Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia hotuba ya Waziri wa Fedha na Mipango juu ya Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2018/2019 na Mwongozo wa mMaandalizi ya Mpango wa Bajeti kwa mwaka 2018/ 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru Mungu kwa kibali chake na rehema zake kwa kutuwezesha kukutana ndani ya Bunge lako tukiwa na afya na nguvu ya kufanya kazi. Ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa uteuzi wake alioufanya hivi karibuni kwenye Baraza lile la Mawaziri na niwapongeze wote walioteuliwa na kuzidi kushirikiana vizuri huku nikiwaasa kuwa Hapa ni Kazi Tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Rais Magufuli kipekee kwa kutimiza ahadi kwa Jimbo langu la Ileje, yeye mwenyewe kwa kutujengea barabara kuu ya kutoka Mpemba hadi Isongole kwa kiwango cha lami. Barabara ya kilometa 51.8 ambayo wananchi wa Ileje wameipigia kelele kwa miaka 42 sasa. Tunaishukuru Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kutimiza ahadi zake kwa Wilaya ya Ileje. Naishukuru Serikali kwa kutujengea Hospitali kubwa ya Wilaya Itumba ambayo itafanya upasuaji mkubwa. Tunaiomba Serikali itusaidie kumalizia hospitali hii ambayo imesimama kwa zaidi ya miaka miwili sasa. Hospitali hii inategemewa na itasaidia hata Wilaya ya jirani za Mkoa wa Songwe na Mbeya Vijijini ili imaliziwe na itazuia wananchi wa Ileje kukimbilia nchi jirani ya Malawi kupata huduma za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kusaidia kuweka miundimbinu mizuri ya maji hasa maeneo ya Isongole, Itumba, Izuba Ilulu ambapo kumekuwa na ukame wakati wa kiangazi na kusababisha upungufu mkubwa wa maji wakati Mto Songwe uko hapo jirani kabisa. Hii imerudisha imani ya wananchi kwa Serikali kwa kiasi kikubwa sana na kuinua ari yao. Tunahamasisha Serikali kuhamasisha mipango yote ya maji kama ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TRA walikuwa na mpango wa kujenga kituo kidogo cha forodha kwenye mpaka wa Tanzania na Malawi kwenye Mto Songwe. Eneo limeshapimwa na TRA wamejenga ofisi ndogo ya forodha lakini bado haitoshelezi. Mpaka wa Tanzania hauna ofisi ya Uhamiaji, Polisi, Kilimo, Jeshi la Wananchi na Idara nyingine muhimu za Kituo cha Forodha Mpakani. Tunaiomba Wizara itusaidie kituo hiki kijengwe kwa kwa sababu kinapunguza msongamano wa Tunduma, kwa njia ya Ileje inapendelewa na wenye magari makubwa kwa sababu hupitia Chitipa upande wa Malawi kutokea Isongole Ileje kuja Mpemba ni tambarare zaidi kuliko ile ya Kasumulo Kyela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia itawezesha kudhibiti mpaka huu ambao umekuwa na matukio ya wakimbizi wa Kisomalia na wengine kuutumia. Kwa hali hiyo huwezi jua athari gani nyingine zinaweza kutokea bila kuwa na kituo cha forodha sehemu muhimu hiyo ya mpaka. Aidha, hicho kituo kitasidia sana pindi mradi wa Bonde la Mto Songwe kati ya Malawi na Tanzania utakapoanza. Vyote hivi vitachangia kwa kiasi kikubwa kuchangamsha uchumi wa Ileje na Wilaya za jirani ambazo kwa muda mrefu zimedumaa kwa kukosa miundombinu ya kisasa na taasisi muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kumekuwa na mwelekeo Wizara ya Mambo ya Ndani wana mpango wa kujenga Chuo cha Uhamiaji