Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kushiriki kuchangia maoni yangu juu ya Mpango. Kabla kuanza kuchangia kwanza, nimshukuru Mwenyezi Mungu lakini pia niwapongeze Mawaziri wote walioteuliwa na zaidi nimpongeze Mheshimiwa Mpango na Naibu wako pamoja na watendaji wote katika Wizara hii ya Mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma Mpango wetu ukianza na ule ukurasa wa 34 hasahasa katika suala la afya imeonesha kwamba utajikita zaidi katika kuboresha Hospitali za Kanda na Mikoa mbalimbali. Mimi nataka niongezee jambo moja kwamba katika Sera ya Afya kama ambavyo tunajua wote inatakiwa kila kijiji kiwe na zahanati, kila kata iwe na kituo cha afya na kila Wilaya iwe na hospitali. Kwa mantiki hiyo katika huu ukurasa wa 34 sijaona kama haya mmeyazingatia kufuatana na Sera ya Afya ambavyo inataka. Kwa hiyo, ningependa hili jambo mlizingatie mtakapokuwa mnaleta ile final draft.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili katika jambo hilo hilo ni katika suala la matibabu (telemedicine). Nimeona mmekazia sana kupeleka ama kutibu watu ambao tayari wameshaathirika na magojwa mbalimbali, aidha, iwe nyemelezi ama yawe magojwa yale ya kuambukiza. Kwa hiyo, nilitaka nitoe maoni yangu kwamba ni muhimu sasa kutoa elimu kwa jamii kuhusu magonjwa mbalimbali kabla ya kuanza kuyatibu kwa sababu tunasema prevention is better than cure kwa maana nyingine ni kheri kinga kuliko tiba na ndiyo maana Serikali inatumia pesa nyingi sana kutibu wakati pengine tungetumia fedha nyingi zaidi kutoa elimu kwa hayo magojwa nafikiri kizazi chetu cha Tanzania tungekuwa tuko salama zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependekeza kwamba muongeze neno ama teknolojia ya kutibu kwa njia ya mtandao (telemedicine). Hii teknolojia nimekuwa nikizungumza humu Bungeni tangu mwaka jana kwa maana itarahisisha kupunguza kwanza muda wa mgonjwa kwenda kwa daktari lakini pili elimu hii ama teknolojia hii itatibu wagonjwa wengi zaidi kwa sababu daktari anaweza akawa yuko Dar es Salaam anatibu wagonjwa ambao wako mikoani. Kama ambavyo mnafahamu madaktari tulionao ni wachache inabidi daktari mmoja huyohuyo awe fully utilized kutibu wagonjwa wengi zaidi kwa njia ya mtandao kwa maana kwamba mgonjwa anaenda sehemu ambapo kuna mawasiliano na anawasiliana na daktari wake through telemedicine. Kwa hiyo, ningefurahi zaidi kuona hii telemedicine inakuwa implemented hapa nchini Tanzania. Najua mmeshaanza pilot study lakini ni vizuri zaidi kuweza kufanya haraka zaidi kwa mikoa mingine kwa sababu wagonjwa wengi wanarundikana mahospitalini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine nikija katika suala la nishati kwa maana ya umeme, ukisoma katika Mpango wetu tumetilia mkazo zaidi kwenye umeme wa maji. Umeme huu wa maji kama mnavyofahamu kwamba unatokana zaidi na maji lakini wakati mwingine mazingira yanakuwa si rafiki sana kwa kuwa vyanzo vya maji huwa vinakauka kufuatana na mabadiliko ya tabia ya nchi ya dunia.

Kwa hiyo, ningependekeza kwamba ni vizuri sasa pia tukajikita katika umeme unaotokana na joto ardhi (geothermal), sijaona katika Mpango wetu hapa. Geothermal ni muhimu kwa sababu ule ni umeme ambao tunaita ni renewable tofauti na maji yakishatumika wakati mwingine kama vyanzo vimekauka na huku umeme hatutaweza kupata.

