wa miradi ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tumeingia REA III, hatuna nafasi ya kufanya makosa kwa sababu tulishapata fursa ya kufanya majaribio na ku-test jinsi yakwenda. Tunakwenda kwenye REA III tumekubaliana kwamba kila kijiji kitakachoguswa tuhakikishe hakuna kitongoji kinaachwa. Naisihi sana Serikali tusije tukarudia makosa ya REA I na REA II ya kuacha baadhi ya vitongoji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu zipo changamoto tumeanza kuziona. Kule Jimboni kwangu kwenye maeneo ya Kidiboni, Kitongoji cha Chakachani kimesahaulika. Ninayo ahadi kwamba kitafanyiwa kazi naiomba Serikali ilikumbuke hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulipofanya REA I tuliacha baadhi ya sekondari, Sekondari za Reanzoni, Duga na Kigongoi. Tunapokwenda sasa kwenye REA III kwa sababu sekondari hizi zipo jirani na maeneo haya basi tuhakikishe tunaziingiza kwenye mpango ili ziweze kupatiwa umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine nataka kuzungumzia deni la TANESCO. Ukienda ukurasa wa 23, Kamati inasema, madeni ya TANESCO yanasababisha kuzorota kwa utendaji wa shirika. Aidha, madeni yameendelea kuongezeka na hakuna jitihada zozote za Serikali za kusaidia kumalizika madeni haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii siyo hali nzuri, TANESCO ina madeni makubwa. Ukienda kwenye ukurasa ule inaonesha kwamba deni la TANESCO limefikia bilioni 913 na katika hizo takribani bilioni 200 ni madeni yanayotokana na taasisi za Serikali. Naisihi sana Serikali ije na mkakati maalum wa kuhakikisha deni hili la TANESCO linalipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Kamati tuliwahi kuletewa taarifa kwamba Serikali ina mpango wa kukopa fedha Benki ya Dunia ili tulipe madeni haya. Naisihi sana Serikali yangu isiende kukopa Benki ya Dunia ili tulipe madeni haya, tutafute njia nyingine za kulipa madeni haya. Wenzetu Afrika Kusini wana mzigo mkubwa sana kutokana na ESKOM inashindwa sasa kufanya kazi, inakuwa mzigo hata kwa nchi zinazopata umeme kutokana na Shirika la Umeme la South Africa. Tusije tukaingia kwenye mtego huo wa kusababisha tukapata umeme kutoka Afrika Kusini ambao bei yake ni ghali. Tuisaidie TANESCO iweze kutupatia umeme kwa bei ya chini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba tujifunze kwa wenzetu wa Ghana. Wenzetu Ghana waliamua kuanzisha energy bond na katika kufanya hivyo wameweza kukusanya dola milioni 750 ambazo zinaelekezwa katika sekta ya umeme. Kama tunataka kuisaidia TANESCO tuangalie option hii, tujifunze wenzetu walifanya nini, tuone kama tunaweza kuleta energy bond, wananchi wanunue bond hizo na tuweze kusaidia Shirika letu la TANESCO liondokane na mzigo wa madeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine nataka kuipongeza sana Serikali kwa uamuzi wake thabiti wa kuamua kuja na Mradi wa Umeme wa Mto Rufiji, ni hatua kubwa ya kimapinduzi, tumechelewa. Wenzetu Ethiopia wameamua kuwa energy hub saa hizi wanazungumzia kuzalisha megawatt 10,000 kutokana na chanzo cha Mto Nile. Sisi tutumie mto huu vizuri kuwekeza ili tuweze kupata umeme wa uhakika ili ndoto yetu ya kuwa na uchumi wa viwanda iweze kutimia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu tuko katika hatua za mwanzo ambazo utekelezaji utaanza hivi karibuni. Naipongeza Serikali kwa kuanza utekelezaji huu kwa kutumia bajeti za Wizara mbalimbali ili hatua za mwanzo ziweze kutekelezwa. Rai yangu, Bunge hili lishirikishwe ipasavyo, Wabunge wa Bunge hili wapate semina ya nguvu ili kujenga uelewa wa pamoja ili tutakapokuja kuleta bajeti ya mradi huu iweze kupita kwa urahisi tukiwa kitu kimoja, tukiwa tunaelewana kwamba jambo hili ni jambo la kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana.