Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Anthony Calist Komu

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na mimi kupata nafasi ya kuchangia huu Mpango ambalo ni jambo muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa sehemu ile kwenye hotuba ya Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mpango, ambapo anazungumza kwenye ukurasa wa tano juu ya kuweka nguvu kwenye maeneo ambayo yanawahusu watu walio wengi. Anasema tuweke nguvu kwenye maeneo hayo ambayo ni kilimo, uvuvi, pembejeo na mitaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninachojiuliza na ambacho mimi naona kwamba ni shida kubwa sana katika huu Mpango ni uhalisia wa hilo tamko ambalo ameliweka hapa na mambo ambayo yanafanyika. Kwa sababu tunapaswa tujiulize tukienda kwenye kilimo tuna mikakati gani ambayo inashikika ya kufanya mapinduzi ya kilimo, uhalisia hauko hivyo. Na kama hatutarekebisha hali hii kwa kweli tutaendelea kubaki watu wa kusema maneno tu na hakuna kitu ambacho kitakuwa kinafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mabonde makubwa, tuna mabonde tisa ambayo ni Rufiji, Kihansi, Pwani na kadhalika. Lakini ukijiuliza kuna mipango gani ya makusudi ya Serikali ambayo inafanya haya mabonde yaweze kuleta mapinduzi ya kilimo, ukweli ni hakuna. Na nimeangalia kwenye ukurasa wa 19 wa hotuba ya Mheshimiwa Dkt. Mpango anasema katika utekelezaji wa bajeti iliyopita wameweza kutenga vyanzo vya maji 78 na kutangaza kwamba haya ni maeneo tengefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni utani, kwa sababu kwa taarifa ambayo sisi tulipata kwenye Kamati yetu ya Mazingira, Bonde la Kihansi peke yake lina vyanzo 901, katika vyanzo hivyo ni asilimia 27 tu ambayo imeshatambuliwa, kuwekewa mipaka na kutangazwa kama ni maeneo ambayo ni tengefu. Maana yake kuna maeneo zaidi ya 600 hayajafanyiwa chochote na maana yake ni kwamba hayawezi kutumika vizuri kwa ajili ya kuleta mapinduzi ya kilimo. Kwa hiyo, katika hali kama hii unaweza ukasema kwamba hatuko serious na hatumaanishi haya ambayo tunayasema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Kamati yetu vilevile ya mazingira tulianzisha hapa Mfuko wa Mazingira na ukazinduliwa na Mheshimiwa Rais na wako watu wa muhimu nawenye uwezo mkubwa sana kwenye ule Mfuko wa Mazingira. Lakini mfuko huu ulitengewa shilimhi bilioni mbili mpaka leo tunavyozungumza, Serikali imetoa shilingi milioni 34 tu kwa ajili ya huo Mfuko wa Mazingira, sasa katika hali kama hiyo tunapigaje hatua. Ukienda kuangalia kwenye eneo hilo la kilimo tuna Benki inaitwa ya Kilimo hapa, hiyo Banki ya Kilimo inafanya nini, Serikali imeipa nguvu kiasi gani ili iweze kufanya mapinduzi ya kilimo katika nchi hii, nimeangalia wametoa mikopo ya kama shilingi bilioni 6.5 kwa watu 2000 na kitu maana yake ni wastani wa kama shilingi milioni 2.6 kwa mtu mmoja. Tunaweza tukafanya mapinduzi ya kilimo katika nchi hii kwa stahili ya namna hiyo!

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kule Moshi kulikuwepo na mradi unaitwa Moshi Lower Irrigation Scheme ambao huu uligharamiwa na Wajapani, baada ya Wajapani kuondoka ekari ambazo zilikuwa zimekwishatayarishwa na kujengewa miundombinu zilikuwa 1,100 na zilikuwa na uwezo wa kuhudumia watu zaidi ya 4,500 leo hii tunapozungumza kutokana na uchakavu, kutokana na mabadiliko ya tabianchi leo ni ekari 417 tu ambazo zinatumika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni wazi kwamba tunarudi nyuma hatupigi hatua na kama Serikali haitachukua hatua za makusudi za kuwekeza kwenye maeneo kama haya na kuangalia maeneo ya miradi ya namna hiyo katika nchi nzima tutaendelea kuwa maskini na hatuwezi kufanya hatua yoyote. Tukienda kwenye uchumi wa viwanda, ni lazima tukubaliane na watu wengi hapa wamezungumza kwamba tunataka kujenga uchumi wa aina gani, uchumi wa kijamaa au wa kibepari au wa kati, kwa sababu ukiangalia tunazungumza kuwa tunataka kujenga uchumi wa viwanda lakini unaona kwamba Serikali bado inarudi kule ambapo tulishatoka miaka mingi. Leo hii Serikali inamiliki TTCL kwa 100%, leo hii Serikali inamiliki kiwanda cha General Tyre kwa 100%, leo hii TBA inafanya kazi za ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi wajibu ule wa Serikali ambao tunauzungumza wa kujenga mazingira wenzeshi, unaendanaje na hali kama hii? Lakini tunazungumza uchumi wa viwanda tumetenga maaneo kwa miaka mingi EPZ na ZSS, na baada ya kuyatenga hakuna hatua za makusudi na uwekezaji wa makusudi katika hayo maeneo kwa ajili ya kujenga miundombinu, kwa ajili ya kuyafanya yale mazingira yaweze kuwa wezeshi, kwa ajili ya kulipa fidia hakuna hatua ambazo za kulizisha. Matokeo yake ni kwamba tunatarajia wawekezaji waje, wajenge barabara, waweke umeme na waweze kujenga viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri atuambie ni mtu exposed sana na sina matatizo naye, ni wapi hapa duniani hata kule China ambapo ardhi ilitengwa halafu...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)