Umeme upo wa aina nyingi kuna ule wa upepo, wa gesi ambao tuko nao lakini nao bado haujawa effectively fully utilized pia ni vizuri tukaendelea kuu-utilize, kuna umeme wa solar energy, biomass energy lakini nikazie zaidi katika geothermal kwa sababu kuna maeneo mengi katika nchi yetu ya Tanzania geothermal ama jotoardhi umeme huu unapatikana. Zaidi katika umeme kuna hili jambo la bomba la gesi ningefurahi ama Watanzania wengi wangefurahi kuona bomba hili linaanza sasa kusambazwa mikoani kote na lisiishie tu Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nikija katika suala la maji, maji ni uzima, maji ni uhai, maji ni utu na maji ni roho. Waheshimiwa Wabunge wengi mmelalamikia hapa mara nyingi ukisoma ule ukurasa wa 32 tunaona kuna baadhi ya miradi ambayo itaendelea katika mpango ujao, ni vizuri katika Mpango wetu kama tutaunda chombo maalum kama ambavyo imeundwa TARURA kwamba chenyewe kijikite zaidi katika kuleta maji kwa maana ya vijijini na mijini. Sasa hivi kwa tafiti niliyoifanya nimeona Halmashauri nyingi sana hazina wataalamu na ndiyo maana miradi mingine mingi inashindwa kuendelea kwa sababu hamna ile M&E (Monitory and Evolution) katika ufuatiliaji wa miradi. Kwa hiyo, ombi langu ni kwamba kiundwe hicho chombo maalum kwa ajili ya suala hili la maji vijijini na mijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikija katika suala la kilimo, ukisoma ule ukurasa wa 28 utaona kwamba kilimo kimetiliwa mkazo lakini wewe Mheshimiwa Waziri unafahamu kwamba sasa tuna shida kubwa sana na masoko ya mazao ambayo tumezalisha, kila zao bei yake imeshuka. Kwa mfano, ukichukulia mahindi yameshuka, viazi nichukulie mfano kwa mfano kule tulikokuwa tunalima nyumbani debe moja lilikuwa linauzwa shilingi 10,000 hadi shilingi 15,000 lakini sasa hivi debe moja ni shilingi 2,000 kwa maana ya gunia zima ni shilingi 10,000 badala ya shilingi 65,000.

Kwa hiyo, kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara katika Mpango wetu kama wataanzisha section ambayo itakuwa inatoa taarifa kupitia njia ya teknolojia kama simu whatever kwa wakulima wote, tuwe na database ya wakulima ambao wanalima mahindi, choroko na kila aina ya zao wanapewa taarifa kupitia hizo simu walizonazo ama hiyo database ili wawataarifu sehemu gani masoko hayo kwa sasa bei ipo juu. Kwa hiyo, kama Mpango huu ungezingatia hilo ingekuwa ni jambo zuri na lenye tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika kuwekeza kwenye kilimo tumeona mazao kama chai, mahindi na baadhi ya maeneo bei ya chai ipo chini sana, lakini wenzetu jirani Kenya iko bei za juu, kwa sababu wametafuta masoko nje ya nchiyao hasa hasa Uingereza. Kwa hiyo na sisi kama tungeweza kutafuta hayo masoko ingekuwa rahisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikija katika suala la teknolojia, tumeona katika ukurasa ule wa kwanza wa mwongozo wa maandalizi wa mpango wa bajeti umezungumzia mifumo mingi ambayo itatengenezwa, mimi nitoe angalizo hapa. Tumeona teknolojia hii imekuja kwa kasi katika nchi yetu ya Tanzania pia nitoe angalizo kwa maana ya mifumo hiihiii ndiyo inatumika katika masuala ya udukuzi.

Kwa hiyo, lazima tuwe very sensitive sana tunapo- implement mifumo hii kwa kuwa hata wale wanaofanya programming, coding na vitu vingine vyote wanajua namna gani ya kuiba kupitia mifumo hii kwa kuwa mimi na wewe ambao ni end user hatuwezi kujua lakini kwa kuwa mimi nimeyaishi haya nafahamu. Kwa hiyo, ni vizuri sana haya mambo yazingatiwe katika Mpango wetu. Tusilete tu mifumo kama kuleta lakini tujue pia na consequences baada ya kutumia mifumo hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeona katika hii mifumo kwa mfano hii ya EFD, EFD ni mifumo ambayo inatumika kukadiria mapato lakini risiti zake zile baada ya muda, ukinunua leo bidhaa ukapewa risiti baada ya wiki moja ama wiki mbili au mwezi zinafutika maana yake unakuwa hakuna tena ushahidi wa kusema wewe ulitumia ile EFD. Kwa hiyo, ni vizuri zaidi kama hizo integrated systems zitakuwa na mifumo ambayo inatoa risiti ambayo ni permanent. Kwa nini mfano ukitoa photocopy karatasi idumu zaidi wakati EFD ambayo ni ya fedha isidumu, kwa hiyo, nafikiri hilo pia mliweke vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwa kuwa hizi teknolojia ni nyingi wakati mwingine wanatumia commercial software ambazo ni gharama zaidi, tunaweza tukafikiri tunapunguza gharama lakini kumbe tunaongeza gharama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ningeshauri watumie open software ambazo zinatumika nchi nyingi za Scandinavia na ambazo ndizo ziko applicable duniani kwa sasa, kwa sababu hizi commercial software ni gharama na tunakuwa hatujapunguza chochote kile zaidi ya kuongeza gharama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho katika suala la TEHAMA, ingependeza na ingefaa zaidi kuundwe Bodi ya wana-TEHAMA kama ambavyo kuna Bodi za Uhasibu, Bodi za Ukandarasi, kwa sababu teknolojia ndani ya nchi yetu inakuja kwa speed zaidi. Kama tutakuwa na hawa watu kwa pamoja maana yake itaturahisishia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi zingine kama Finland wameendelea zaidi kwa sababu waligundua ile Kampuni ya Nokia, ukienda Korea Kusini kuna Samsung, ukienda Marekani hivyo hivyo lakini tukiwa na Bodiā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.