Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia hoja iliyoko mbele yetu. Nianze kwa kuwapongeza Wenyeviti wa Kamati ya Bajeti, PIC pamoja na Kamati ya Viwanda na Biashara kwa jinsi ambavyo wameweza kutoa hoja zao lakini pia wameweza kulishauri Bunge na Serikali kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya PIC ambayo inazungumzia masuala ya uwekezaji wa mitaji ya umma. Katika Taifa la Tanzania ni kwamba Serikali iliweza kuanzisha mashirika zaidi ya 269 kwa lengo kubwa kwamba mashirika haya yaweze kufanya kazi zake vizuri na hatimaye yaweze kuweka mchango mkubwa kwa ajili ya pato la Taifa katika Taifa hili la Tanzania. Hata hivyo kwa uhalisia, baada ya kuwa tumepitia mashirika haya tumeona changamoto zipo; na ndiyo maana mashirika mengi na taasisi za umma zimeshindwa kufikia yale malengo ambayo yamekusudiwa wakati yalipoundwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya Kamati ya PIC ambayo imezungumzia kwamba Taasisi nyingi zimeshindwa kujiendesha kutokana na kuwepo na madeni makubwa ambapo Serikali inapata huduma kutoka katika Taasisi hizi, lakini Serikali inachelewa kulipa madeni hayo na hatimaye taasisi inashindwa kujiendesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo katika suala hilo tulivyokuwa tukichambua tuliona kabisa kwamba kuna baadhi ya mashirika mengi tu ikiwemo taasisi ya MSD ambayo inafanya shughuli kwa ajili ya kupeleka dawa sehemu mbalimbali katika nchi ya Tanzania. MSD inaidai Serikali zaidi ya bilioni mia moja kumi na nne; kwa hiyo kutokana na deni hilo kubwa taasisi hii inashindwa kujiendesha kwa ufanisi mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo naishauri Serikali sasa iweke mkakati madhubuti, iangalie taasisi zote ambazo inadaiwa ihakikishe kwamba inalipa madeni yote ambayo inadaiwa na taasisi hizi muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile katika madeni haya tumeona kwamba si taasisi tu ambazo zinadaiwa, tumeona pia hata halmashauri nyingi kuna wakandarasi ambao wametoa huduma mbalimbali na hatimaye Serikali imeshindwa kuwalipa kwa wakati, matokeo yake taasisi nyingi au mashirika mbalimbali yameshindwa kufanya shughuli zao kwa ufanisi mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo sasa naendelea tu kuiomba Serikali, kama ambavyo Mheshimiwa Rais anasisitiza kwamba unapopata huduma ni vizuri ukalipia kwa wakati. Kwa mfano katika suala la umeme yeye mwenyewe amesema kama mtu umetumia umeme ukishindwa kulipa basi watu wa TANESCO wakate umeme. Kwa hiyo, nasisitiza sasa kwamba Serikali iangalie uwezekano mzuri wa kuangalia madeni yote na kuweka mkakati maalum wa kuweza kuyalipa madeni hayo ili taasisi hizi ziweze kuendelea vizuri kufanya kazi zao kwa ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile katika sheria za manunuzi tuliona pia kuna changamoto kubwa kwamba taasisi nyingi zinashindwa kufanya kazi vizuri na kwa ufanisi kutokana na kwamba Sheria ya Manunuzi inakwamisha baadhi ya juhudi na shughuli mbalimbali katika kujiendeleza na kuweza kufikia ufanisi ambao taasisi inakuwa imekusudiwa. Kwa hiyo niombe Serikali sasa iangalie sheria hizi, hasa hii Sheria ya Manunuzi katika vipengele ambavyo vinakwamisha ifanye marekebisho ili taasisi hizi ziweze kufanya kazi zake kwa ufanisi mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo katika taasisi nyingi tuliona kwamba hazimtambui Msajili wa Hazina, wakati Msajili wa Hazina ndiye ambaye anasimamia taasisi hizi. Kwa hiyo tuombe Serikali iboreshe zaidi ili taasisi hizi ziweze kumtambua Msajili wa Hazina, kwa sababu ndiye anayesimamia uwekezaji wa kila siku katika taasisi hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Msajili wa Hazina aimarishwe zaidi kama alivyo CAG, tunaona CAG anafanya kazi kubwa kwa sababu ana wafanyakazi wengi na ana bajeti kubwa. Kwa hiyo niombe Serikali ili tuweze kuona mashirika haya zaidi ya 269 yanafanya kazi kwa ufanisi, ni vizuri Serikali ikaangalia uwezekano wa kumwezesha sasa hivi Msajili wa Hazina ili aweze kufanya kazi zake vizuri kwa kuzisimamia taasisi vizuri na hatimaye ziwe na mchango mkubwa kwenye pato la Taifa la Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika masuala mazima ya uwekezaji. Tumeona pia kwamba Serikali inapeleka mtaji kidogo sana kwa baadhi ya taasisi ambazo ni muhimu kama benki. Kwa mfano kuna Benki ya TIB; ambapo benki hii ni muhimu sana kwa ajili ya kuwezesha masuala ya kilimo; na tunakoelekea kwenye suala la viwanda hatuwezi kufikia kama benki hii haitawezwa inavyostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sasa Serikali iangalie namna ya kuwezesha taasisi hii, hasa Benki ya TIB kwa kuwa ni benki ambayo inashughulika na kutoa mikopo pia kwa ajili ya wakulima; na tunajua zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania wanategemea kilimo na hasa waishio vijijini. Serikali ikitoa mtaji huu itaiwezesha TIB kuweza kujitanua zaidi hata kwenye mikoa kwa sababu sasa hivi ilivyo iko kikanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia kwa mfano kanda yetu ya ziwa Benki hii ya TIB iko Mwanza Mjini. Sasa mkulima atoke Geita huko vijijini aende asafiri mpaka Mwanza mjini kwenda kutafuta huduma za fedha ili kujiimarisha naona kama ni changamoto kubwa. Kwa sababu hiyo sasa, ili iweze kufanya kazi zake kwa ufanisi mzuri taasisi hii TIB, tunaomba kwa kweli Serikali ingalie uwezekano mzuri wa kuweza kuiwezesha zaidi ili iweze kufanya kazi zake vizuri kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika masuala ya uwekezaji wa mitaji ya umma tumegundua kwamba taasisi nyingi za Serikali zinafanya kazi lakini zinafanya kazi vizuri hatimaye yale mapato ambayo inapata yanatumika yote au unakuta kwamba zaidi ya asilimia iliyowekwa kwamba kila taasisi inatakiwa itumie isizidi asilimia 60 lakini unakuta mashirika mengi yanatumia zaidi ya asilimia 60 mengine hata mpaka
90. Kwa hiyo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja.