Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi hii. Na mimi ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais kunipa dhamana hii ya kuwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi na kumuahidi kabisa kwamba nitaitumikia nafasi hii na kuwahakikishia Watanzania wenzangu kwamba nitawatumikia kupitia nafasi hii kwa nguvu zangu zote na kipaji chote nilichopewa na Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni Mapendekezo ya Mpango wetu wa Maendeleo. Waheshimiwa Wabunge wetu wamezungumza mambo mengi sana, lakini ninachotaka kusema kwa sababu haya ni mapendekezo ya mpango, zile inputs zao walizozisema tumezichukua ili sasa tuje na Mpango wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa hatujibu sana kihivyo kwa sababu tumepewa ushauri na Waheshimiwa Wabunge ili tukaandae Mpango wenyewe. Hata katika mapitio hapa nimeona kwenye Wizara yangu na wamependekeza mambo mengi, wamezungumzia suala la bandari ya uvuvi, meli ya uvuvi, umuhimu wa kuwa na viwanda vya kuchakata samaki, umuhimu wa kuwa na viwanda vya nyama, umuhimu wa kuwa na viwanda vya maziwa, haya yote ni inputs wametupa ili tukaandae Mpango wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kabisa kwamba kwa moyo mmoja, michango yote ambayo imehusu sekta yangu nimeichukua ili kwenda kutengeneza Mpango wenyewe ambao ndiyo baadae muda utakapofika tutauwasilisha hapa Bungeni na hapo ndipo mtakapoona kwamba tumefanya kufikia wapi zile inputs ambazo ninyi mmetuwekea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo na kwa sababu muda unakuwa hautoshi sana nitoe ufafanuzi wa baadhi ya mambo machache.

Moja, limezungumza sana suala hili la uchomaji wa vifaranga vya kuku 6,400 ambavyo vilikuwa vinasafirishwa kuingia nchini mwetu kutoka Kenya. Tukajaribiwa kulaumiwa sana kama Wizara na kama nchi wakati mwingine kwa kitendo hicho tulichokifanya. Jambo moja tu niseme, hapa tuko Mawaziri pamoja na Wizara yangu tumeapishwa kusimamia sheria na tunatekeleza kwa misingi ya sheria iliyowekwa katika kutekeleza majukumu yetu na kwamba hatuwezi kufanya vinginevyo kwa sababu tukifanya vinginevyo Bunge hili litatuuliza kwa nini tumefanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria yetu ya Magonjwa ya Wanyama Namba 17 ya mwaka 2003 inatoa utaratibu wa namna ya kuingiza kuku pamoja na mazao yake ndani ya nchi. Vilevile kuna mazuio ambayo yalitolewa kulingana na jambo hili. Tarehe 29 Oktoba, 2017 tulipowakamata hao vifaranga, tuliwachoma moto kwa sababu kubwa kwamba tulikuwa na zuio ambalo tulishaliweka toka tarehe 7 Juni, 2006 kwamba kutokana na tishio la ugonjwa wa mafua ya ndege lililokuwepo duniani tulilazimika kuzuia uingizaji wa kuku pamoja na mazao yake na tukawa tumezuia mtu yeyote kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu ndugu aliyeingiza hawa vifaranga kwanza aliingiza kinyume cha utaratibu bila kibali chochote ilikuwa ni illegal importation, pili, alitaka kuingiza wale kuku wakiwa hawajakaguliwa. Kwa namna yoyote ile kuingia ndani ya nchi ambako kungesababisha kero kubwa. Kwa mfano, kuku wale wangekuwa wana ugonjwa huo wa mafua ya ndege maana yake tungeua ndege wetu wote walioko hapa nchini, vilevile mafua haya ya ndege yanambukizwa mpaka kwa binadamu tungeweza kuua binadamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kuzungumza kwa urahisi jambo la vifaranga hivi kuwateketeza ukawa unazungumza tu kiurahisi kwamba unajua, sijui mambo gani! Ni lazima tuchukue hatua hizi kali kwanza kwa yule aliyefanya hivyo kuhakikisha kwamba hakuna mtu mwingine ambae atafanya jambo kama hilo, mtaji wake tumeuteketeza maana yake kama ana njia zingine ambazo alikuwa anatumia kuingiza vifaranga nchini hawezi kurudia tena, Watanznaia watuelewe kwamba tunasimamia maslahi ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuku wakifa, biashara Tanzania imekufa ya kuku, Watanzania watakufa kwa mafua ya ndege na kama Watanzania watakufa kwa mafua ya ndege kutokana na uzembe wa Wizara yangu na wale askari au watu waliokuwa wanafanya inspection kama wasingewachoma kuku siku ile, ningewafukuza kazi wote siku hiyo.

T A A R I F A . . .