cha Ulende katika Wilaya ya Ileje na eneo tayari limeainishwa, hii pia ingesaidia sana kujenga uwezo wa Maafisa Uhamiaji wa Tanzania lakini hata wale wa nchi za SADC na hii itasaidia kuinua uchumi wa Jeshi la Tanzania kwa ujumla. Hii ni miradi ya kitaifa naomba Serikali iangalie jinsi ya kutusaidia kwa kuingiza mipango yake ya kipindi hiki ili Ileje nayo ipate maendeleo ya haraka zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ileje ni kati ya Wilaya inayozalisha mazao ya kilimo kwa wingi sana hususani mahindi, ulezi alizeti, mpunga, kahawa, pareto, hiliki, tangawizi, ndizi, viazi mviringo, viazi vitamu, soya, maharagwe, karanga, matunda ya aina mbalimbali pamoja na mazao ya misitu ikiwa ni pamoja na mbao, nyuki na kadhalika. Zaidi ya hayo Ileje ina uwezo wa kuzalisha maziwa kwa wingi, mifugo midogo midogo, viungo na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na haya yote Ileje inakabiliwa na tatizo kubwa la upungufu wa maghala, masoko, Maafisa Ugani na kwa kiasi kikubwa mitaji kwa sababu maeneo yote ya Ileje hayajapimwa na tumehusisha upungufu wa wataalam wa kupima maeneo haya. Tunaomba Serikali iweke bajeti na nguvu ya ziada na ya upendeleo kwa maeneo ya pembezoni hasa Ileje na hasa kwa sababu tumejaliwa kuwa na hali ya hewa nzuri sana, udongo mzuri, mvua nyingi na za kutosha ni rahisi kwa kilimo na ufugaji huwainua na kupanua uzalishaji sana kwa mazao yote hayo na huwaondolea wananchi kwenye umaskini na ukosefu wa ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijikite katika mpango na nianze kwa kuwapongeza sana Serikali kwa kuwashirikisha wadau katika mchakato mzima wa kutayarisha mpango na mwongozo huu, ni jambo la kupongezwa kwa sababu limekuwa shirikishi zaidi. Lakini tunaiomba Serikali iyazingatie maoni haya na kuyazingatia katika Mpango ili uwe na tija zaidi. Maoni mengi ya wadau yanaonesha uzoefu wao kwenye soko na utekelezaji ambao umezidi ule ambao watumishi wa Serikali ambao wana ofisi tu au ni wa wananchi wanaotumiwa na masuala mbalimbali kwa hiyo, siyo ya kupuuzwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali imepokea na kuorodhesha maeneo waliyopata ushauri ninaomba Serikali itupatie masharti ya jinsi wanapanga utekelezaji na fedha itakayotumia, maoni yote yaliyo ukurasa wa tano wa Mpango huu wa 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti,ni kweli uchumi wetu umekua vizuri kwa muda mrefu lakini bado kwa kiasi kikubwa tuna utegemezi mkubwa kwa wafadhili wa fedha za nje ambazo haziji zote kwa wakati. Tupate sasa wakati wa kupunguza zaidi utegemezi huu na vilevile kutumia sekta binafsi zaidi kutengeneza miradi ili kupunguza utegemezi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mfumuko wa bei kuendelea kuwa mdogo tumeona kuwa umepanda kidogo kutokana na bei za chakula kupanda na bei zinapanda kwa sababu utaratibu wa soko la mazao nchini haujawa vizuri kitu kinchosababisha wakulima kukosa mapato stahiki na wateja pia wanaathirika na kuwapa faida kubwa walanguzi. Lakini kama haitoshi zao la mahindi limekuwa yatima nchini, liliachiwa na wakulima kuhangaika wenyewe wazalishe mazao mengine kama korosho, pamba na kadhalika kunachangiwa kwa kupatiwa pembejeo, madawa na kadhalika.

Je, ni kwa nini Serikali inaacha mazao haya yanayolisha nchi nzima na kuwawezesha wananchi kunufaika kwa biashara ya mazao yao? Serikali ije na mustakabali wa kuwasaidia wakulima wa mazao ya nafaka na jamii za kunde na ya mbegu za mafuta ili ziwe na tija na yachangie Pato la Taifa na kuwaodolea umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na Deni la Taifa kuonesha liko himilivu, lakini tukiendelea hivi litatupeleka pabaya hususani kama hatutaongeza mauzo ya kuuzwa nje (exports) ili yabadilishe balance of trade yetu Tanzania. Nchi nyingi zenye deni kubwa vilevile ni nchi za viwanda zenye uchumi mkubwa, kwa hiyo malipo ya madeni hayo hayaathiri sana uendeshwaji wa uchumi. Lakini kwa Tanzania deni lilikua sana dhidi ya ukuaji wa uchumi kwa maana Pato la Taifa tutafikia hatari. Tujitahidi kuboresha na kuinua viwanda, kuanzisha viwanda vingi, huongeza masharti ya uwekezaji, kupunguza viwango vya kodi ili tupate ufanisi na mwisho wa madeni yote ya ndani na ya nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha kuwa pato la ndani halitoshi hutokana na ukusanyaji mdogo wa mapato ya ndani, uzembe na hata rushwa. Vilevile sekta isiyo rasmi imesahauliwa katika suala nzima la makusanyo ya kodi. Sekta hii ni kubwa na ina wajasiriamali wa aina mbalimbali wadogo, wa kati na wanazalisha bidhaa na huduma za kutosha na kulipa kodi nyingi. Serikali ina mpango wa kurasimisha shughuli hizi, hili ni jambo la msingi na kwa hakika zimechelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Serikali sasa hivi iweke utaratibu mzuri na ishirikishe. Aidha, Serikali ishirikishe taasisi zake zinasimamia vizuri sekta hii na kuwapatia huduma zao za kifedha na mafunzo ya kuwawezesha kuinua shughuli zao. Hii iendane na kuwapatia maeneo ya kufanyia shughuli zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza sana Serikali kwa kuanza kutengeneza miradi ya maendeleo kwa mwaka 2016/2017 pamoja na kugharamia ujenzi wa awamu ya kwanza wa reli ya kati kwa standard gauge kutoka Dar es Salaam kwenda Morogoro, pamoja na miradi mingine, miradi hii mikubwa itakayoleta mageuzi makubwa ya kiuchumi, Serikali ianze kutayarisha watumishi wa kuhudumia reli hii mapema kwa kuwapa mafunzo stahiki ili imalizike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ya msingi inayopanuliwa iendane na ujenzi wa madarasa ya kutosha, vyuo vya kutosha, maji na vyumba vya walimu na maabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ya viwanda ni muhimu sana na tuipongeze Serikali kwa kuwezesha viwanda hivi kuanza uzalishaji na kudumisha mahusiano mazuri nao. Tunaomba mvisaidie hivi viwanda kupata umeme wa gesi wa uhakika na kuhakikisha hawapati ushindani usio wa haki na bidhaa kwa mfano, mali zinazoingizwa na Good One wa China amekuwa yeye mwenyewe akiagiza na kuuza jumla na rejareja lakini huwahujumu wateja wake hao hao kwa yeye kuweka bei ndogo kwenye bidhaa zake na kufanya kushindwa kuuza. Huu ni mchezo mchafu, TFC walifuatilie hili kwa bidhaa zote zinazoingizwa na ambazo zina sababisha bidhaa za viwanda visishindwe kuuza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Serikali itenge pesa za kujenga vituo vya afya Wilayani, aidha, zahanati nyingi zilizojengwa kwa nguvu za wananchi sasa zimaliziwe kwa awamu hadi na kuweka vifaa na watumishi wa kutosha zimalizike zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapongeza juhudi za kuboresha huduma ya maji nchini. Tunaishauri Serikali itoe kipaumbele kwenye uvunaji maji ya mvua katika maeneo yenye tatizo la umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania bado tunalalamikiwa kwa urasimu mkubwa katika kuhudumia wawekezaji na bado tunachukua muda mrefu, hutoa maamuzi na tunakuwa waoga kuamua. Hii inapunguza kasi ya kufanya biashara Tanzania.Jina la Tanzania sio zuri nje ya nchi, mwisho Serikali inatuhumiwa kuwa haizingatii mikataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza Serikali kwa kuboresha huduma za afya katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, lakini kuna haja ya kuhalalisha kuwa hospitali zote za Wilaya, Kata, Mitaa zinapata huduma muhimu za kutosha na vifaa na watumishi ambao wanahitajika sana kwenye maeneo yetu nchi nzima. Pesa ya kutosha hupewa kwa ajili ya huduma za afya nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti,kwa kuhitimisha nataka kuiomba Serikali itufanyie kuboresha maendeleo ya kilimo cha kisasa, miundombinu ya vijiji na mitaa. Wakati huo huo Serikali itoe kipaumbele katika kupima maeneo ya vijijini ili kurasimisha ardhi na kuwawezesha wazalishaji kukopa. Kilimo hakionekani kuwa kweli ni uti wa mgongo na kilete tija kubwa kwa ajili ya viwanda, ajira na mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Serika ije Bungeni na mkakati wa kuanza kutekeleza miradi ya kielelezo na maeneo yale ya SEZ na EPZ ambayo yamekaa muda mrefu ilhali ni miradi muhimu kwa kuviwezesha kuanza viwanda kwa uhakika zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho tunaiomba Serikali itafakari kwa kina na kuzingatia maoni ya Wabunge kwenye Mpango wa 2018/2019.