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema kwamba Bunge hili ndilo ambalo linatunga sheria. Utekelezaji wa sheria hauwezi ukafanyika kama Mheshimiwa Mbunge anavyopendekeza. Sheria ya Magonjwa ya Mifugo, Magonjwa ya Wanyama Na. 17 ya mwaka 2013, Kifungu cha 8(2) kinasema “ni kukamata na kuteketeza” na siyo anavyozungumza yeye. Tumekamata na tunateketeza na tunapelaka salamu Afrika na duniani kwamba lazima wanapotaka kufanya hivyo waangalie sheria za nchi yetu zinasema nini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili tunafanya operation ya mifugo kutoka nje ya nchi. Ni takribani asilimia 30 ya malisho ya nchi hii yanalishwa na mifugo ya kutoka nje, napo tunalalamikiwa, tumekatana ng’ombe, tumekamata, tumetaifisha na tumepiga mnada. Napenda niwambie watu ambao wanatetea mambo haya, kuna jambo moja tu wanalotaka kufanya…

TAARIFA . . .

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafanya operation ya kuondoa mifugo kutoka nje ya nchi ambao wameingia nchini kinyume cha sheria. Hili pia limelalamikiwa na wakati mwingine wanaolalamika ni watunga sheria za nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa sheria hiyo niliyoitaja Sheria ya Magonjwa ya Mifugo Namba 17 ya mwaka 2013 imeonesha utaratibu wa kuingiza mifugo ndani ya nchi kutoka nchi nyingine. Ukieda kinyume na huo utaratibu umevunja sheria. Sheria hiyo pia inakataza kuingiza mifugo kwa ajili ya malisho. Watanzania wetu sasa ukiruhusu mifugo ile kuingia hapa nchini madhara yake ni nini? Madhara yake unaweza kuleta ugonjwa wa kutoka nchi jirani kuingia hapa nchini. Kwa hiyo, tumekamata ng’ombe wale 1,325 wa kutoka Kenya na sasa hivi tunashikilia ng’ombe wengine zaidi ya 10,000 kutoka Rwanda na Uganda ambao tutawapiga mnada hivi karibuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafanya hivyo kwa sababu gani, moja, kuhakikisha kwamba tunalinda mifugo ya Watanzania isipate magonjwa, mbili, tunalinda Watanzania wasipate magonjwa kupitia mifugo hiyo,tatu; tunalinda pia malisho ya Tanzania, Tanzania haiwezi ikawa malisho ya nchi za kutoka nje, nne, tunahakikisha kwamba migogoro ya wakulima na wafugaji inayochochewa na mifugo ya kutoka nje inakwisha, tano, kuhakikisha kwamba tunalinda mazingira pamoja na vyanzo vyetu vya maji ambavyo vinaharibiwa na makundi makubwa haya ya mifugo. (Makofi)

Kwa hiyo basi, watu wanaojaribu kuhusisha mahusiano yetu na Kenya pamoja na nchi zingine za jirani wanatakiwa wazingatie mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna ushirika wa uhalifu. Watu wanaoingiza mifugo kutoka nje ya nchi ni wahalifu kwa sababu wamevunja sheria na wale wanaozungumza hivyo ni kwa sababu Waziri wa Mifugo ametangaza. Je, ni Watanzania wangapi wamekamatwa Kenya leo wako lockup, wapo wamefungwa kwa kuvunja sheria nani anajua idadi? Nani anajua Watanzania ambao wako Uganda kwa kuvunja sheria leo wako mahabusu, leo wamefungwa nani anajua kuwa Rwanda, Burundi. Hivyo hivyo, mhalifu akija hapa hawezi kutetewa kwa sababu ya ushirika, ushirika wetu siyo wa uhalifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mashirikiano yetu yanayoendelea katika nchi za Afrika Mashariki ni mazuri mno, ecellent. Mahusiano tuliyonayo na Kenya ni mazuri mno kwa sababu mashirikiano yetu ni ya kisheria, mashirikiano na Uganda yapo kwa sababu ni ya kisheria. Kukamatwa kwa ng’ombe hawa ni wavunja sheria haiwezi kuhusishwa na ushirika wetu, wanashauriwa wahusika kufuata sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri nilipotangaza operation hii ya siku saba, Waziri wa Mambo ya Nje alichukua hatua ya kuzijulisha nchi zote kwamba wawaambie watu wao kuondosha mifugo Tanzania kulingana na sheria yao. Ng’ombe wengi waliondolewa, sasa hivi nimesema tuna ng’ombe 10,000 tunawashikilia ambao tutawapiga mnada hivi karibuni lakini mifugo mingi imeondolewa, wale ambao wamekaidi ukweli tutapiga mnada ng’ombe zao bila huruma, operation inaendelea na tunaendelea kuwashauri ambao hatujawakata waondoe mifugo yao kwa hiari yao.